Thursday, December 29, 2016

Tume ya Mipango yatembelea ujenzi wa kituo cha kuzalisha Umeme Kinyerezi II

Msimamizi wa Mradi wa Ujenzi wa Kituo cha kuzalisha Umeme cha Kinyerezi II, Mhandisi Bernd Siegemund akiweka bayana mipango na mikakati ya kumalizika kwa ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi II katika muda uliopangwa. Wengine ni wataalam kutoka Tume ya Mipango, wataalam kutoka TANESCO pamoja na wahandisi wanaotekeleza mradi huo.

Na Adili Mhina, Dar
Timu ya Ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Tume ya Mipango imetembelea mradi wa ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha Kinyerezi II kwa lengo la kuangalia maendeleo ya kituo hicho ambacho kinatarajiwa kuzalisha kiasi cha megawati 240 pale kitakapokamilika.

Akizungumzia juu ya maendeleo ya mradi huo, msimamizi wa shughuli za ujenzi katika kituo hicho, Mhandisi Bernd Siegemund kutoka Ujermani alieleza kuwa ujenzi wa kinyerezi II unaendelea vizuri na unatarajia kukamilika kwa muda uliopangwa.

Ujenzi huo ulianza tarehe 13 Machi, 2015 na kutokana na kasi yake, Mhandisi Siegemund alieleza kuwa matarajio ni kwamba hadi kufikia mwezi Novemba mwaka 2017 mtambo wa kwanza utaanza kuzalisha umeme huku mitambo mingine ikiendelea kuwashwa kadiri itakavyokuwa inakamilika.

Kuhusu vifaa vya ujenzi vinavyohitajika, Mhandisi Siegemund alisema kuwa wanajitahidi kununulia ndani ya nchi vifaa vyote vinavyopatikana na vinavyokidhi mahitaji katika mradi huo na pale inapobidi hulazimika kuagiza kutoka nje. 

Aliongeza kuwa pamoja na nondo kuzalishwa ndani ya nchi wamelazimika kuagiza kutoka nje kwa kuwa viwanda vya ndani bado havijazalisha aina ya nondo wanayohitaji katika ujenzi wa kituo hicho.  

“Vifaa kama saruji na vingine tunaagiza kutoka kwa wazalishaji wa ndani ili kusaidia kukua kwa uchumi wa nchi. Tulitaka kuagiza nondo hapa nchini lakini hatukupata kiwango tunachohitaji kwa kuwa ujenzi huu hautumii nondo tulizozizoea katika ujenzi wa kawaida,”alieleza Siegemund.

Aliongeza kuwa mradi  huo utakapokamilika utakabidhiwa na kuendeshwa na Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ambapo wataalam wa shirika hilo wanaendelea kupata elimu na uzoefu katika kutumia mitambo ya kisasa zaidi na wanashirikishwa katika kila hatua ya ujenzi wa kituo hicho. 

Wataalam kutoka Tume ya Mipango walipata fursa ya kukagua maeneo mbalimbali ya mradi huo ambao umesaidia kupatikana kwa ajira takriban 400 katika ngazi mbalimbali na kumshauri mkandarasi huyo kuendelea na kasi hiyo ili malengo ya Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/17-2020/21) pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 yafikiwe kwa haraka.

Msimamizi wa Mradi wa ujenzi wa Kituo cha kuzalisha Umeme cha Kinyerezi II, Mhandisi Bernd Siegemund akitoa maelezo ya historia ya mradi huo kwa maofisa wa ukaguzi wa Miradi ya Maendeleo kutoka Tume ya Mipango wakati wataalam hao walipofanya ziara kukagua maendeleo ya ujezi wa kituo hicho.

Mhandisi Omari Athuman (aliyeshika notebook) kutoka Tume ya Mipango akitoa ushauri kwa mkandarasi wa mradi wa ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha kinyerezi II.

Picha ya pamoja kati ya wataalamu kutoka Tume ya Mipango, wataalam kutoka TANESCO pamoja na wahandisi wanaotekeleza mradi wa ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha kinyerezi II.



Shughuli za ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha kinyerezi II zikiendelea.

Moja ya sehemu ziliyojengwa kwa ajili ya kusimika mitambo ya kuzalisha umeme.

No comments: