Monday, June 5, 2017

UNESCO YATAKA WANANCHI KUENZI URITHI WA DUNIA KWA KUTEMBELEA

Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO, Bi. Irina Bokova, katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani, leo ametaka wananchi mbalimbali kutenga muda binafsi na kutembelea moja ya maeneo ambayo ni urithi wa dunia yakifadhiliwa na UNESCO.

Amesema anaamini kuwa kwa wananchi kushiriki watashawishika kuendelea kuishi kwenye maeneo hayo na kuyaenzi.

Amesema kitendo hicho kidhati kitakuwa kimewaunganisha watu na asili na hivyo kuondoa dhana ya zamani ya kuweka maeneo hayo mbali na watu.

“Inaweza kuwa vigumu kuamini sasa, lakini miaka hamsini iliyopita ilidhaniwa kuwa njia bora ya kulinda asili ni kuiweka mbali na watu ...Hii leo, tunajua vyema zaidi kwamba kwa kadri uhusiano baina ya watu na mazingira yao unavyokuwa wa karibu zaidi ndivyo watu wanavyofahamu zaidi juu ya umuhimu wa asili na viumbe hai, urithi na maji, kwa ajili ya ustawi wao binafsi na kwa ajili ya hali ya baadaye ya sayari yetu.” Alisema.

Mkuu huyo alisema hayo akizungumzia umuhimu na uhifadhi kwa maeneio zaidi ya 2000 duniani ya bayongahewa, maeneo ya hifadhi ya jiolojia ya na maeneo ya Urithi wa Dunia yanayodhaminiwa na UNESCO.

Alisema maeneo hayo pamoja na kuhifadhi urithi wa dunia pia hutoa ajira kwa watu wanaoyazunguka na milango yake iko wazi kwa umma wote.

“Maeneo ya hifadhi ya jiolojia ni vitabu vilivyo wazi vya kihistoria ambavyo huturudisha nyuma mamilioni ya miaka. Hifadhi za Bayongahewa ni mahali ambapo jamii hukabiliana na changamoto za maendeleo kwa kuunda njia mpya za kijamii na uchumi endelevu. Maeneo ya hifadhi ya jiolojia na hifadhi za Bayongahewa huunganisha uhifadhi na elimu kwa mbinu mpya ya maendeleo endelevu, kama vile utalii wa mazingira na kilimo hai.” alisema katika ujumbe wake kwa dunia.

Aliwataka wananchi kuheshimu mazingira ya asili hutokana na uelewa.

Aliwataka wananchi kupitia katika tafakari ya kina kujitumbukiza katika Bustani ya Kiajemi ya Iran ambako maji hufanya ishara za maumbo ya mapambo mbalimbali.

Aidha alisema vyema kuona eneo la hifadhi ya jiolojia la UNESCO la Tumbler Ridge nchini Canada, na kuogelea katika maziwa ya Alpine yenye maji angavu kama kioo na kulala chini ya nyota.

Pia amewataka kufanya safari ya kutembea kwa miguu katika hifadhi ya Bayongahewa ya Mujib huko Jordan ambayo ipo mita 420 chini ya usawa wa bahari ikiwa karibu wake na Bahari ya Chumvi.

Mkuu huyo wa Unesco ametaka wakazi wa dunia hii wakati wakiadhimisha Siku ya Mazingira Duniani, kutumia ipasavyo maeneo teule ya UNESCO kila mahali kuungana na asili inayowazunguka na inayoleta uzuri, maana na amani katika maisha.

No comments: