Wednesday, May 17, 2017

Watumishi wa umma kuweni karibu na wananchi, Balozi Mwinyi

Taasisi za Serikali zimehimizwa ziwe karibu na wananchi ili ziweze kuwahudumia na kuwaelimisha juu ya huduma inazozitoa. Wananchi wengi wamekuwa wakilalamika mara kwa mara kuhusu watumishi wa umma kutotumia weledi na ubunifu katika kuwahudumia wananchi jambo ambalo likiachwa liendelee, Tanzania itaachwa nyuma ndani ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na ulimwengu mzima kwa ujumla.

Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhan Mwinyi katika semina kuhusu elimu ya mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki na fursa zake inayotolewa na wataalamu wa Wizara yake kisiwani Pemba. Semina hiyo iliyoanza jana inafanyika kwenye uwanja wa Gombani, Pemba na itamalizika tarehe 18 Mei 2017.

"Kuna fursa nyingi za kiuchumi katika Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki lakini kama wananchi wetu hatutawasaidia na kuwaelimisha kuhusu nyaraka na masharti yanayokidhi vigezo wataachwa nyuma na kubaki kuwa watazamaji na walalamikaji" Balozi Mwinyi alisema.

Wajasiriamali walielezea masikitiko yao juu ya ugumu wa kupata hati za kusafiria kutokana na mlolongo wa masharti hususan, inapotokea kuwa safari ni ya ghafla. Aidha, wajasiriamali wamekuwa wakilalamika kuwa wanapata tabu kusajili bidhaa zao katika mamlaka zinazosimamia ubora wa viwango wa bidhaa, chakula na madawa kwa kuelezwa kwamba bidhaa zao ni duni, hivyo wameiomba Serikali iwawezeshe kupata teknolojia ya kisasa ikiwa ni pamoja na vifungashio.

Balozi Mwinyi alisisitiza umuhimu wa taasisi zote bila kukiuka Sheria, kanuni na vigezo vilivyowekwa kurahisisha taratibu zao ili wananchi wapate nyaraka zinazotakiwa kwa urahisi ili iwe wepesi kwao kuchangamkia fursa za kiuchumi na kibiashara katika soko la pamoja la Afrika Mashariki.

Akitoa ufafanuzi kuhusu upatikanaji wa hati za kusafiria, Afisa Uhamiaji, Bw. Haji Kassim Haji alisema kuwa taratibu zilizowekwa hazina lengo la kukwamisha shughuli ya mtu yeyote isipokuwa zimewekwa kwa kuzingatia maslahi mapana ya nchi. Katika ulimwengu wa leo ambao unakabiliwa na changamoto nyingi za kiusalama kama, ugaidi, uharamia, Biashara haramu ya binadamu, uhamiaji haramu, lazima masharti yazingatiwe ili kuepuka uwezekano wa kutokea uovu huo.

Aidha, Balozi Mwinyi alishauri wajasiriamali wajiunge katika vikundi ili masuala yao ikiwa ni pamoja na maombi ya hati za kusafiria yafanywe kwa pamoja wakidhaminiwa na taasisi zinazosimamia shughuli zao.


Imetolewa na:

Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, 
Pemba, 16 Mei, 2017
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Mwinyi akitoa mwongozo kwa wajumbe wa semina ya Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inayoendelea kufanyika kisiwani Pemba. Pamoja na mambo mengine amewahimiza wananchi kuchangamkia fursa zinazopatikana kwenye mtangamano. 
Mbunge wa jimbo la Konga, Mhe. Mbarouk Ali akichangia jambo kwenye semina. 
Sehemu ya wajumbe wakiendelea kusikiliza mada mbalimbali zilizokuwa zikiendelea kutolewa kwenye semina. 
Afisa kutoka Ofisi za Uhamiaji Pemba Bw. Haji Kassim Haji akijibu hoja mbalimbali zilizokuwa zikitolewa na wajumbe kwenye semina juu ya upatikanaji wa Hati ya Kusafiria ya Afrika Mashariki. 
Bw. Amedeusi Mzee akitoa mada kuhusu Soko la Pamoja na faida zinazopatikana kwenye soko hilo. 
Luteni wa JKU naye akitolea ufafanuzi kwenye maswala mbalimbali yenayohusiana na maswala ya magendo. 
Wajumbe wakisikiliza kwa makini mada na majibu ya hoja mbalimbali walizokuwa wakihitaji kufahamu kutoka kwa Bw. Amedeusi (hayupo pichani) na mjumbe kutoka JKU. 

No comments: