Sunday, July 9, 2017

WAZIRI MWAKYEMBE APAMBA MAADHIMISHO YA MIAKA 100 YA DAR GYMKHANA

Mwenyekiti wa klabu ya Dar es salaam Gymkhana, Walter Chipeta akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 100 ya Klabu ya Dar es salaam Gymkhana yaliyofanyika jana jijini Dar es salaam. 
Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakeyembe akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 100 ya Klabu ya Dar es salaam Gymkhana yaliyofanyika jana jijini Dar es salaam. 
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akikabidhi kikombe kwa Nahodha wa mpira wa miguu wa Klabu ya Gymkhana Aliabid Mamdani (kulia) baada ya timu yake kuibuka washindi wa jumla katika michuano iliyofanyika hivi karibuni katika kuadhimisha ya miaka 100 ya klabu ya Gymkhana. Hafla ya makabidhiano ilifanyika jana wakati wa kilele cha maadhimisho hayo jijini Dar es salaam. Anayeshuhudia kushoto ni Mwenyekiti wa klabu ya Gymkhana Walter Chipeta.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe akisalimiana na Mwenyekiti wa zamani wa Klabu ya Dar Gymkhana, George Kritsos wakati wa hafla ya maadhimisho ya miaka 100 ya Klabu ya Dar es salaam Gymkhana yaliyofanyika jana jijini Dar es salaam. 



Klabu ya Dar es Salaam Gymkhana (DGC) ambayo ni miongoni mwa klabu kongwe za michezo hapa nchini Tanzania, leo imeadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwake kwa mtindo wa aina yake uliowakutanisha wadau mbalimbali wa klabu hiyo kupitia chakula cha jioni jijini Dar es Salaam.

Tangu wiki iliyopita, kumekuwa na shughuli mbalimbali za kimichezo ambazo zilianza kufanyika tangu 3 Julai na kilele chake kuwa siku ya leo ya tarehe (08/07/2017). Shughuli hizo ziliandaliwa kwa lengo la kupamba tukio hili muhimu.

Miongoni mwa michezo iliyokuwa ikifanyika ni pamoja na tenisi, kriketi, squash, mashindano ya gofu na michezo mingine mingi.

Mgeni rasmi aliyehudhuria sherehe ya kilele cha maadhimisho hayo wakati wa kufunga michezo hiyo, alikuwa ni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe ambaye alizungumiza shamrashamra za kuadhimisha miaka 100 ya klabu hii mkongwe.

“Binafsi nimefurahishwa sana kusikia kwamba michezo yote iliyohusishwa kwenye maadhimisho ya tukio hili kubwa na muhimu ambalo imefanyika na kuisha salama kwa kipindi chote cha wiki moja, jambo ambalo linaonyesha waandaaji walijapanga vyema. Ni imani yangu kwamba udhamini wa wadau mbalimbali umewezesha kufanikisha kufanyika michezo yote hii muhimu,” alisema Waziri Dk Mwakyembe.

Dk Mwakyembe alisema matarajio ya serikali ya awamu ya tano ni kuona wadau wanaongeza nguvu kujihusisha zaidi kwenye shughuli za michezo jambo ambalo linaweza kuibua vipaji zaidi kwa Watanzania wote.

Waziri Mwakyembe alimwaga pongezi kwa wanachama wote wa klabu hiyo wa sasa na wale waliopita pamoja na kila mtu ambaye alishiriki kwa nafasi yake kuhakikisha klabu ya Dar Gymkhana inafanikiwa zaidi.

“Ninatambua fikaumuhimu wa klabu hii kwa ngazi ya taifa letu kwani imekuwa miongoni mwa taasisi ambayo imekuwa ikihamasisha kukuza michezo, utalii na kuwakutanisha pamoja watu kwenye matukio ya kijamii,” alisema.

Waziri Mwakyembe aliwataka Watanzania kujenga utamaduni wa kushiriki michezo mbalimbali kwa ajili ya kuimarisha afya zao na kuwahamasisha wananchi kujiunga na klabu hii ambayo ina michezo mbalimbali. Alisema klabu hii imekuwa ikiwakutanisha wageni kutoka mataifa mbalimbali na Watanzania.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Dar es Salaam Gymkhana, Bw. Walter Chipeta alisema, 

“Tunayofuraha kubwa kusherehekea kutimiza miaka 100 ya uwajibikaji na mafanikio yetu makubwa tuliyoyopata kama klabu. Katika kuhakikisha kwamba tunaadhimisha tukio hili kwa aina ya kipekee, tuliona ni muhimu kuwaletea mashindano yaliyofanyika wiki nzima mfululizo kwa wanachama wa klabu hii waweze kushiriki na kujipatia zawadi mbalimbali.

Alisema mshindi wa jumla wa mashindo yote amepata ofa mbalimbali ikiwamo kujishindia safari iliyolipiwa kila kitu ya kwenda Dubai kwa kupitia Shirika la Ndege Qatar.

Bwana Chipeta alielezea furaha yake kwa kufikia hatua kubwa ya mafanikio ya kuadhimisha sherehe hii, akisema klabu kwa miaka mingi ya shughuli zake imekuwa kituo cha maendeleo ya aina zote za michezo na burudani ikiwamo kama vile soka, gofu, squash, kriketi, snooker, tenisi na mchezo wa kuogelea.

“Klabu ya Dar Gymkhana imeendelea kuwa imara. Nafikiri tunaweza kukubaliana kwamba kitu pekee katika maisha ni mabadiliko. Klabu hii imepitia misikusuko mbalimbali kipindi cha nyuma na imani yangu itafanikiwa zaidi kwa sababu ya uwezo wetu wa kuendana na mabadiliko yanayotokea,” alisema.

Alisema idadi ya wanachama imeongezeka tangu kuanzishwa kwake hadi kufikia zaidi ya wanachama 1,000 wakiwamo wanachama wa kudumu, wageni, wakaazi, wazalendo, waheshimiwa, watoto na wale wa muda.
Sherehe ya kuadhimisha miaka 100 ya klabu hii ilidhaminiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) pamoja na wengine; Qatar Airways, Clouds Media Group, ALAF, NMB, Eagle Africa Insurance brokers, BRITAM na Aqua Cool.


Kuhusu Klabu ya Dar es Salaam Gymkhana

Klabu hii ya michezo mbalimbali ilianzishwa mwaka 1916 ikiwa inaendeshwa na aliyekuwa Gavana wa Tanganyika Cameron. Klabu ya Dar es Salaam Gymkhana imekuwa ikijihusisha na michezo mbalimbali na kuwa kituo bora kwa michezo na buruduani kwa miaka mingi kama vile soka, gofu, squash,snooker, riketi, tenisi na kuogelea.

Wanachama wake wamekuwa wakiongezeka na kufikia 1,000 ikiwamo wale wenye uanachama kamili ambao ni wageni wanaoishi hapa nchini, wanachama waliopo nchini, wanachama wa heshima, wanachama wa muda, wanachama watoto na wanachama wa muda.

Licha ya kuwa na huduma za michezo pia Klabu ya Dar es Salaam Gymkhana ina sehemu ya baa, hoteli ili kuhakikisha huduma zote za vyakula zinapatikana muda wote kwa wanachama wake.

Kwa ujumla huduma za michezo zinazopatikana zinaendana na mazingira mazuri kutoka na mahali ilipo katikati ya jiji.

Klabu hiyo imekuwa kituo cha mambo mbalimbali ya kijamii ikiwamo mashindano Nyama Choma Festival yaliyofanyika mwaka 2014 na maaadhimisho ya July Mug mwaka 2014.

Katika sekta ya michezo, Dar Gymkhna imekuwa kiongozi wakati wote. Klabu imeshinda mataji ya mashindano mbalimbali kwenye michezo tofautitofauti ambayo huwa inashiriki ndani na nje ya Tanzania.

No comments: