Friday, February 24, 2017

DC MTATURU AITUMIA SIKU YA ALHAMISI KUSHUKA KWENYE TARAFA KUSIKILIZA KERO ZA WANANCHI NA KUZITATUA

Mkuu wa wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu akimkabidhi mashuka Dk. Frank kwa ajili ya kituo cha afya cha Ihanja wakati akiwa katika ziara ya kukagua huduma zinazotolewa kituoni humo na kusikiliza kero za wananchi.
Dk. Frank wa kituo cha afya cha Ihanja akitoa maelezo mbele ya mkuu wa wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu na diwani wa kata ya Kituntu Said Tumbwi wakati walipofika kituoni hapo.
Mkuu wa wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu akikagua shamba la mtama la mwananchi wa kijiji cha Puma ikiwa ni muendelezo wa ziara yake aliyoifanya katika tarafa ya Ihanja.
Miraji Mtaturu mkuu wa wilaya ya Ikungi akiwa na afisa kilimo wa tarafa ya Ihanja Azizi Mwamakula wakikagua shamba la viazi la hekari mbili linalomilikiwa na vijana wa tarafa hiyo.
Baadhi ya wakazi wa tarafa ya Ihanja wakimsikiliza mkuu wa wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu hayupo pichani alipokuwa anasikiliza kero zao na kuzijibu katika ukumbi wa kanisa lililopo makao makuu ya tarafa ya ihanja.

……………………………………..

KATIKA moja ya mambo ambayo serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa rais dokta John Magufuli inasisitiza kuyafanya ni kwa viongozi kushuka kwa wananchi kwa kuwatembelea ,kusikiliza kero zao na kuzitatua.

Ili kulitekeleza hilo mkuu wa wilaya ya Ikungi Miraji Mtaturu ameitenga siku ya alhamisi ya kila wiki kuhamishia ofisi yake kwenye tarafa maalum kwa ajili ya kusikiliza kero za wananchi na kuzipatia ufumbuzi kutoka kwa wahusika.

Alhamisi hii akiwa ameweka kambi tarafa ya Ihanja wilayani humo Mtaturu amemuagiza kaimu mkurugenzi wa wilaya hiyo Haika Massawe kumuelekeza mwanasheria wa halmashauri kutoa msaada wa kisheria kwa Fatma Mohammed ambaye anasumbuliwa kupata haki yake ya ardhi.

Mama huyo anafuatilia shamba la baba yake mzazi ambaye ni mzee na anaumwa lililovamiwa na mtu bila ya mafanikio pamoja na kwamba alishinda kesi katika baraza la kata na wilaya lakini alikatiwa rufaa mahakama ya rufaa ya Dodoma.

“Mkurugenzi fuatilia kwa mwanasheria ilia toe msaada wa kisheria,kesi hii imeelekezwa na jaji wa mahakama ya rufaa ya Dodoma kuwa kuna makosa yamefanyika kwenye baraza la kata huku,”alisema Mtaturu.

Katika ziara hiyo alitembelea kituo cha afya cha Ihanja na kutoa agizo kwa kaimu mkurugenzi Massawe kuhakikisha anamsimamia mhandisi wa maji wa halmashauri hiyo afanye tathimini ya kuchimba kisima kirefu cha maji ili kumaliza tatizo la maji kituoni hapo.

“Serikali ipo kwa ajili ya kuwahudumia wananchi hivyo nawaelekeza viongozi wote wa vijiji,kata na tarafa kujenga utaratibu wa kusikiliza kero za wananchi hawa na zilizo ndani ya uwezo wenu mzitatue ili kutimiza zana ya utawala bora,”alisema Mtaturu.

Kwa upande wake afisa tarafa Modesta Manyungu akisoma taarifa alisema wananchi wa tarafa hiyo wanaendelea kufanya kazi ya kujiletea maendeleo pamoja na changamoto mbalimbali zilizopo ikiwemo upungufu wa walimu,watumishi wa idara ya afya,polisi na afisa ugani,upungufu wa visima vya maji na wanasiasa wenye nia ovu kurudisha kukwamisha juhudi za kuwaletea maendeleo wananchi.

“Pamoja na changamoto hizo yapo mafanikio ikiwemo uandikishaji wa asilimia mia moja kwa wanafunzi katika elimu ya msingi,kuongezeka kwa mwamko kutokana na serikali kutekeleza ahadi ya elimu bila ya malipo,”alisema Manyungu.

Mbali na kutembelea kituo cha afya cha Ihanja Mtaturu alitembelea pia mashamba ya mtama,viazi na wafugaji wa kuku,alikagua ujenzi wa maabara na madarasa mawili yaliyopo katika shule ya sekondari ya Masinda ambapo katika kuunga mkono ujenzi huo mbunge wa Singida Magharibi Elibariki Kingu alichangia mabati 106 na Mtaturu alikabidhi mashuka 20 kwa ajili ya kituo hicho cha afya.

No comments: