Thursday, March 30, 2017

SERENGETI BOYS WAJIFUA TAYARI KUWAVAA BURUNDI LEO UWANJA WA KAITABA, BUKOBA


Timu ya Taifa ya mpira wa miguu ya vijana wenye umri wa miaka 17 maarufu kwa jina la Serengeti Boys jana Jamatano wamefanya mazoezi kujiweka tayari na mchezo wao wa kesho na Timu ya U17 ya Burundi.
Serengeti Boys itakuwa kambini Bukoba hadi Aprili 2, mwaka huu ambako inatarajiwa kucheza michezo miwili ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya timu vijana ya Burundi kwenye Uwanja wa Kaitaba, mjini Bukoba mkoani hapa Kagera. Michezo hiyo itaanza kuchezwa Machi 30, 2017 na kurudiana Aprili mosi, mwaka huu. 

Serengeti Boys ambayo inajiandaa na michuano Afrika huko Gabon itarejea Dar es Salaam Aprili 2, mwaka huu ambako imepangwa kucheza na Ghana Aprili 3, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Mchezo huo utatanguliwa na hafla ya kuagwa kwa kukabidhiwa bendera. 

Timu itaelekea Morocco Mei 5, mwaka huu baadaye itapita Cameroon kwenye kambi ya zaidi ya mwezi mmoja baadaye itakwenda Gabon katika michuano itakayoanza Mei 14, 2017. Ikiwa Cameroon itacheza mechi mbili za kimataifa dhidi ya wenyeji kabla ya kwenda kwenye fainali. 

Serengeti Boys ni timu ya vijana ambayo imefuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika Gabon kuanzia Mei 14, mwaka huu. Timu hiyo imepangwa Kundi ‘B’ pamoja na mabingwa watetezi Mali, Niger na Angola. Ina lengo la kurejea na Kombe la Afrika kwa vijana. 
Na ikitokea imekosa nafasi hiyo angalau ikafika nusu fainali ambako kwa mafanikio hayo itakuwa tayari ina tiketi mkononi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia huko India, Novemba, mwaka huu. 
Kikosi cha Serengeti Boys kinaundwa na Makipa: Ramadhan Kabwili, Samwel Edward na Kelvin Kayego. 
Walinzi: Kibwana Ally Shomari, Nickson Kibabage, Israel Mwenda, Dickson Job, Ally Msengi, Issa Makamba na Enrick Vitalis Nkosi. 
Viungo: Kelvin Nashon Naftali, Ally Ng’anzi, Mohamed Rashid, Shaaban Ada, Mathias Juan, Marco Gerald, Abdulhamis Suleiman, Saidi Mussa na Cyprian Benedictor Mtesigwa. 

Washambuliaji: Muhsin Malima Makame, Yohana Mkomola, Ibrahim Abdallah, Assad Juma na Abdul Suleiman. 
Benchi la Ufundi: 
Bakari Shime (Kocha Mkuu) 
Oscar Mirambo (Kocha Msaidizi) 
Muharami Mohamed (Kocha wa makipa) 
Kim Poulsen (Mshauri wa Ufundi) 
Edward Evans (Mtunza Vifaa) 
Shecky Mngazija (Daktari wa timu)

Serengeti Boys watacheza mchezo wao wa kwanza kesho jioni na Timu ya U17 ya Burundi ambayo imeingia Bukoba hii leo jioni kwenye muda wa saa 11 na hatimaye hawakuweza kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Kaitaba kutokana na uchovu wa safari yao na hivyo kutoa taarifa kuwa watafanya asubuhi saa moja.

No comments: