Tuesday, August 8, 2017

VETA YANG’ARA NANENANE KWA TAASISI ZA MAFUNZO YA FUNDI STADI

Na Chalila Kibuda, Lindi

Kwa mara nyingine tena Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imepata ushindi wa kwanza kwenye kundi la Taasisi za Utafiti na Mafunzo katika maonesho ya Wakulima Nanenane, 2017 yaliyokuwa yakifanyika kitaifa kwenye uwanja wa Ngongo mkoani Lindi.

Baada ya kutangazwa mshindi katika sherehe za ufungaji rasmi wa Maonesho, VETA imekabidhiwa kombe na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika shughuli za ufungaji wa maonesho hayo zilizofanyika leo 8 Agosti, 2017. 

VETA ilifuatiwa na Chuo cha Maji katika nafasi ya pili na Chuo cha Uhasibu Arusha ambacho kilishika nafasi ya tatu katika kundi hilo. Kaulimbiu ya maonesho hayo ilikuwa, "Zalisha kwa Tija Mazao na Bidhaa za Kilimo, Ufugaji na Uvuvi ili kufikia Uchumi wa Kati." 

Katika maonesho hayo, VETA ililenga kutoa taarifa na kuhamasisha wananchi kutumia fursa mbalimbali za mafunzo ya ufundi stadi ili kuboresha shughuli za kilimo, ufugaji na uvuvi, hivyo kuzalisha kwa tija. 

Vilevile VETA ilionesha ubunifu wa teknolojia bora na rahisi katika kilimo, mifugo na uvuvi na kwa ajili ya kuboresha maisha ya jamii ya wananchi wa kijijini. 

Mfano wa ubunifu na teknolojia ni pamoja na mashine za kufukuza ndege waharibifu wa mazao mashambani, vifaa vya kumwagilia, ujenzi wa nyumba kwa gharama nafuu, mashine za kisasa za usanifu wa nguo, jiko la kisasa linalotumia mafuta ya taa na nyinginezo. 

Katika maonesho hayo VETA imepokea wageni mbalimbali ikiwemo viongozi wa kitaifa ambao kwa pamoja walikiri kufurahishwa na juhudi zinazofanywa na vyuo vya ufundi stadi nchini hasa kupunguza tatizo la ajira kwa vijana nchini huku wakishauri kutanua wigo wa utoaji mafunzo ili kufikia makundi mengi zaidi. 

Mkuu wa JKT Meja Jenerali Michael Isamuhyo aliiomba VETA kushirikiana na jeshi hilo kuandaa mafunzo maalum ya ufundi stadi kwa vijana wanaojiunga na kambi za JKT katika maeneo mbalimbali nchini. Lengo la ombi hilo ni kuhakikisha kuwa vijana hao wakimaliza mafunzo ya jeshi watoke pia na ujuzi na vyeti vinavyotambulika na VETA na kukubalika kitaifa. 

Akizungumzia ushindi huo, Meneja Uhusiano wa VETA, Sitta Peter alisema, ni ishara kuwa jamii na mamlaka mbalimbali wanazidi kutambua na kuamini mchango muhimu unaotolewa na VETA. 

Aliwaasa wakulima na wanajamii kuendelea kutumia fursa mbalimbali za mafunzo zinazotolewa na VETA ili waweze kunufaika kwa kupata ujuzi utakaoweza kuwasaidia kuongeza tija katika uzalishaji na kujipatia ajira na kuongeza vipato vyao. 
Mkuu wa Chuo cha VETA Lindi akipeana mkono na Makamu wa Rais Samia Hassan Suluhu baada ya VETA kuchukua kikombe cha mshindi wa kwanza wa Taasisi Mafunzo ya Ufundi Stadi katika kilele cha maonesho ya Kitaifa ya Nanenane katika viwanja Ngongo mkoani Lindi.
Watendaji na Veta wakishangalia baada ya kupata kikombe cha mshindi wa kwanza wa Taasisi Mafunzo ya Ufundi Stadi katika kilele cha maonesho ya Kitaifa ya Nanenane katika viwanja Ngongo mkoani Lindi

No comments: