Thursday, November 17, 2016

MKUU WA MKOA WA SINGIDA AIPONGEZA HOSPITALI YA KIOMBOI, IRAMBA KUPEWA HADHI YA MBILI NA KUHIMIZA IPATE NYOTA TATU

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew John Mtigumwe akipata maelezo kuhusu kitengo cha huduma ya watoto mahututi (Neonatal Intensive care unit) katika hospitali ya Kiomboi Wilayani Iramba. 
Mwakilishi wa Shirika la Water Aid International akiangalia akinamama wanaosubiri kujifungua wakichota maji, miundombinu ya maji imekarabatiwa na shirika hilo wakishirikiana na shirika la SEMA Tanzania. 
Mwakilishi wa Shirika la Water Aid International akipata maelezo kuhusu kitengo cha huduma ya watoto mahututi (Neonatal Intensive care unit) katika hospitali ya Kiomboi Wilayani Iramba, pembeni yake ni Mganga Mkuu wa Wilaya ya Iramba Dokta Boniphace Richard. 
Akina mama wanaosubiria kujifungua wakiwa nje ya wodi ya kusubiria iliyokarabatiwa kwa ufadhili wa shirika la Water Aid wakishirikiana na shirika la SEMA Tanzania. 
Matenki ya maji yaliyokarabatiwa na Shirika la Water Aid International kwa ushirikiano na shirika la SEMA Tanzani 
Jengo la mbele ni Kichomea taka cha zamani na nyuma yake ni jengo jeupe jipya ni kichomea taka kipya na cha kisasa kilichojengwa na Shirika la Water Aid International kwa ushirikiano na shirika la SEMA Tanzania.

……………………………………………………………………

Na Grace Singida

Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew John Mtigumwe ameipongeza hospitali ya Kiomboi ambayo ni ya Wilaya ya Iramba kwa kupata hadhi ya nyota mbili kutoka sifuri na kuwahamasisha kuendelea kuboresha utendaji ili kupata hadhi ya nyota tatu.

Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe ametoa pongezi hizo alipotembelea hospitali hiyo akiambatana na wageni kutoka shirika la Water Aid International ambalo limefadhili ukarabati wa miundombinu hospitalini hapo kwa shilingi milioni mia tano kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Amesema hospitali ikiwa na hadhi ya nyota tatu itasaidiwa na serikali pamoja na wadau mbalimbali katika kuipatia wataalamu zaidi, kuboreshewa zaidi miundombinu, kuwekwa katika mipango ya kitaifa pamoja na kupata fedha zaidi.

Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe ameongeza kuwa kutokana na kuboreka kwa huduma za hospitali ya Kiomboi wagonjwa wameongezeka sana na hivyo ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa kushirikiana na halmashauri ya Wilaya ya Iramba inaboresha Vituo vya Afya vya Mgongo na Ndago ili vituo huduma za zarudha za Mama na mototo kwa kufanya upasuaji na hivyo kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali ya Kiomboi.

Naye Mkurugenzi wa shirika la Water Aid Tanzania Dokta Ibrahim Kabole ameshukuru ushirikiano wanaoupata kutoka kwa watendaji wa wilaya ya Kiomboi hadi kufanikisha ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya hospitali ya Kiomboi huku akiwataka kuitunza na kuendeleza pale shirika hilo lilipoishia.

Dokta Kabole amesema shirika hilo limekarabati wodi ya wazazi wanaosubiria kujifungua, kuweka miundombinu ya maji na matenki, kujenga kichomea taka kipya chenye hadi ya kisasa hospitalini hapo, kununua friji ya kuhifadhia damu katika kituo cha acya cha ndago na kutoa mafunzo kwa watoa huduma.

Ameongeza kuwa shirika hilo litaendelea kushirikiana na viongozi wa Mkoa wa Singida katika kuboresha sekta ya afya mkoani hapa hasa katika kuboresha afya ya mama na mtoto.

Naye Mganga Mkuu wa Hospitali ya Kiomboi Dokta Boniphace Richard ameishukuru Water Aid na kuongeza kuwa imesaidia hospitali hiyo kupata hadhi ya nyota mbili kutoka sifuri kutokana na kuboreshwa kwa miundombinu ya hospitali hiyo.

Dokta Richard amesema Wodi iliyoboreshwa na shirika hilo kwa sasa inapokea wakina mama wanaosubiria kujifungua 50 ambapo awali walikuwa wana uwezo wa kulaza 30 kwa siku, maji yanahifadhiwa lita 4500 ambazo zinasadia akina mama hao pamoja na uendeshaji wa shughuli nyingine za hospitalini hapo, kupungua kwa vifo vya akina mama kwa asilimia 30.

Ameongeza kuwa uboreshaji wa miundombinu hospitalini hapo kumepelekea kuanzishwa kwa kitengo cha Watoto mahututi katika wodi ya wazazi (Neonatal Intensive care unit), ambapo watoto wanaozaliwa na matatizo mbalimbali wanapatiwa huduma hapo na kuokolewa maisha tofauti na awali.

No comments: