Thursday, October 20, 2016

Mtandao wa Mawasiliano wa Serikali kuipunguzia Serikali gharama ya mawasiliano kwa njia ya simu




Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao (eGA) Bi. Suzan Mshakangoto akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu matumizi ya Mtandao wa Mawasiliano wa Serikali leo Jijini Dar es Salaam. Taasisi 72 za Serikali tayari zimekwishaunganishwa na Mtandao huo kupitia Mkongo wa Taifa.
: Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao (eGA) Bi. Suzan Mshakangoto akiongea na mtu kutoka Taasisi ya Uongozi wa Elimu (ADEM) ya Bagamoyo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu matumizi ya Simu zilizounganishwa na Mtandao wa Mawasiliano wa Serikali leo Jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya waandishi wa habari wakifuatilia maelezo kutoka kwa Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa Wakala ya Serikali Mtandao (eGA) Bi. Suzan Mshakangoto (hayupo pichani) wakati wake na waandishi hao kuhusu matumizi ya Mtandao wa Mawasiliano wa Serikali, leo Jijini Dar es Salaam. Picha na: Frank Shija, MAELEZO.

Na: Lilian Lundo – MAELEZO

Serikali kupitia Wakala ya Serikali Mtandao (eGA) imeendelea kutekeleza uunganishwaji wa mtandao wa Mawasiliano wa Serikali ambapo mpaka sasa Taasisi 72 zimeunganishwa na mtandao huo. Hayo yamesemwa na Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano eGA Suzan Mshakangoto alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu utekelezaji wa miundombinu ya Tehama inayohusisha Serikali, leo Jijini Dar es Salaam.

Suzan amesema kuwa Taasisi za Serikali zilizounganishwa na mtandao huo zitakuwa zinawasiliana kwa gharama ndogo kwa kutumia simu zitakazokuwa zikitumika kama ‘extension’ ambazo zitakuwa zinatumia internet kupitia Mkongo wa Taifa. “Mtumishi wa Taasisi moja katika taasisi zilizounganishwa na mtandao huo anaweza kupiga simu kwenda taasisi nyingine ya nje ikawa kama amepiga simu ya ‘extension’ ndani ya ofisi moja,” alifafanua Suzan.

Vile vile Taasisi za Serikali zitapunguza gharama za kuchajiwa huduma za internet kutoka kwa watoa huduma binafsi ambao gharama zao ziko juu ukilinganisha na huduma inayotolewa na wakala wa Serikali. Aidha Taasisi na Idara zote za Serikali zitakuwa ndani ya mtandao na mtoa huduma mmoja wa huduma za mtandao ambapo itasaidia kwenye utunzaji wa nyaraka za Serikali na kurahisha mawasiliano ndani ya taasisi hizo.

Hivyo basi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora kwa kushirikiana na wakala imetoa mafunzo kwa wataalamu wa TEHAMA na Makatibu Muhtasi kutoka taasisi zilizounganishwa na mtandao huo juu ya uendeshaji na usimamizi wa mtandao wa Serikali pamoja na matumizi ya simu zinazotumia itifaki (IP Phones).

Mpango wa Serikali ni kuzifikia Ofisi za Mikoa na Halamashauri zote hapa nchini ili kutumia mawasiliano ya simu za itifaki, barua pepe na mifumo ya TEHAMA katika kubadilishana taarifa, ambapo kufikia Disemba 2016 taasisi nyingine 77 kutoka mikoa 20 ya Tanzania Bara zitakuwa zimeunganishwa kwenye mtandao huo.

No comments: