Monday, June 5, 2017

RAS SHINYANGA AFUNGUA MAFUNZO YA MFUMO WA UHASIBU NA UTOAJI TAARIFA ZA FEDHA KWA NGAZI YA KITUO CHA KUTOLEA HUDUMA - FFARS

Mafunzo hayo ya siku mbili Juni 5 na 6, 2017, yanafanyika katika ukumbi wa Vigirmark Hotel mjini Shinyanga, na yamekutanisha wadau mbalimbali wakiwemo wawakilishi kutoka PS3, TAMISEMI, Wizara ya Afya, Wizara ya Elimu, na wakufunzi kutoka mikoa mbalimbali ambako mradi unatekelezwa. 

Akizungumza wakati wa kufungua mafunzo hayo, Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, alisema mfumo wa FFARS utasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha kuwa vituo vya kutolea huduma vinakusanya na kuhifadhi taarifa za mapato na matumizi zilizotengwa na Serikali kwa ajili ya kusaidia maendeleo ya vituo hivyo ili wananchi waweze kupata huduma bora. 

“Ikumbukwe kuwa Mheshimiwa Rais katika kutekeleza mpango wa elimu bila malipo aliamuru kuwa fedha za ruzuku za gharama za uendeshaji wa shule lakini pia vituo vya kutolea huduma zitapelekwa moja kwa moja katika vituo hivyo, hivyo basi usimamizi wa ruzuku hizo utafanywa na vituo husika,” alieleza Msovela. 

“Lengo la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo ili kuhakikisha kuwa vituo vyetu vya kutolea huduma kupitia fedha za ruzuku vinakuwa na mfumo maalum wa kuandaa taarifa za mapato na matumizi, hali ambayo itachangia uwajibikaji na utoaji wa huduma bora kwa wananchi,” aliongeza Msovela. 

Aidha, alisema Serikali inatambua kazi nzuri inayofanywa na PS3 katika kuunganisha wadau, na kuongeza kuwa ni wakati mzuri watanzania wakaiga mfano wa nchi kama Marekani ambao wapo mbele zaidi katika masuala ya uwazi na utawala bora katika kuwapa taarifa wananchi zinazohusu maeneo yao. 

Awali akizungumza katika mafunzo hayo, Mkuu wa Idara ya Ufuatiliaji, Tathmini na Tafiti Tendaji kutoka PS3, Dkt. Suma Kaare, alisema mfumo wa mpya wa uhasibu na utoaji taarifa - FFARS unafadhiliwa na Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Marekani (USAID) kupitia Mradi wa Uimarishaji wa Mifumo ya Sekta za Umma (PS3). 

“Tumeandaa mafunzo ya kina kwa wakufunzi 490 katika ngazi ya taifa na halmashauri, yatakayofanyika mikoa minne nchini: Dodoma, Mbeya, Mtwara na Shinyanga, ili kuwawezesha watumishi katika vituo vya afya na elimu kupata ujuzi wa namna ya kutumia mfumo mpya wa FFARS,” alifafanua Dkt. Kaare. 

“Wakufunzi hawa wataweza kutoa elimu hii kwa watumiaji wa mwisho wa mfumo wa FFARS katika zaidi ya vituo vya afya 550, zahanati 6800, hospitali za wilaya 135 na takribani shule za msingi na sekondari 20,000 katika mikoa 26 ya Tanzania bara, vikiwemo vituo vya kutolea huduma kutoka mikoa 13 na halmashauri 93 zinazotekeleza mradi wa PS3,” aliongeza Dkt. Kaare. 

Katika hatua nyingine, alisema FFARS itaweza kufuatilia matumizi ya fedha zinazotolewa na Serikali katika kufikia malengo ya utoaji huduma na kuhakisha yanaendana na sheria ya manunuzi na utoaji taarifa, ili kuisaidia Serikali kuimarisha mfumo wa usimamizi wa fedha za umma na kuongeza uwazi na watoa huduma kuwa na wajibu kwa jamii wanayoihudumia. 

Naye Afisa Msimamizi wa Fedha Mwandamizi kutpka TAMISEMI, Elisa Rwamiago, alisema mfumo wa FFARS utaanza kutumika kuanzia Julai 1, 2017, ambapo Serikali itaanza kupeleka rasilimali fedha moja kwa moja kwenye vituo vya afya kwa ngazi za halmashauri.

“Vituo vya kutolea huduma vitakavyopokea fedha hizo ni pamoja na zahanati, vituo vya afya, na hospitali za wilaya. Zoezi hili ni sambamba na inavyotekelezwa kwenye sekta ya elimu, serikali za vijiji na ofisi za kata,” alieleza Rwamiago. 

Mwandishi wetu, Kadama Malunde, ametuletea picha za matukio yaliyojiri wakati wa mafunzo hayo siku ya kwanza Jumatatu, Juni 5, 2017 .
Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, amefungua mafunzo ya mfumo mpya wa uhasibu na utoaji taarifa za fedha kwa ngazi ya kituo cha kutolea huduma ‘Facility Financial Accounting and Reporting System – FFARS) kupitia mradi wa Uimarishaji wa Mifumo ya Sekta za Umma ‘ Public Sector Systems Strengthening – PS3’.
Mgeni rasmi, Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, akifungua mafunzo kuhusu mfumo mpya wa uhasibu na utoaji taarifa za fedha kwa ngazi ya kituo cha kutolea huduma ‘Facility Financial Accounting and Reporting System – FFARS) katika ukumbi wa Vigirmark Hotel mjini Shinyanga 
Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, akifungua mafunzo mafunzo kuhusu mfumo mpya wa uhasibu na utoaji taarifa kwa wakufunzi zaidi ya 130 kutoka mikoa ya kanda ya ziwa na kati waliohudhuria mafunzo hayo 
Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, akizungumza ukumbini. Kulia ni Afisa Msimamizi wa Fedha Mwandamizi TAMISEMI, Elisa Rwamiago, na kushoto ni Mkuu wa Idara ya Ufuatiliaji, Tathmini na Tafiti Tendaji kutoka PS3, Dkt. Suma Kaare 
Katibu Tawala mkoa wa Shinyanga, Albert Msovela, alisema wananchi wana haki ya kuhoji pale ambapo mambo yanakuwa hayaendi sawa na serikali ina wajibu wa wananchi inayowatumikia hivyo kuwataka wakufunzi hao kutumia mafunzo wanayopatiwa kutoa elimu kuwapa pia watu wengine 
Mkuu wa Idara ya Ufuatiliaji, Tathmini na Tafiti Tendaji kutoka PS3, Dkt. Suma Kaare akizungumza wakati wa ufunguzi
Mkuu wa Idara ya Ufuatiliaji,Tathmini na Tafiti Tendaji kutoka PS3, Dkt. Suma Kaare akizungumza ukumbini 
Afisa Msimamizi wa Fedha Mwandamizi TAMISEMI, Elisa Rwamiago, akielezea kuhusu umuhimu wa mfumo mpya wa uhasibu na utoaji taarifa za fedha kwa ngazi ya kituo cha kutolea huduma ‘Facility Financial Accounting and Reporting System – FFARS) 
Afisa Msimamizi wa Fedha Mwandamizi TAMISEMI, Elisa Rwamiago, akielezea jambo kwa washiriki wa mafunzo hayo 
Kaimu Mratibu wa Mradi wa PS3 mkoa wa Shinyanga, Glory Mbia akizungumza wakati wa mafunzo hayo 
Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea ukumbini 
Washiriki wa mafunzo hayo wakiwa ukumbini 
Mshauri wa Masuala ya Usimamizi wa Fedha za Umma kutoka Mradi wa HPSS Dodoma, Elezeus Rwezaula, akitoa mada wakati wa mafunzo hayo 
Mshauri wa Masuala ya Usimamizi wa Fedha za Umma kutoka Mradi wa HPSS Dodoma, Elezeus Rwezaula, akielezea kuhusu mfumo wa FFARS 
Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia mada 
Washiriki wa mafunzo hayo wakifuatilia mada ukumbini 
Mafunzo yanaendelea 
Washiriki wa mafunzo wakisikiliza kwa makini kilichokuwa kinaendelea ukumbini 


Picha zote na Kadama Malunde- Malunde1 blog

No comments: