Tuesday, July 11, 2017

JAFO AWATAKA WAHANDISI KUSIMAMA IMARA KATIKA USIMAMIZI WA MIRADI

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Tamisemi Selemani Jafo amewataka wahandisi wa Halmashauri nchini kutumia taaluma zao ipasavyo katika usimamizi wa miradi mbalimbali ya ujenzi wa miundombinu katika halmashauri zao.

Jafo aliyasema hayo leo alipokuwa katika ziara maalum ya ukaguzi wa miradi ya barabara na madaraja katika Halmashauri ya wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.

Katika ziara hiyo, Jafo alikagua ujenzi wa barabara ya Lami ya kilometa moja katika mji wa Bahi inayojengwa na Ofisi ya Rais Tamisemi kupitia mfuko wa barabara.

Jafo alisema maagizo ya kuzingatia ubora wa barabara inayo jengwa ili iweze kudumu kwa muda ulio kusudiwa.Katika ukaguzi wa madaraja, Jafo alikagua ujenzi wa madaraja mawili ya Nkulugano na Chipanga pia daraja la barabara ya Chipanga- Kigwe yanayojengwa kwa mradi maalum wa kuondoa vikwazo kwa ufadhili wa fedha za DFID.

Jafo alimpongeza mhandisi wa halmashauri ya Bahi Eng. Geofrey Mkinga kwa usimamizi mzuri wa kazi hizo zinazoendelea.Akihitimisha ziara yake, Naibu Waziri Jafo aliwataka wahandisi wa halmashauri zote hapa nchini kusimamia ubora wa kazi za ujenzi kwa umakini na kuweka mbele maslahi ya Taifa.

Madaraja hayo mawili yanatarajiwa kukamilika mwezi oktoba mwaka huu na yatakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wanaotumia barabara hizo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Bahi Omary Badwel ameishukuru sana serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk.John Magufuli kwa kuwa madaraja hayo yalikuwa ni kikwazo kikubwa sana kwa maendeleo ya wananchi wa jimbo hilo.

No comments: