Monday, November 7, 2016

TYPF yatoa huduma ya upimaji afya kwa akina mama

Taasisi ya Tanzania Yemeni Professional Foundation (TYPF), Jumamosi ya Novemba 5 mwaka huu iliendesha huduma ya upimaji wa afya kwa akina mama wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa udhamini wa Ofisi ya Ubalozi wa Kuwait nchini Tanzania.
Shughuli iliyopewa jina la Women’s Health Day, ilikuwa na lengo la taasisi hiyo kutoa huduma bora kwa akina mama kama sehemu ya kuangalia namna ya kusogeza huduma karibu na wananchi sambamba na kuhamasisha suala zima la upimaji wa afya ya akina mama.
Akizungumza katika shughuli hiyo ya upimaji afya kwa wanawake, Mwenyekiti wa Tanzania Yemen Professional Foundation (TYPF), Dr Ameir Binzoo, alisema huduma hiyo ya upimaji afya ilikuwa na dhamira ya kuwasaidia akina mama kufahamu afya zao.
Alisema Siku hiyo ya afya ya wanawake ilidhaminiwa na Ubalozi wa Kuwait, ikiwa ni hatua bora ya kushirikiana na wadau wa afya kuwasaidia wanawake wote wa jijini Dar es Salaam, wakiwamo wale waliohudhuria katika upimaji huo.
“Tunashukuru kwa kufanikiwa kumaliza salama tukio letu kwa sababu limefanyika vizuri na kusudio letu tulilotaka limefika kwa wahusika, wakiwamo akina mama wa jijini Dar es Salaam ambao ndio walengwa haswa.
“Tunawapongeza pia wenzetu wa Ubalozi wa Kuwait kwa kuguswa kwenye suala la afya ya wanawake hali iliyowasukuma kuingia kwenye tukio letu la kutoa huduma ya bure ya afya ya wanawake,” alisema Dr Binzoo.

Kwa mujibu wa Dr Binzoo, mbali na kuwapima wanawake hao waliohudhuria, pia walikuwa wakitoa elimu na mbinu ya kukabiliana na magonjwa ikiwamo kujiwekea utaratibu wa kupima afya zao mara kwa mara.
Mwenyekiti wa Tanzania Yemen Professional Foundation (TYPF), Dr Ameir Binzoo (kushoto) akimpatia zawadi Balozi wa Kuwait nchini Tanzania, Mheshimiwa Jasem Al Najem kwa udhamini wa siku ya afya ya mwanamke iliyoandaliwa na taasisi hiyo nchini na kudhaminiwa na Ubalozi wa Kuwait kwa ajili ya kuboresha afya ya mwanamke jijini Dar es Salaam.


Balozi wa Kuwait akipata picha ya pamoja na wadau wa taasisi hiyo baada ya kumalizika shughuli ya upimaji afya kwa akina mama.

Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Jasem Al Najem akipewa maelekezo aliposhiriki katika shughuli ya upimaji afya kwa wanawake jijini Dar es Salaam iliyoandaliwa na Tanzania Yemen Professional Foundation (TYPF).


No comments: