Tuesday, January 17, 2017

WAZIRI MWIJAGE AZINDUA BODI YA MAMLAKA YA MAENDELEO YA BIASHARA TANZANIA


Mhe Charles Mwijage akimkabidhi vitendea kazi Mhandisi Christopher Chiza Mwenyekiti mpya wa bodi ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara ya Tanzania baada ya uzinduzi wa bodi hiyo


Mhe Charles Mwijage, Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji asisitiza mageuzi ya kiuchumi kwa maendeleo ya watu yanayolenga katika kujenga viwanda na kupunguza biashara ya kuuza malighafi na ilenge kwenye kuhamasisha biashara za kuuza bidhaa zilizoongezwa thamani. 

Hayo aliyasema kwenye uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maendelo ya Biashara Tanzania (TanTrade) uliofanyika tarehe 16 Januari, 2017 katika ofisi za TanTrade zilizopo kwenye kiwanja cha Mwl J.K Nyerere barabara ya Kilwa. 

Mhe Mwijage amesema kuwa kazi kubwa ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) ni kuhamasisha shughuli za biashara Tanzania na wizara ya Viwanda,Biashara na Uwekezaji ni wizara ambayo matumaini mengi ya watanzania yameangalia huko hivyo watu wanategemea matumaini makubwa sana. 

Akaendelea kwa kusema kuwa kwa mwaka 2017 kwenye maonesho ya 41 ya kimataifa ya biashara ya Dar es Salaam (DITF) yawe ya tofauti kwa watakaokuja kuonyesha bidhaa zao kutoka nchi za nje, waoneshaji hao waje na mashine za viwanda vidogo ili watanzania watakaokuja kuona na kununua mashine hizo ziweze kusaidia kuongeza thamani za bidhaa zao ili kasi ya kuuza malighafi nje ya nchi ipungue bali bidhaa za viwandani ziweze kuongezewa thamani ili kuweza kuuza nje ya nchi. 

Mhe Mwijage aliendelea kuiambia Bodi ya Wakurugenzi iliyoteuliwa kuwa kazi zote ambazo zilisimama zifanyiwe kazi mapema ili kueza kukamilisha maamuzi yote usiku na mchana akaongeza kwa kusema kuwa maamuzi ambayo hayakufanyika ni mabaya mno na gharama zake ni kubwa afadhali maamuzi ambayo yamefanyika ila mabaya hivyo asingependa kufanya maamuzi ya bodi bila bodi kumshauri ili aweze kufanya kazi yake kwa ufanisi. 

Akaongeza kwa kusema kuwa tunapoelekea kwenye uchumi wa viwanda Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) yapaswa kwenda kuwafundisha watanzania ili waelewe kile wanachopaswa kwenda kukiuza nchi za nje na kuwashawishi wale wanaokuja kuonesha bidhaa zao nchini waje kuonesha vitu gani kwetu vyenye tija. Natamani maonesho ya kimataifa ya biashara Dar es salaam (DITF) kuwe na viwanda vidogovidogo vingi, tuwashawishi wanaokuja kuonesha kwa kutumia teknolojia zao ila yatupasa kufanyaTantrade kutumia mwenyekiti wao wafanye survey kwa kuhusisha wataalam kama teknolojia zao zinakidhi haja ya mazingira ya nchi yetu na matakwa ya wananchi.

Mhe Mwijahe akatoa maagizo kwa Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) kuulizia ofisi zote za serikali na za watu binafsi ni maonesho gani yaliyopo mwaka 2017 sababu kisheria maonesho yote Tanzania yanasimamiwa na tantrade hata wanaokwenda nje ya nchi kwenye maonesho mbalimbali wapate Baraka za TanTrade kwa kutambulika hivyo asionekane asionekane mtu anaenda bila kupata kibali kupitia TanTrade na pia kuhakikisha taasisi hiyo haitawanyi rasilimali zilizopo bali ikazane kuongeza trade volume za bidhaa za viwanda ziende kwa wingi nje ya nchi. 

Nae mhe Mhandisi Christopher Chiza Mwenyekiti wa bodi mpya ya wakurugenzi kutoka Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) alisema kuwa nguzo kubwa atakayotumia katika kutekeleza majukumu ni sheria iliyoanzisha mamlaka ya kuendeleza Biashara Tanzania ya mwaka 2009 na sheria zingine za nchi. 

Akaendelea kusema kuwa kwa uchache majukumu ambayo atakayosimamia ni pamoja na kusimamia na kujiridhisha kwamba mali za mamlaka zinazohamishika na zisizohamishika zinatunzwa na zinatumika vzuri kwa manufaa ya Umma, Kuelekeza mamlaka kubuni na kutafuta vyanzo mbalimbali vya fedha na kwa fedha zote zitatumika kwa manufaa ya umma, kusaidia mamlaka kubuni na kubaini fursa za biashara na kuziunganisha fursa hizo na wadau mbalimbali ili zijulikane ndani na nje ya nchi kuwawezesha wadau wengine wazichangamkie. Hivyo kama taasisi ya muungano ambayo sehemu kubwa inawagusa makundi mbalimbali ya wazalishaji hawana budi kupanua wigo wa huduma hizo ilikuwafikia kwa ukaribu. 


Mnamo Desemba 17, 2016 Mhe Dkt John Magufuli Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alifanya uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania na kumteua Mhandisi Christopher Kajolo Chiza kuwa mwenyekiti wa Bodi hiyo na kufuatiwa uteuzi wa wajumbe wa bodi hiyo uliofanywa na Mhe Charles Mwijage Waziri wa Viwanda Biashara na Uwekezaji.

No comments: