Thursday, November 17, 2016

ANNE MAKINDA AZITAKA HOSPITALI ZA SERIKALI ZIBORESHE HUDUMA ILI ZIPATE WATEJA WENGI WA BIMA YA AFYA.


Mwenyekiti wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda katikati kulia kwake ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mtahew John Mtigumwe na kushoto kwake ni Katibu Tawala Mkoa wa Singida Dokta Angelina Mageni Lutambi na Mkuu wa Wilaya ya Singida Elias Tarimo, wa kwanza kulia ni meneja Mfuko wa Bima ya Tifa Mkoa wa Singida Bwana Adamu Salumu.
Mwenyekiti wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda akikagua hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Singida, mwenye tai nyekundu ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew John Mtigumwe.

Mwenyekiti wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda akikagua hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Singida,kulia kwake ni Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dokta Ramadhani Kabala na kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew John Mtigumwe.


Mwenyekiti wa bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Anne Makinda amezishauri hospitali, vituo vya afya na zahanati za serikali kuboresha huduma za afya ili wananchi waliojiunga katika mifuko ya afya ya jamii (CHF) na mfuko wa bima ya afya washawishike kutumia huduma katika hospitali zao.

Makinda ametoa rai hiyo alipotembelea hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida kujionea huduma za Bima ya afya zinavyotolewa na changamoto zilizopo ili kwa ushirikiano wa mfuko wa bima ya afya na wadau wake waweze kuzitatua.

Amesema hospitali na vituo binafsi au vya mashirika mbalimbali wamekuwa wanufaikaji wakubwa wa kupata wateja wengi wa bima ya afya na mifuko ya afya ya jamii kutokana na kusifiwa kuwa wanatoa huduma bora tofauti na hospitali za serikali ambazo hupata wateja wachache na hivyo kupata faida kidogo.

Makinda amesema hamasa anayoitoa ya kuboresha huduma kwa vituo vya serikali haimaanishi mfuko wa taifa wa bima ya afya hauthamini vituo na hospitali binafsi bali inataka hospitali za serikali kuboresha huduma na kuingia katika ushindani.

Ameongeza kuwa changamoto ya ukosefu wa dawa na vifaa tiba inawakatisha tamaa watumiaji wa bima ya afya pamoja na watu wengine kujiunga hata hivyo mfuko wa bima ya afya na hospitali za serikali zimejipanga kuziondoa changamoto hizo.

Aidha Makinda ameupongeza Mkoa wa Singida kwa kufanya vizuri katika mfuko wa afya jamii na bima ya afya huku akisisitiza kuendelea kuboresha ili Mkoa wa Singida uwe mfano kwa mikoa mingine ya Tanzania.

Akitembelea majengo mapya ya hospitali rufaa iliyopo eneo la Mandewa Makinda amevutiwa sana na majengo hayo huku akiutaka uongozi wa Mkoa kwa kushirikia na wadau wengine hasa mfuko wa bima ya afya kutafuta pesa za ukamilishaji wa majengo muhimu ili huduma zianze kutolewa katika hospitali hiyo kwakuwa itakuwa msaada hata kwa kanda nzima ya kati.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Singida Mheshimiwa Mhandisi Mathew J Mtigumwe  amemshukuru Anne Makinda kwa kuutembelea mkoa wa Singida ili kujionea  huduma za Bima ya afya zinavyotolewa.

Mheshimiwa Mhandisi Mtigumwe amemuahidi Makinda kuwa Mkoa utaendeleza ushirikiano mzuri na Mfuko huo na kuomba waendelee kutoa ushirikiano wa vifaa tiba na ukarabati wa miundombinu ya hospitali na vituo vya afya vya serikali ili kuboresha huduma za afya Mkoani Singida.

Ameongeza kuwa Mkoa utaendelea kuhamasisha wananchi kujiunga na mfuko wa afya ya jamii na bima ya afya ili wapate huduma bora hata wakati wakiwa na upungufu wa fedha kwani bima huokoa maisha. MAELEZO YA PICHA

No comments: