Saturday, August 5, 2017

Mradi wa Bomba la Mafuta Waurejesha Mkoa wa Tanga Katika Historia

Na: Judith Mhina – MAELEZO

Hakika historia imejirudia, mkoa wa Tanga ni kati ya mikoa mashuhuri nchini Tanzania kabla ya uhuru wa Tanganyika katika kupigania uhuru, kwa kuwa ni mkoa uliokuwa na wasomi wengi kuliko mikoa mingine wakati huo.

Hii ilitokana na uwepo wa shule za wamisionari wa kanisa la Anglikana (UMCA) ambalo ni la kwanza kuingia katika Pwani ya Afrika Mashariki mwaka 1878 na waliojenga shule za Magila na Kiwanda Muheza, Korogwe misheni, Kideleko Handeni (Shule za Kati) na Saint Andrew Minaki Pwani (shule ya Sekondari).

Hata baada ya uhuru chini ya Serikali ya Awamu ya Kwanza na ya Pili ya uongozi wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius K. Nyerere na Rais Msataafu Ali Hassan Mwinyi, mkoa wa Tanga ulikuwa maarufu kutokana na uwepo wa viwanda vingi, njia za reli na Bandari yenye kina kirefu yenye uwezo wa kuingiza meli kubwa za mizigo za Kitaifa na Kimataifa.

Viwanda ambavyo vilijengwa katika mkoa wa Tanga ni pamoja na vya chuma, mbolea, saruji, maziwa, kamba za katani na mazulia, amboni plastic, mbao, sabuni maarufu ya mbuni, gardenia, foma na mafuta ya nazi.

Historia hii sasa inajirudia katika mkoa wa Tanga baada ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt, John Pombe Magufuli, kupigania kwa nguvu zote Mradi wa ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kuja nchini Tanzania ambalo litaishia katika kijiji cha Chongoleani.

Wananchi wote wa Tanzania wana kila sababu ya kujivunia ujenzi wa bomba hilo la mafuta ambalo litawapatia ajira Watanzania hususan wananchi wa mkoa wa Tanga. Pongezi kubwa ziende kwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa juhudi zake za kuhakikisha kwamba Mradi huu unakuja Tanzania. Wananchi wa mkoa wa Tanga na Tanzania kwa ujumla wana kila sababu ya kulinda heshima ya nchi yetu kwa kuhakikisha kuwa kunakuwepo na ulinzi mkali wa Bomba hilo kila mahali lilikopita.

Kurejea kwa mkoa wa tanga katika ramani ya Tanzania ya viwanda umedhihirishwa na Wananchi wa Chongoleani ambao siku ya uwekaji jiwe la msingi walikuwa wawakilishi wa Watanzania ambao hawakupata fursa ya kwenda Tanga kumshuhudia Mheshimiwa Rais na na mgeni wake Rais wa Jamhuri ya Uganda Yoweri Kaguta Museveni wakifungua pazia la jiwe la msingi kuashiria uzinduzi wa Mradi huo.

Kutokana na tukio hilo la uwekaji wa jiwe la msingi wana Chongoleani walitoa ya moyoni kwa kuonyesha furaha yao isiyo na kifani kupitia kwa Mwenyekiti wao wa kijiji Ndugu Mbwana Nondo wakisema; “Kwa moyo wa dhati kabisa tunamshukuru sana Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutujali Wananchi wake kwa kutuletea neema ya mradi huu wa bomba la mafuta”.

Aidha, Mwenyekiti huyo aliongeza kwa kusema kwamba, katika maisha yetu Wananchi wa Chongoleani hatutaweza kumsahau Mheshimiwa Rais kwa mambo mengi anayowafanyia Watanzania na Taifa kwa ujumla na itakuwa ni kumbukumbu kwa kizazi kijacho.

“Napenda kusisitiza kwamba tunamuahidi Rais, kuwa wote watakaopata fursa kwenye Mradi huu wa Bomba la Mafuta, watafanyakazi kwa bidii ili kujiletea maendeleo ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla”. Alihitimisha Bw Nondo.

Naye Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Bibi Ummy Mwalimu, amewaomba wanawake wa Mkoa wa Tanga kuchangamkia fursa zinazojitokeza, kutokana na uwepo wa mradi wa bomba la mafuta.

Akisisitiza kuhusu ajira hizo amesema; “Kwa wale wenye ujuzi wanaweza kupata ajira za kudumu katika mradi, ila kwa wale ambao hawana ujuzi wachangamkie fursa nyingine kama mama lishe ambapo mkoa unjulikana kwa kujua kupika mapishi yanayovutia walaji wengi”

Aidha, amewaasa wakulima kuona fursa ya kulima mazao ambayo yataliwa kwa wingi kwa watumishi watakaoajiriwa Tanga katika mradi wa bomba la mafuta. Mfano matunda na mbogamboga ambavyo ni sehemu ya kuimarisha lishe za watumishi hao watakao kaa Tanga.

Mradi wa Bomba la Mafuta ni ishara njema kwa Watanzania, Serikali na Taifa kwa ujumla maana inaonyesha dhahiri kukosekana kwa fursa kama hii kwa miaka mingi katika mkoa wa Tanga ni fundisho kwa Watanzania hususan Wananchi wa mkoa wa Tanga kama waswahili wasemavyo “usichezee shilingi chooni” ikiwa na maana shilingi ikitumbukia kuipata sio rahisi.

Kila jambo jema lina fursa zake, nalo bomba la mafuta limekuja na neema zake, mfano wana Chongoleani kupata barabara ya kilometa 8 inayowaunganisha na barabara kuu ya kutoka Tanga kwenda Horohoro. Hii ina maana kubwa kwa wana chongoleani kiuchumi, maana watakuwa na wepesi wa usafiri wa mabasi na malori. Hivyo, bidhaa zitokazo chongoleani sasa zitaenda Tanga na nje ya mkoa wa Tanga kwa urahisi. Mfano samaki, mazao ya chakula na mengineyo.

Wafanyabiashara wetu wachangamkie fursa iliyojitokeza watembelee eneo husika na kudadisi kipi wanachoweza kufanya biashara kwa ajili ya kuinua kipato chao binafsi na Taifa kwa ujumla.

Kama tujuavyo Taifa letu liko kwenye harakati za kuelekea katika uchumi wa viwanda, na kama ujuavyo Tanga ni Mkoa wenye kuzalisha matunda ya aina mbalimbali na mbogamboga kwa wingi, nazi, katani, mahindi, viazi, maharagwe, samaki, viungo kama tangawizi, iliki, pilipili manga, mdalasini, chai na mifugo kama ngombe mbuzi na kondoo wapo kwa makundi katika ranchi zinazotambulika na wale wanaofugwa kiasili.

Katika suala zima la bomba la mafuta ni muhimu mikoa yote ambapo bomba linapita kutambua na kujiandaa kuitumia fursa zilizopo na zitakazo jitokeza katika mikoa ya; Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma Morogoro na Tanga. Wilaya zitakazopitiwa na bomba hilo zipo 24 na vijiji zaidi ya 180, vitafahamishwa kwa usahihi hapo baadaye.

Kwa kuwa Wizara ya Nishati na Madini inahamasisha kwa pamoja na wadau mbalimbali ni vema kutumia mafunzo hayo, kujiimarisha na kuwa sehemu ya matokeo mazuri ya bomba husika.

Bomba la Mafuta la kutoka Hoima Uganda mpaka Tanga Chongoleani lina urefu wa Kilometa 1445 ambapo kwa upande wa Tanzania itakuwa na jumla ya kilometa 1115 na Uganda 330. Aidha, Mradi utatarajia kusafirisha mapipa laki mbili na kumi na sita elfu (216,000) kwa siku .

Kijiji cha Chongoleani ndio kituo cha mwisho ambapo mitambo mikubwa itasimikwa katika eneo hili kwa ajili ya kusukuma mafuta eneo la baharini ili, kuweka kwenye vyombo vya usafirishaji kusafirisha maeneo mbalimbali duniani ambayo Uganda watakuwa wamepata soko.

Tanzania itafaidika na mradi huu kutokana na kodi, tozo na mrahaba wa bomba la mafuta, itakayofanywa moja kwa moja na mradi huo. Faida nyingine ambazo, sio za moja kwa moja ni ajira, fursa za kufanya biashara katika mikoa 8 ambayo ni Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora, Singida, Dodoma, Morogoro na Tanga.

Tusisahau unapopata fursa moja, ni vema kuitumia kwa kuimarisha na kuitangaza Tanga kimataifa kwa upande wa utalii katika machimbo ya Amboni, utalii wa samaki adimu duniani Silikanti eneo la ufukwe wa Kigombe. Samaki huyu alikuwepo duniani miaka 6000 iliyopita, ambapo alitoweka na kugundulika kuwa yupo katika pwani ya bahari ya hindi eneo la Kigombe Muheza Tanga.

Aidha, utalii wa milima ya Usanbara na Nnguu Kilindi, misitu ya asili ambayo kama vile miti ya miwati inayotengeneza nta au gundi, Tao la Mashariki misitu ya asili ya Nguu na maporomoko ya maji katika Tao la mashariki ikiwa ni pamoja na milima ya usambara, amani, maghamba, na nguu. Uoto wa asili na baridi ambayo isingedhaniwa kabisa kuwepo katika milima inayoelekea bahari ya Hindi.

Pia Hifadhi ya Taifa ya wanyamapori ya Saadani yenye kivutio cha ngiri wanaoishi katika makazi ya binadamu ambayo ni mbuga pekee iyopo pembezoni mwa bahari katika Afirka mashariki, pia mbuga ya Mkomazi na mbuga ya uwindaji wanyapori ya Nnguu, madini ya aina mbalimbali, Kasa wa pembezoni mwa ufukwe wa bahari ya Hindi na vipepeo adimu duniani wa milima ya usambara Amani. Ni vema kuwakarimu wageni kwa utamaduni wa asili wa Tanga kwa kuwaonyesha mapishi na ukarimu uliotukuka wa Watanzania wapatapo wageni. 


Mungu Ibariki Tanzania na watu wake.

No comments: