Thursday, March 23, 2017

VIJANA WA SERENGETI BOYS WAKABIDHIWA KADI ZA BIMA YA AFYA NA NHIF


Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii.


MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umetoa kadi za bima kwa wachezaji wote 23 wa timu ya Taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 17 'Serengeti boys' kwa ajili ya masuala ya matibabu.

Kaimu Mkurugenzi na Masoko Mfuko huo Angela Mziray alisema wamekuwa washirikiana na Shirikisho la mpira wa miguu Tanzania (TFF) katika shughuli mbalimbali ikiwemo kuwa sehemu ya udhamini wa ligi kuu ya Vodacom Tanzania bara.

Angela alisema kwa sababu ugonjwa unakuja bila taarifa na wachezaji wapo kwenye hatari ya kuumia na kuugua pia kwahiyo imekuwa vizuri kwa TFF kuliona hilo nakuwapatia kadi za bima ya afya.

"Namshukuru Rais Jamal Malinzi kwa kusimamia suala hili mpaka leo tumefikia hatua hii na ninaahidi kwa niada ya NHIF tutaendelea kushirikiana na TFF katika masuala mbalimbali," alisema Mziray.

Kwa upande wake Katibu mkuu wa TFF Selestine Mwesigwa alisema bima hizo zitakuwa msaada mkubwa kwa wachezaji hao kwakua wataweza kutibiwa mahali popote nchini hata wasipokuwa kambini.

NHIF imefika asilimia 90 nchi nzima wakiwa na zaidi ya vituo 6000 kwa ajili ya kutoa huduma ya afya.

Serengeti ambayo inaendelea na kambi jijini Dar es Salaam inataondoka wiki ijayo kuelekea mkoani Kagera kwa kambi ya wiki moja kabla ya kuelekea nchini Morocco kwa kambi ya mwezi mzima.
Kaimu Mkurugenzi na Masoko Mfuko wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Angela Mziray akizungumza na vijana wa Serengeti Boys pamoja na waandishi wakati wa makabidhiano ya kadi za Afya za Bima kwa ajili ya matibabu leo Jijini Dar es salaam. Kushoto ni Mwenyekiti wa kamati ya soka la Vijana Ayubu Nyenzi na Meneja wa Uanachama wa NHIF Eletruda Mbogoro.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) Selestine Mwesigwa akizungumza na vijana wa Serengeti Boys pamoja na waandishi wakati wa makabidhiano ya kadi za Afya za Bima kwa ajili ya matibabu leo Jijini Dar es salaam. 

Kaimu Mkurugenzi na Masoko Mfuko wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Angela Mziray akikabidhi kadi za Bima kwa ajili ya matibabu kwa vijna wa Serengeti Boys leo Jijini Dar es salaam.
Vijana wa Serengeti Boys wakiwa katika chumba cha Mazoezi (Gym) ambapo Mwenyekiti wa Michezo wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Msifu Chenjela kuwa wana ruksa ya kuutumia pale watakapohitaji .

Viongozi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wakiwa pamoja na viongozi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Nchini (TFF) na vijana wa Serengeti Boys mara baada ya kukabidhiwa kadi za Bima ya Afya leo Jijini Dar es salaam.

No comments: