Tuesday, April 4, 2017

KAIMU MKURUGENZI MKUU NIDA AFANYA ZIARA KUKAGUA SHUGHULI ZA USAJILI VITAMBULISHO VYA TAIFA MKOANI IRINGA

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), Ndugu Andrew W. Massawe yuko mkoani Iringa kukagua maendeleo ya zoezi la Usajili na Utambuzi wa watu; ambapo pamoja na mambo mengine anatazamiwa kushuhudia sherehe za uzinduzi wa utoaji Vitambulisho vya Taifa kwa wananchi wa Wilaya ya Mufindi na kuzinduliwa kwa kampeni ya Usajili wa wananchi na wageni wenye umri wa miaka 18 na kuendelea wanaoishi mkoani humo.
Katika ziara yake; leo amekutana na Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mhe. Jamhuri William, ambaye amemweleza Mkurugenzi huyo hatua kubwa ambayo Wilaya yake imefikia mpaka sasa katika kuwasajili wananchi, ambapo takribani asilimia 60 ya wananchi wameshasajiliwa, kuchukuliwa alama za vidole na baadhi Vitambulisho vyao kuzalishwa, mbali na kukamilika kwa zoezi la kuwasajiliwa Watumishi wa Umma.
Akiwa Wilayani Mufindi Mkurugenzi huyo ametembelea na kukagua shughuli katika ofisi ya Usajili na kukagua vifaa vinavyotumika katika Usajili. Aidha; amefanya mazungumzo na wadau wakubwa wa NIDA likiwemo Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kikosi cha Mafinga namba 841, kinachoongozwa na Kanali Hamisi Maiga; ambaye amehakikishia NIDA ushirikiano zaidi katika kufanikisha zoezi la kuwasajiliwa wananchi.
Mkurugenzi huyo pia alitembelea Kata za Boma na Upendo na kukutana na watendaji wa Kata hizo pamoja na kufanya mazungumzo na Diwani wa Kata ya Boma Mhe. Julist Kisoma (Chadema) ambaye ameishukuru NIDA kwa kufanikisha zoezi la kuwasajili wa wananchi.
Mbali na kukagua shughuli za Usajili Wilaya ya Mufindi; pia amekutana na Katibu Tawala wa Wilaya ya Iringa bwana Joseph Meshacky Chitnka ambaye alieleza mikakati ya Wilaya yake katika kuhakikisha watu wote wanafikiwa kwa wakati kusajiliwa na kupata Vitambulisho vya Taifa.
Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa ilianza utekelezaji wa zoezi la Usajili na Utambuzi wa Watu kwa mara ya kwanza mkoa wa Iringa mwezi Septemba, 2016 kwa kuanza na kuwasajili Watumishi wa Umma zoezi lililomalizika hivi karibuni na kuanza mikakati ya kuwasajili wananchi na Wageni. 
 Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mhe. Jamhuri William akizungumza jambo na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Nida Ndugu Andrew W. Massawe wakati alipofanya ziara Wilaya ya Mufindi 
 Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Mhe. Jamhuri William (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA Ndugu Andrew W. Massawe (katikati kulia), wengine wa kwanza kushoto ni ndugu Alphonce Malibiche Kaimu Mkurugenzi Uzalishaji Vitambulisho vya Taifa (NIDA) na wa kwanza  kulia ni Katibu Tawala Wilaya ya Mufindi Ndugu Bernard.
 Wafanyakazi wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa Wilaya ya Mufindi wakiwa kwenye picha ya pamoja na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA; Ndugu Andrew W. Massawe
 Ndugu George Mushi Afisa Usajili Mkoa wa Iringa (RRO), akitoa maelezo kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, kuhusu vifaa vinavyotumika kwenye usajili wa wananchi alipotembelea ghala la kuhifadhi vifaa wilayani Mufindi
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA akiwa na Kanali Hamisi Maiga Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kikosi cha Mafinga namba 841, wakati alipotembelea kambi hiyo.
 Mtendaji wa Kata ya Boma; Joseph Kiwele akitoa taarifa ya utekelezaji wa zoezi la usajili wananchi kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA Ndugu Andrew W. Massawe akisalimiana na Diwani wa Kata ya Boma Mhe. Julist Kisoma (Chadema).
 Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa NIDA ndugu Andrew W. Massawe akiweka saini kwenye ofisi ya Katibu Tawala wa Wilaya ya Iringa bwana Joseph Meshacky Chitinka wakati alipofanya ziara.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu NIDA (Katikati) akiwa na Katibu Tawala wa Wilaya ya Iringa bwana Joseph Meshacky Chitinka (katikati kulia). Wengine ni Ndugu Alphonce Malibiche Kaimu Mkurugenzi Uzalishaji Vitambulisho (wa kwanza kushoto) na  wa kwanza kulia ni ndugu George Mushi, Afisa Usajili Mkoa wa Iringa.

No comments: