Wednesday, June 14, 2017

WADAU WA KILIMO WAKUTANA KUJADILI MIKAKATI YA KUBORESHA UWEZESHAJI KWENYE KILIMO NA VIWANDA

Katika kuhakikisha dhamira ya Serikali ya dhamira ya Serikali ya kujenga Uchumi wa Viwanda wadau wa kilimo na viwanda wamekutana ili kuzungumzia nafasi ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB) katika  kuhakikisha Benki hiyo inasaidia sekta ya Kilimo nchini.

Wakizungumza katika Kikao hicho kilichoandaliwa na TADB ili kujadili mikakati ya kuboresha uwezeshaji kwenye kilimo na viwanda nchini.
Akizungumza katika kikao hicho Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga amesema kuwa Benki imejipanga kuleta matokeo makubwa kwenye mapinduzi ya kilimo na viwanda hasa vya uchakakataji na usindikaji wa mazao ya kilimo.

Bw. Assenga amesema kuwa mipango hii itasaidia upatikanaji wa mali ghafi kwa viwanda vya ndani hivyo kusukuma ndoto ya Serikali kufikia lengo lake la Kujenga Uchumi wa Viwanda na kuhuisha uwekezaji kwenye Viwanda vidogo vidogo na vya kati vya usindikaji na uchakataji wa mazao ya Kilimo na mifugo.

“Benki imejikita kwenye kusaidia Sekta ya Kilimo iweze kusukuma dhamira ya Serikali ya Uchumi wa Viwanda uweze kutoa matunda yaliyokusudiwa ili kuchagiza na kusaidia Mapinduzi ya Kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda cha kibiashara ili kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini,” alisema.

Bw. Assenga amesema katika kuhakikisha azma hiyo inatimia TADB imejipanga kutoa elimu ili kuwajengea uwezowakulima na taasisi mbali mbali za fedha pamoja na vyama vya ushirika kuweza kukopa toka TADB pamoja na kushirikiana na wadau mbali mbali kusaidia uwekezaji mkubwa kwenye Sekta ya Kilimo ili iweze kuinua pato la Taifa na kumkomboa Mwananchi.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji huyo ameongeza kuwa TADB imeanza kujiimarisha  na kuchochea mabenki na taasisisi za fedha kuongeza utoaji wa mikopo na fedha zingine kwenye Sekta ya Kilimo ili kuongoza utoaji mikopo ya uongezaji wa thamani katika shughuli za kilimo.

TADB ni taasisi ya serikali ambayo ilianzishwa kwa ajili ya kutatua ufinyu mkubwa wa upatikanaji wa fedha mikopo kwa ajili ya maendeleo ya kilimo nchini ambao ulikuwa unachangiwa kwa kiasi kikubwa na mikopo mingi kutoka taasisi za fedha kuelekezwa zaidi kwenye upande wa biashara za bidhaa; riba kubwa kwenye mikopo ya kilimo; mikopo ya muda mfupi; masharti magumu ya kukopa bila kuzingatia hali halisi ya sekta ya kilimo  na mazao ambayo inaathiriwa kwa kiasi kikubwa na mabadiliko ya hali ya hewa.
 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB), Bibi Rosebud Kurwijila (kushoto) akizungumza na aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mzee Peniel Lyimo (kulia) wakati wa Kikao cha Wadau wa Kilimo Kujadili Mikakati Ya Kuboresha Uwezeshaji Kwenye Kilimo Na Viwanda kinachofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) Dar es Salaam.
 Mwenyekiti wa Kamati ya Biashara ya TADB, Bibi Rehema Twalib (kulia) akizungumza wakati wa Kikao cha Wadau wa Kilimo Kujadili Mikakati Ya Kuboresha Uwezeshaji Kwenye Kilimo Na Viwanda kinachofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNICC) Dar es Salaam.
 Aliyewahi kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Mzee Peniel Lyimo (kulia) akiongoza Kikao hicho.
 Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Francis Assenga (kushoto) akisisitiza nafasi ya Benki yake katika kuleta matokeo makubwa kwenye mapinduzi ya kilimo na viwanda hasa vya uchakakataji na usindikaji wa mazao ya kilimo.
 Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa TADB wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi, Bibi Rosebud Kurwijila (kushoto) wakifuatilia kwa makini Kikao hicho.
 Washiriki wa Kikao hicho wakifuatilia mawasilisho mbali mbali wakati wa Kikao cha wadau wa kilimo waliokutana kujadili mikakati ya kuboresha uwezeshaji kwenye kilimo na viwanda. Kikao hicho kiliandaliwa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ya Tanzania (TADB).
Wadau wa kilimo waliokutana kujadili mikakati ya kuboresha uwezeshaji kwenye kilimo na viwanda wakiwa katika picha ya pamoja.

No comments: