Monday, June 5, 2017

BENKI YA NMB YAIKABIDHI SERIKALI GAWIWO LA SHILINGI BILIONI 16.5

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Philip Isdor Mpango (Mb) (kushoto) akipeana mkono na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB , Ineke Bussemaker (kulia) baada ya kupokea mfano wa hundi wa gawiwo la shilingi bilioni 16.5 ambazo Serikali kama mwanahisa imepata katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa wanahisa wa Benki hiyo uliofanyika Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NMB, Ineke Bussemaker akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mafanikio ya Benki hiyo ambayo kwa mwaka ulioishia Disemba 31,2016 ilipata faida ya shilingi bilioni 153.8 licha ya changamoto za kibenki, likiwa ni ongezeko la asilimia 2, ukilinganisha na mwaka 2015 ambapo ilipata faida ya shilingi bilioni 150.3.
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Philip Isdor Mpango (Mb) akiishukuru Benki ya NMB kwa kutoa gawiwo la shilingi bilioni 16.5 kwa Serikali wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa wanahisa uliofanyika jijini Dar es Salaam .
Wanahisa wa Benki ya NMB wakiwa katika Mkutano wao Mkuu wa Mwaka ambapo uliofanyika Jijini Dar es Salaam ambapo Benki hiyo imetangaza jumla ya shilingi bilioni 52 kama gawiwo kwa wanahisa wote. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha na Mipango) 

……………………………………………………………………. 

Benki ya NMB imepata faida ya ya shilingi bilioni 153.8 kwa mwaka 2016 hivyo kuiwezesha kutoa gawiwo la shilingi bilioni 16.5 kwa Serikali ambayo inamiliki asilimia 32 ya hisa za Benki hiyo. 

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango (Mb) alikabidhiwa hundi kifani ya gawiwo hilo katika Mkutano Mkuu wa Mwaka wa wanahisa wa Benki hiyo uliofanyika Jijini Dar es Salaam. 

Dkt. Mpango amezipongeza juhudi za watendaji wa Benki hiyo waliofanikisha kupatikana kwa faida iliyowezesha Serikali kupata gawiwo. Aidha, Serikali inajivunia mafanikio makubwa ya kiutendaji ya NMB na uwekezaji wake ambao unatija na unaifanya serikali isijutie uamuzi wake wa kuibinafsisha Benki hiyo. 

Amesema fedha hizo zilizopatikana kutokana na gawiwo zitaelekezwa kwenye maendeleo ili kutatua baadhi ya kero zinazowakabili wananchi. 

Ameahidi kuwa, Serikali kama mwanahisa itaendelea kuitumia Benki hiyo kikamilifu katika huduma za kibenki ili kuiwezesha kuongeza mapato. 

“Shughuli ambazo Serikali itazifanya kupitia NMB Bank Plc ni pamoja na malipo ya mishahara ya wafanyakazi wa Umma na pia kukusanya mapato ya Serikali yanayotokana na kodi na yasiyo ya kodi. 

Waziri Mpango ametumia nafasi hiyo kuagiza kampuni ambazo zenye ubia na Serikali kuiga mfano wa NMB Benki Plc na kupeleka gawiwo katika faida wanayopata. 

“Katika Serikali ya Awamu ya Tano ya Mhe. Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli haiingii akilini kusikia kila mwaka mnapata hasara lakini mpo hamtoki, tumevumilia vya kutosha sasa imetosha, haiwezekani unawekeza miaka 10 lakini watanzania hawapati chochote” alionya Dkt. Mpango. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Ineke Bussemaker amesema jumla la gawiwo lote litakalolipwa kwa wanahisa ni shilingi Bilioni 52 kiwango ambacho kinaendana na sera ya Benki ya kutoa theluthi moja ya asilimia 33.3 ya faida baada ya kodi kwa wanahisa wake. 

Bussemaker alisema kuwa mafanikio ya Benki hiyo katika mwaka ulioishia Disemba 31,2016 ilipata faida ya shilingi bilioni 153.8 licha ya changamoto za kibenki, likiwa ni ongezeko la asilimia 2, ukilinganisha na mwaka 2015 ambapo ilipata faida ya shilingi bilioni 150.3 

Wanahisa wa Benki hiyo wamekubaliana kubadili jina la Benki hiyo kutoka National Microfinance Bank na kuwa NMB Bank Plc. Waziri mpango amesema mapendekezo ya kubadili jina yalifika Serikalini na Serikali imeridhia. 

Hii itakuwa mara ya pili kwa Serikali kupata gawiwo kutoka Benki ya NMB ambapo mwaka uliopita, Benki hiyo ilitoa gawiwo la kiasi kama hicho cha shilingi bilioni 16.5 baada ya kutengeneza faida.

No comments: