Monday, July 31, 2017

VIJIJI VYOTE KUWA NA UMEME IFIKAPO 2021 –DKT. KALEMANI

Na Tiganya Vincent
Serikali imesema kuwa jumla ya vijiji 7873 na vitongoji vyake vyote hapa nchini vitakuwa vimeshaunganisha na umeme chini ya Mradi wa Umeme Vijijini Awamu wa Tatu ifikapo mwaka 2021.

Kauli hiyo imetolewa jana mjini Tabora  na Naibu Waziri wa Nishati na Madini Dkt. Medard Kalemani wakati alipomtembelea Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri.
Dkt. Kalemani alisema REA III itasaidia kukamilisha vijiji vilivyobaki ambavyo havijaunganishwa na umeme ifikapo mwaka 2021 kwa ajili ya kuchochea maendeleo ya uchumi kati kuelekea uchumi wa viwanda.
Alisema kuwa lengo la Serikali ni kutaka wananchi wote hata wale wanaoishi visiwani waweze kufikiwa na huduma ya umeme kwa ajili ya matumizi yao na kwa ajili ya uendeshaji wa viwanda.
Aidha kwa upande wa Mkoa wa Tabora alisema vijiji vipatavyo 510 na vitongoji vyake vinatarajiwa kuwa vimeshaunganishwa na umeme wa uhakika wa ifikapo mwaka 2021 kupitia mradi wa REA III.
Aliongeza kuwa ili kuhakikisha lengo hilo la kuunganisha vijiji vyote vinakuwa na umeme, Serikali imeamua kuweka Wakandarasi wengi katika kila mradi na kuwaagiza kugawa kazi kwa Wakandarasi wadogo ambao ni wazawa na wenye sifa ili kurahisisha kazi na kuifanya iwe na ufanisi.
Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri alisema kukamilika kwa mradi wa REA III utaufanya mkoa huo kukua kwa kasi zaidi na kutoa wito kwa wawekezaji kuja kuwekeza katika viwanda vya sekta mbalimbali ikiwemo za usindikaji wa mazao ya kilimo na mifugo na uchimbaji madini.
Alisema kuwa hivi sasa Mkoa huo unazidi kuimarika katika miundombinu ya barabara , reli , anga na upatikanaji wa maji  na umeme wa uhakika na hivyo kutokuwepo na vikwazo katika uzalishaji.
Uzinduzi wa uunganishwaji mradi wa umeme vijijini kwa awamu ya tatu unatarajiwa kufanyika tarehe 1 Agosti 2017 katika Wilaya ya Sikonge kwa niaba ya Wilaya zote za Mkoa wa Tabora.

No comments: