Tuesday, February 28, 2017

MWAKIFAMBA AKANUSHA UJUMBE ULIONEZWA MITANDAONI

Na Jacquiline Mrisho – MAELEZO.

Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania, Simon Mwakifamba amekana kuhusika na utumaji wa ujumbe katika mitandao ya kijamii juu ya kuitisha mkutano na waandishi wa habari. 

Kauli hiyo imetolewa leo Jijini Dar es Salaam na Rais wa Shirikisho hilo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya ujumbe huo uliokuwa ukisambazwa katika mitandao mbalimbali ya kijamii na kumuhusisha Rais wa Shirikisho hilo. 

Mwakifamba amesema kuwa ujumbe huo umeeleza kuwa Rais wa shirikisho hilo atakuwa na mkutano na waandishi wa habari utakaohusu wasanii waliokipigia kampeni Chama cha Mapinduzi (CCM) na kutolipwa fedha zao pamoja na kuunga mkono jitihada za msanii Wema Sepetu kujiunga na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

“Kiukweli sikushiriki kwa namna yoyote katika kuuandika ujumbe huo na nimesikitishwa kuona kwamba huo ujumbe unasambazwa ukiwa na jina langu hivyo umeniletea picha mbaya kwani ni kinyume na taratibu na sheria za Shirikisho,”alisema Mwakifamba.

Amefafanua kuwa Shirikisho hilo sio chama cha siasa na hawajasajiliwa na msajili wa vyama vya siasa bali wamejisajiliwa na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) na kazi zote zinafanyika kwa Sheria Na. 4 ya mwaka 1976 ambayo iko chini ya Bodi ya Filamu Tanzania.

Ameongeza kuwa mwanachama wa shirikisho hilo hafungwi kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa lakini kwa mujibu wa katiba ya vyama na shirikisho ni marufuku siasa kuletwa katika shirikisho au vyama vyake.

Kwa upande wake Afisa Mipango wa Chama cha Waigizaji, Saimon Mwapagaja ametoa rai kwa wananchi wanaotumia vibaya mitandao ya kijamii kwa lengo la kuchafua majina ya watu kuacha tabia hiyo kwani inashusha hadhi ya mtu husika na sio utaratibu mzuri.

“Changamoto tulizonazo katika tasnia ya filamu ni nyingi sana hivyo ifike wakati wasanii tuanze kuangalia vitu vya msingi na vyenye tija vitakavyomaliza changamoto hizo, pia wananchi wapunguze kujiamulia kufanya mambo ambayo baadae yanaweza kumsababishia muhusika matatizo mabukwa,” alisema Mwapagaja.

No comments: