Wednesday, January 18, 2017

WAZIRI MKUU AMALIZA MGOGORO WA MPAKA KILINDI NA KITETO

*Awaonya viongozi wa siasa wasiwavuruge wananchi

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ameumaliza mgogoro wa mpaka wa ardhi baina ya vijiji vya wilaya za Kiteto na Kilindi uliodumu kwa muda mrefu.

Mgogoro huo ambao ulianza kusuluhishwa tangu mwaka 1997, umepata suluhu kwenye mkutano wa hadhara uliohutubiwa na Waziri Mkuu na kuwajumuisha Wakuu wa Mikoa hiyo miwili, Wabunge wa Kiteto na Kilindi, wenyeviti wa Halmashauri na madiwani wa kata mbili za mpakani pamoja na wananchi wa kata hizo.

Waziri Mkuu pia amewataka wanasiasa na viongozi wengine kutowavuruga wananchi na badala yake wawaongoze vizuri na kutoa maelekezo kwa mujibu wa sheria za nchi.Ametoa agizo hilo leo (Jumatano, Januari 18, 2017)  wakati akizungumza na wananchi wa wilaya za Kiteto na Kilindi katika kijiji cha Lembapili wilayani Kiteto, mkoani Manyara ambako ni kuna mpaka wa  wilaya hizo mbili alipokwenda kutatua mgogoro huo.

Amesema viongozi wa wilaya hizo lazima wafuate sheria na wawaelekeze wananchi umuhimu wa kuzingatia sheria za nchi ikiwa ni pamoja na kuheshimu mipaka iliyowekwa kwa mujibu wa sheria ili kuepusha migogoro.

Akizungumzia kuhusu mgogoro huo wa mpaka, Waziri Mkuu amesema nchi ilishaweka mipaka ya mikoa na wilaya zake yote tangu zamani na kumbukumbu zipo zikiwemo za mpaka wa  wilaya hizo tangu mwaka 1961 kwa  tangazo la Serikali namba 65 na hakuna mabadiliko. Hivyo, aliwasisitiza wauheshimu na kuufuata.

Amesema Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi itakwenda kuweka alama vizuri na viongozi wa wilaya hizo watashirikishwa. Alama hizo zitawekwa na kifaa maalumu, hivyo amewataka wahusika watoe ushirikiano.

Waziri Mkuu amesema katika kipindi ambacho Serikali itakuwa ikiweka alama hizo, wananchi waendelee na shughuli zao hadi hapo zoezi litakapokamilika na wala wasibughudhiwe.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu ametoa siku nane kwa watu wote wanaomiliki silaha katika wilaya za Kilindi na Kiteto wazipeleke kwenye vituo vya Polisi ili zisajiliwe upya na kisha Wakuu wa Mikoa wafanye operesheni maalum na atakayekutwa anamiliki silaha kinyume cha sheria achukuliwe hatua.

“Wakuu wa Mikoa fanyeni ukaguzi maalum na atakayekutwa anamiliki silaha kinyume na utaratibu achukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria. Pia kuna watu wana mitambo ya kutengenezea bunduki hapa, nao pia waisalimishe haraka,” amesisitiza. 

Kwa upande wake, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. William Lukuvi amesema mwanzoni mwa Februari wataalamu wake watakwenda katika mpaka huo ili kuanza kuweka alama vizuri.

Amesema baadhi ya viongozi huwa wana tabia ya kuzuia watendaji kutekeleza majukumu yao, hivyo ametumia gursa hiyo kuwaomba viongozi wa wilaya hizo watoe ushirikiano.

Amesema moja ya majukumu aliyopewa na Mheshimiwa Rais, Dk. John Pombe Magufuli ni kuhakikisha ndani ya miaka hii mitano anamaliza migogoro ya ardhi nchini ukiwemo huo wa Kilindi na Kiteto.

IMETOLEWA NA
OFISI YA WAZIRI MKUU

JUMATANO, JANUARI 18, 2017.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizugumza na  Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi   (kushoto),  Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Joel Bendera wakiwa katika kijiji cha Lembapuli kilichopo kwenye mpaka  wa wilaya ya Kiteto na Kilindi  Januari 18, 2017.  Mheshimiwa Majaliwa alikwenda Kiteto na Kilindi kutatua mgogoro wa mpaka unaovikabili vijiji vya  Mafisa na Kijungu. Wapili kushoto ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga na Muu wa Wilaya ya Tanga mjini , Thobias Mwilapwa. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
 Waziri   Mkuu, Kassim Majaliwa  akielekea kwenye moja ya  jiwe la mpaka wa  wilaya ya Kilindi na Kiteto wakati alipokwenda  kwenye kijiji cha Lembapuli kilichopo kwenye mpaka wa Kiteto na Kilindi kutatua  mgogoro wa mpaka Januari 18, 2017. Kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Joel Bendera na kulia kwake ni  Mkuu wa wilaya na Tanga na Kaimu  Mkuu wa Mkoa wa Tanga Thobias Mwilapwa. 
 Waziri Mkuu, Kassim  Majaliwa akipata maelezo  kutoka kwa watalaam wa upimaji ardhi kuhusu jiwe la alama ya mpaka wa wilaya ya Kilindi na Kiteto katika kijiji cha  mpakani cha Lembapuli  Januari 18, 2017. . Kushoto kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Dkt. Joel Bendera na kulia kwake ni  Mkuu wa wilaya na Tanga na Kaimu  Mkuu wa Mkoa wa Tanga Thobias Mwilapwa. 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akipata  maelezo kuhusu ramani inayoonyesha mpaka  wa wilaya  ya Kilindi na Kiteto katika kijiji cha mpakani cha Lembapuli wakati alipokwenda kutatua mgogoro wa mpaka kati ya wialya hizo Januari 18, 2017.  Mheshimiwa  Majaliwa apia alifuatana na Mawaziri , William Lukuvi wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya makazi na George Simbachawene  wa Ofisi ya Rais- TAMISEMI.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiwapungia wananchi wa Kiteto na Kilindi  wakati  alipokwenda kwenye kijiji  cha Lembapuli  kilichopo kwenye mpaka wa wilaya hizo  kutatua mgogoro wa mpaka Januari  18, 2017.  Wapili kushoto ni Mkuu wa mkoa wa Manyara, Dkt. Joel Bendera na wapili kulia ni Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tanga na Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Thobias Mwilapwa. 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akihutubia  mkutanao wa hadhaa katika kijiji cha  Lembapuli kilichopo mpakani mwa wilaya za Kilindi na Kiteto alikokwenda kutatua mgogoro wa  mpaka  Januari 18, 2017. 
  Baadhi ya wananchi wa  wilaya za Kilindi na Kiteto wakimshangilia  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati alipohutubia mkutano wa hadhara katika kijiji  cha  Lembapuli kilichopo  mpakani mwa wilaya za Kiteto na Kilindi alikokwenda kutatua mgogoro wa mpaka Januari 18, 2017. (Picha na Ofisi ya  Waziri Mkuu)

No comments: