Tuesday, May 30, 2017

POLISI TABORA YAKAMATA KIJANA MMOJA KWA KUTUMIA NGUO ZA JWTZ KUTAPELI

Mkulima mmoja Kitangili mkoani Shinyanga Francis Martin Kilalo (31)anashikiliwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora kukutwa na sare na vifaa vingine vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ) ambavyo anatuhumiwa kuvitumia kupateli na kuwadanganya kwa kuchukua fedha kutoka kwa vijana wanaotafuta nafasi ya kujiunga na Jeshi hilo.

Taarifa hiyo imetolewa jana na Kamanda wa Mkoa wa Tabaora Wilbroad Mtafungwa alipokuwa anaongea na waandishi wa habari Ofisi kwake juu ya hatua mbalimbali walizochukua katika kupambana na uhalifu mkoani humo.

Alisema kuwa Polisi walifanikiwa kumukamata mtuhumiwa huyo katika Hoteli ya JM iliyopo Wilayani Igunga akiwa na sare mbalimbali za Jeshi la waananchi Tanzania (JWTZ) zikiwa na cheo cha Koplo ambavyo ni pamoja na kofia tatu, begi, sweta, buti jozi moja, magwanda na mikanda mitatu.

Mali nyingine zilikamatwa kwa mtuhumiwa huyo ni pamoja na fomu za likizo cha likizo , fomu za kujaza vijana wanaotaka kujiunga na Jeshi hilo na Jeshi la Kujenga Taifa(JKT) kwa mujibu wa Sheria na hiari na mihuli zenye nembo inayofanana na Jeshi hilo.

Kamanda Mtafungwa alisema kuwa mtuhumiwa alikuwa akitumia nyaraka na sare za Jeshi hilo kuchukua fedha kwa kuwadanganya na kuwatapeli wananchi mbalimbali kwa kudai atawatafutia ajira katika majeshi ya Kujenga Taifa na la Wananchi.

Kamanda huyo wa Mkoa wa Tabora aliongeza kuwa mtuhimiwa huyo pia alikutwa barua kutoka Serikali za mitaa za Dar es salaam na gari aina ya Toyota Starlet yenye namba za Usajili T633 ARF ambalo wanaendelea kuchunguza uhalali wa umiliki wake na ambalo mtuhumiwa alikuwa akilitumia na kuwafanya baadhi ya wananchi wamuamini kuwa atawasaidia kupata nafasi katika majeshi.

Aliongeza kuwa mtuhimiwa huyo pia alikuwa na barua za maombi ya watu ya kuomba kujiunga na Jeshi, Fomu za Matibabu za Hospitali ya Jeshi ya Lugalo na nakala ya Vyeti vya kumaliza elimu ya Sekondari vya baadhi ya watu.

Kufuatia tukio hilo alitoa wito kwa waananchi waliowahi kutapeli ndani na nje ya Mkoa wa Tabora kujitokeza katika vituo vya Polisi ili waweze kutoa ushahidi utakasaidia kuonyesha ni jinsi gani walivyumizwa na mtuhumiwa huyo .

Kamanda Mtafungwa alisema kuwa Polisi inaendelea kushirikiana na JWTZ ili iweze kubaini sare na vifaa hivyo alivipata wapi , kwa lengo lipi na ni nani aliyompatia ili wahusika wote waweze kufikishwa katika vyombo vya Sheria kwa hatua zaidi.

Aidha , Kamanda huyo aliwaasa wananchi kuwa makini na matapeli wanaowadai fedha na kuwadanganya kuwa watawatafutia kazi katika Majeshi kwani vyombo hivyo vinaotaratibu wake ambao ndio unaotumika kuwapata vijana wanaojiunga kwa mujibu wa sheria na wale wa hiari na sio kwa kuchangishwa fedha.

Wakati huo huo Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora limefanikiwa kukamata watuhimiwa 17 kwa kukutwa na lita 205.25 za gongo wakati wa msako wa kukamata wa watumiaji na wauzaji wa bidhaa hizo haramu.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora Mtafungwa alisema kuwa watuhimiwa watafikishwa Mahakamani kujibu tuhuma zao wakati wowote.
Aidha , alisema kuwa katika zoezi hilo pia Polisi ilifanikiwa kuteketeza ekari tano na nusu za mashamba ya zikiwa na uzito wa kilogramu 220 yalikuwa yamelimwa katika Msitu wa Hifadhi wa Igombe wilayani Uyui.

Alisema kuwa jitihada za kuwasaka watuhumiwa wa mashamba hayo zinaendelea na kuwaomba wananchi wenye taarifa ya walipo wahusika walisaidie Jeshi la Polisi ili wahusika waweze kufikishwa Mahakama kujibu tuhuma zao

No comments: