Sunday, August 20, 2017

DKT ANGELINE LUTAMBI AZINDUA “IKUNGI ELIMU CUP 2017” AMFAGILIA DC MTATURU KWA UBUNIFU

Na Mathias Canal, Singida
 
SERIKALI imekuwa ikifanya jitihada za dhati katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya elimu nchini ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya elimu ikiwemo ujenzi wa vyumba vya madarasa, Nyumba za walimu, Maabara, Matundu ya vyoo na mabweni.

Ili kunusuru kadhia hiyo imeelezwa kuwa moja ya mikakati ni pamoja na wakuu wa Wilaya kuwashirikisha wananchi pamoja na wadau wa elimu kuchukua hatua madhubuti ili kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa watoto na hatimaye kuwafanya wanafunzi wawe na furaha na amani. 

Hayo yameelezwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi wakati akihutubia mamia ya wananchi wa Wilaya ya Ikungi waliojitokeza katika hafla ya uzinduzi wa Mashindano ya Mpira wa miguu yanayojulikana kama “IKUNGI ELIMU CUP 2017” itakayofanyika katika vijiji vyote 101 vilivyopo katika wilaya ya Ikungi.

Mashindano hayo yaliyoanza leo Agosti 19, 2017 katika Uwanja wa Shule ya Sekondari Ikungi yanataraji kufika ukomo siku ya Jumanne Septemba 19, 2017 kwa matazamio ya kuwafikia zaidi ya wanachi 5000 katika Wilaya hiyo.

Dkt Lutambi alisema kuwa Mashindano hayo yenye kauli mbiu isemayo “CHANGIA, BORESHA ELIMU IKUNGI” yamebeba mtazamo chanya wa elimu wenye manufaa kwa wananchi katika kizazi cha sasa kuelimika na kizazi kijacho.

Alitumia nafasi hiyo pia kumpongeza Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu huku akiwaeleza wananchi kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli alichagua mtu muhimu kumuwakilisha katika Wilaya hiyo kwani ubunifu wake katika utendaji una manufaa makubwa kwa wananchi na jamii kwa ujumla.

Awali akisoma taarifa ya uzinduzi wa Mashindano hayo, Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu alisema kuwa mashindano hayo ambayo yatakuwa yanalenga kuhamasisha wananchi na wadau mbalimbali kuchangia vitu mbalimbali kwa ajili ya kuboresha changamoto zinazoikabili sekta ya elimu katika Wilaya ya Ikungi ikiwemo upungufu wa nyumba za walimu, maabara ya masomo ya sayansi kwa shule za sekondari, Madarasa kwa shule za msingi pamoja na vifaa vya kujifunzia.

Sambamba na mashindano hayo ya mpira wa miguu lakini pia umezinduliwa ufyatuaji wa matofali kwa ajili ya ujenzi wa maabara ya masomo ya Sayansi ambazo zipo katika hatua za msingi kwa muda mrefu.

Aidha, zimetolewa zawadi kwa wanafunzi waliopata daraja la kwanza (Division One) katika matokeo ya mtihani wa Taifa wa kidato cha sita mwaka huu 2017 na walimu wao ikiwa ni ahadi iliytolwa na mkuu wa wilaya hiyo.

Mhe Mtaturu aliahidi kutoa shilingi laki moja kwa kila mwanafunzi atakayepata Daraja la Kwanza na shilingi milioni moja kwa walimu kwa wanafunzi 10 watakaopata Daraja la Kwanza.

MWISHO


Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi akihutubia mamia ya wananchi wa Wilaya ya Ikungi waliojitokeza katika hafla ya uzinduzi wa Mashindano ya Mpira wa miguu ya “IKUNGI ELIMU CUP 2017”
Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi akihutubia mamia ya wananchi wa Wilaya ya Ikungi waliojitokeza katika hafla ya uzinduzi wa Mashindano ya Mpira wa miguu ya “IKUNGI ELIMU CUP 2017”
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akisoma taarifa ya “IKUNGI ELIMU CUP 2017” mbele ya Mgeni rasmi ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi wakati wa ufunguzi wa mashindano ya mpira wa Miguu.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akibeba tofali lililofyatuliwa na Mgeni rasmi ambaye ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi wakati wa ufunguzi wa mashindano ya mpira wa Miguu ya “IKUNGI ELIMU CUP 2017”
Katibu wa Chama Cha Mapinduzi Mkoa wa Singida Ndg Jimson Mhagama akibeba tofali lililofyatuliwa wakati wa ufunguzi wa zoezi la ufyatuaji matofali kwa ajili ya ujenzi wa maabara na madarasa.
Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akifyatua matofali wakati wa ufunguzi wa zoezi la ufyatuaji matofali kwa ajili ya ujenzi wa maabara na madarasa.
Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Ikungi akifyatua matofali wakati wa ufunguzi wa zoezi la ufyatuaji matofali kwa ajili ya ujenzi wa maabara na madarasa.
Kikosi cha Timu ya Ikungi United
 Kikosi cha Timu ya Puma Combine kilichoshinda goli 3 kwa 2 dhidi ya Ikungi United
Moja ya wanafunzi waliofanya vizuri katika mtihani wa kidato cha sita kwa kupata Daraja la kwanza akipokea shilingi 100,000 ikiwa ni ahadi ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji J. Mtaturu
Matofali ambayo yamefyatuliwa na wadau wakati wa ufunguzi wa ufyatuaji matofali Wilayani Ikungi


Mipira iliyotolewa kwa jili ya timu zote washiriki wa “Ikungi Elimu Cup 2017”


Mwenyekiti wa Mtandao wa Wazo huru Ndg Mathias Canal akiwa na watumishi mbalimbali kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Singida na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Ikungi


Kutoka kulia ni Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dkt Angeline Lutambi, Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji J. Mtaturu na kushoto ni Katibu wa CCM Mkoa wa Singida Ndg Jimson Mhagama wakifatilia mchezo wa ufunguzi wa Ikungi Elimu Cup 2017

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mhe Miraji Jumanne Mtaturu akimzuia mchezaji wa timu ya Madiwani wa Manispaa ya Singida asipite katika lango la Timu ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi wakati wa mchezo wa mapema kabla ya mchezo wa ufunguzi wa mashindano ya Ikungi Elimu Cupa 2017.

No comments: