Friday, June 9, 2017

Wasindikaji Wadogo 1287 Wanufaika na TFDA

Na Frank Mvungi-Maelezo

Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imetoa mafunzo kwa wasindikaji wadogo wa vyakula 1287 tangu mwaka 2013 ili waweze kusindika vyaklula vyenye ubora kwa mujibu wa sheria na kanuni za uzalishaji na kuhimili ushindani wa soko.

Akifungua mafunzo ya wasindikaji wadogo wapatao 60 wa vyakula yaliyoratibiwa na Mamlaka hiyo leo jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Hiiti Sillo, Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula Bw. Raymond Wigenge, amesema dhamira ya Serikali ni kuwawezesha wajasiriamali wadogo hapa nchini.

“Kukua kwa viwanda hivi kutakuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ajira na kipato katika ngazi ya kaya, kukuza kilimo cha mazao ya chakula kutokana na kuwepo kwa soko la mazao ya vyakula”. Alisisitiza Wigenge.

Akifafanua Wigenge amesema Serikali inatambua kuwa viwanda vidogo vina nafasi kubwa ya kuchangia pato la Taifa hasa katika kipindi hiki ambacho Serikali inasisitiza ujenzi wa uchumi wa Viwanda.

Alieleza kuwa Mamlaka hiyo imeingia mkataba wa maridhiano (MOU) na Shirika la Viwango Tanzania (TBS) ambapo mchango wa taasisi hizo mbili utatambuliwa katika tasnia ya ujasiriamali wa bidhaa zinazodhibitiwa na Mamlaka.

“Katika makubaliano tuliyofikia kati ya TFDA na TBS ambapo kuanzia sasa mamlaka yetu itatumia matokeo ya vipimo vya maabara za TBS kusajili bidhaa husika na TBS itazingatia usajili wa TFDA wa jengo la bidhaa wakati wa kutoa alama ya ubora”. Alisisitiza Wigenge.

Akizungumzia umuhimu wa mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Chama Kuweka na Kukopa cha Wajasiliamali Wadogo Wanawake Tanzania (TASWE) na mwakilishi wa wanawake wajasiriamali Bi. Anna Matinde amesema kuwa mafunzo kwa wajasiriamali wadogo yana umuhimu katika kuchochea maendeleo ya Viwanda hapa nchini.

“Sasa tumeona juhudi za Serikali katika kuwawezesha wajasiriamali wadogo hapa nchini na tunapongeza hatua hizi ikiwemo kuandaa mafunzo haya na tumeona kweli kuna mabadiliko makubwa katika kuwawezesha wajasiriamali”. Alisisitiza Matinde.

Alieleza kuwa kwa ni vyema wajasiriamali wakaunga mkono juhudi hizo ili waweze kunufaika na uwezeshwaji unaofanywa na Serikali kwa wajasiriamali wote bila kujali ni wadogo au wa kati na hata wakubwa.Mada zilizowasilishwa katika mafunzo hayo ya siku moja ni pamoja na taratibu za usajili wa majengo ya vyakula, usajili wa vyakula, utaratibu wa utoaji wa alama ya ubora na teknolojia ya usindikaji wa vyakula.

Mafunzo hayo yamefanyika katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma, Rukwa, Manyara, Lindi,Mtwara,Tanga, Singida, Iringa, Kigoma, Kilimanjaro, na Morogoro.
Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Bw. Raymond Wigenge akifungua mafunzo ya wasindikaji wadogo wa vyakula (hawapo pichani) ambayo yaliatibiwa na Mamlaka hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Ukaguzi na Ufuatiliaji wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Bw. Justin Makisi akitoa ufafanuzi kuhusu umuhimu wa mafunzo kwa wasindikaji wadogo wa vyakula.
Mwenyekiti wa Chama cha Kuweka na Kukopa Wajasiriamali Wadogo Tanzania (TASWE) na muwakilishi wa wanawake wajasiriamali Bi. Anna Matinde akipongeza juhudi za Serikali katika kuwawezesha wajasiriamali wadogo hapa nchini. Kulia ni Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula wa Mamlaka hiyo Bw. Raymond Wigenge na kushoto ni Afisa Udhibiti Ubora Bi. Prisca Kuela
Baadhi ya wajasiriamali wakifuatilia mafunzo yaliyoratibiwa na Mamlaka ya Chakula na Dawa Nchini (TFDA) kwa wasindikaji wadogo wa vyakula .
Mkurugenzi wa Usalama wa Chakula wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Bw. Raymond Wigenge akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo Bw. Hiiti Sillo wakati wa mafunzo ya wasindikaji wadogo wa vyakula.(Picha zote na Frank Mvungi-Maelezo)

No comments: