Friday, April 14, 2017

MKUTANO BAINA YA SERIKALI NA SEKTA BINAFSI UMEKUWA WA MAFANIKIO


Waziri Charles Mwijage akizungumza na wadau wa Sekta Binafsi katika Mkutano maalum kati ya Sekta hiyo na Serikali.Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikutana na wadau wa Sekta Binafsi mapema wiki hii katika mkutano maalum ulioandaliwa na Chemba ya Wafanyabiashara, Viwanda na Kilimo nchini (TCCIA) kwa kushirikiana na Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF).
Kutoka kushoto ni Godfrey Simbeye, Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF, Gotfrid Muganda Mkurugenzi Mtendaji TCCIA, Octavian Mshiu, Makamu wa Rais TCCIA ambao ni waandaaji wa Mkutano huo maalum baina ya Serikali na Sekta Binafsi wakiwa na Hussein Kamote, Mkurugenzi wa Huduma na Uanachama-CTI.Lengo la mkutano huo maalum baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ulikuwa na lengo la kuboresha mazingira ya biashara nchini, kukuza ushirikiano kati ya Serikali na Sekta Binafsi pamoja na kuongeza njia za kukuza uchumi utakaochochea ya azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Tanzania kuwa nchi ya Viwanda.
Mkutano huo uliofanyika mjini Dodoma katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango (Treasury Square) uliongozwa na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji (MB) Mh. Charles Mwijage pamoja na Waziri wa Fedha na Mipango (MB), Mh. Dkt. Philip Mpango na kuhudhuriwa na wabunge, makatibu wakuu na manaibu katibu wakuu, Kamishna wa TRA, Mwenyekiti wa TPSF Makamu wa Rais- viwanda wa TCCIA, Mwenyekiti wa TRADEMARK EAST AFRICA, Wafanyabiashara wa Sekta mbalimbali nchini na wawekezaji, viongozi wa ACT, ATE, MOAT, TASOA pamoja na wajumbe wedau wengine wa biashara.
Makamu wa Rais Sekta ya Viwanda TCCIA Octavian Mshiu akizungumza jambo na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mh. Charles Mwijage (MB) katika Mkutano huo. 
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mh. Charles Mwijage (MB) kushoto, akifurahia jambo na Mwenyekiti wa TPSF Bw. Reginald Mengi kulia, anayeshuhudia ni Waziri wa Fedha na Mipango Mh. Philip Mpango (MB). 
Mkutano huo uliipa Serikali fursa ya kusikiliza changamoto zinazoikabili Sekta Binafsi na kukusanya maoni ya wadau wa sekta hiyo na kuahidi kuzifanyia kazi na kuzitatua ili kuweza kuimarisha mahusiano, umoja, mshikamano, ushiriakiano na uaminifu baina ya sekta hizi muhimu katika uchumi wa taifa la Tanzania.
Akizungumza katika Mkutano huo, Waziri Mwijage aliwashukuru wadau wa Sekta Binafsi kwa kujitokeza kwa wingi ili kuzungumza na Serikali na kuwa njia hii ya kukutana kwa vile imeonekana kuwa njema basi itaendelea kutumika ili kuhakikisha sekta hizi zinakutana mara kwa mara. Waziri aliahidi kushughulikia kero zinazokabili mazingira ya biashara kama kuwepo kwa kodi na kuahidi upunguzwaji wa kodi utitiri ambazo zimekuwa kero kwa wafanyabiashara na pia kuweka mazingira rafiki baina ya Sekta Binafsi na Serikali. 
Kwa upande wake Waziri Mpango alisema, “Tulipofikiria wazo hili hatukutegemea muitikio huu na kwamba ni utaratibu muafaka na napendekeza kwa kuanzia tuendeleze huu utaratibu na tukutane angalau mara moja katika kila robo ya mwaka, asanteni sana. Mmeipongeza serikali na hata mmetuelezea changamoto ambazo ni za msingi sana, mmeifanya siku hii kuwa na thamani kubwa katika kujenga Tanzania mpya”. 
Waziri Philip Mpango akizungumza na wadau wa Sekta Binafsi katika Mkutano maalum kati ya Sekta hiyo na Serikali.
Maofisa waandamizi wa Serikali na wadau wa Sekta Binafsi wakifatilia mazungumzo katika Mkutano maalum baina ya Serikali na Sekta Binafsi uliofanyika mjini Dodoma wiki hii.

No comments: