Thursday, July 20, 2017

SHAKA APONGEZA WAGANGA NA WAUGUZI MKOANI KIGOMA

Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) umesema serikali ya awamu ya tano itaendelea kuwajali na kuwahudumia wagonjwa kwa kupeleka idadi ya waganga, wauguzi, dawa na utoaji wa vifaa tiba katika zahanati vituo vya afya na hospitali za wilaya nchini .

Pia Serikali itafanya kila linalowezekana kuhakikisha katika kila Kata na Wilaya kunajengwa zahanati na vituo vya afya ili kunusuru pia kupunguza vifo vya kina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano .

Msimamo huo umetolewa jana na Kaimu Katibu Mkuu wa UVCCM Shaka Hamdu Shaka alipotembelea katika kituo cha Afya cha kijiji cha Nguruka Wilaya ya Uvinza Mkoani Kigoma katika siku ya pili ya ziara yake kuona utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya ccm katika maendeleo ya kisekta.
Shaka alisema serikali ya Chama Cha Mapinduzi zina wajibu wa kufuatilia kwa karibu na kujua kama yale yote yalioahidiwa katika ilani , yanayotimizwa na iwapo yanawafikia na kuwahudumia wananchi kama inavyokusudiwa na serikali Kuu kwa wananchi wake. 

Alisema pamoja na kukabiliwa na upungufu wa idadi ya Waganga na Wauguzi katika Kituo cha Afya Nguruka, waliopo wamekuwa wakijituma bila kuchoka huku wakitoa huduma kwa njia makini na sahihi ili kunusuru na kutibu wagonjwa . 

"Serikali ya CCM katu haitapuuzia dhamana waliopewa na wananchi kwa kuiweka madarakani kidemokrasia , maeneo yote ya kisekta yataendelea kupata huduma bora kwa wakati stahili hususan eneo la Afya kwa upelekaji vifaa tiba, dawa, Waganga na Wauguzi " Alisema Shaka .

Alisema katika kuonyesha serikali kujali matatizo ya wagonjwa hivi karibuni Rais John Magufuli amepeleka shilingi milioni kumi katika kituo cha Afya Nguruka kwa ajili ya kufanyika upanuzi wa wodi ya wazazi huku kanisa la shalom likijenga wodi hiyo. 
"Rais wetu hapati usingizi kwa raha kutokana na kufikiria wanachi wake, kila wakati amwkuwa akiwahimiza wataalam wa huduma za afya na watendaji dhamana wa serikali watimize wajibu wao bila kuchoka. Huuu ndiyo uungwana alionao kiongozi wetu na kila mmoja wetu sasa lazima awajibike 'Alisema Shaka mara baada ya kutazama wodi hiyo.

Aidha Kaimu huyo Katibu Mkuu wa UVCCM aliwataka watendaji wa halmashauri ya wilaya ya Uvinza kujiongeza katika mikakati ya ubunifu, utendaji unaoonekana na kujali maisha ya watu, matumizi bora ya fedha za ruzuku ya umma toka serikali kuu na kuhakikisha wanawatibia wagonjwa kwa wema. 

Kwa upande wake Mganga Mkuu Msaidizi wa Kituo cha Afya Nguruka Dk Beatrice Mtasigwa alimueleza Shaka licha kukabiliwa na upungufu wa Waganga na Wauguzi, wamekuwa wakiwahudumia wagonjwa mbalimbali toka vijiji vyote wanaofika kituoni kati 80 hadi 120 kwa siku. 

Dk Mtasigwa alisema hatua ya ujenzi na upanuzi wa wodi ya wazazi , uwepo wa badhi ya vifaa tiba vya kisasa utasaidia kwa kiasi kikubwa kunusuru maisha ya kina mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano. 

Naye Mbunge wa Vijana Mkoa Kigoma Zainab Katimba alitoa shilingi laki mbili na kumkabidhi Mganga Mkuu Msaidizi wa Kituo hicho cha Afya kusaidia kununulia shuka ambazo zitatumika katika wodi ya wazazi.

Katimba alisema bila kina mama hakutakuwa na Taifa kwasbabau nchi na mataifa yote yanajazwa na nguvu za kina mama ambazo ndiyo wazazi wanaoleta neema ya kupatikana watoto duniani , wataalam wa fani mbalimbali, viongozi, wabunge na wanasiasa.
Shaka anaendelea na ziara yake ya kikazi katika wilaya ya Kigoma Mjini kabla ya kuelekea Kibondo, kasulu, Buhigwe, Kakonko na Kigoma vijijini mkoani hapa.

No comments: