Tuesday, July 5, 2016

WAKUU WAPYA WA WILAYA ZA MKOA WA MWANZA WAPEWA MAJUKUMU MARA BAADA YA KUAPISHWA

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, akizungumza katika hafla ya kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza hii leo, Julai 04,2016 katika viunga vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Na BMG
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, amewataka wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa huo kuhakikisha wanashirikiana na kamati za ulinzi na usalama pamoja na wananchi kwenye wilaya hizo ili kukomesha mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi na vikongwe yanayochangiwa na imani potofu za kishirikina.

Akizungumza baada ya kuwaapisha wakuu hao wa wilaya zote saba za mkoa wa Mwanza, Mongella amesema kwa muda mrefu mkoa wa Mwanza umekumbwa na matukio ya mauaji ya watu wenye ualbino na vikongwe kutokana na imani za kishirikina na kwamba wakati umefika kuhakikisha matukio hayo yanakwisha.

Amesema mkoa huo umejipanga vyema kuhakikisha matukio hayo yanakuwa historia kwa kuwa hakuna binadamu mwenye mamlaka ya kutoa uhai wa binadamu mwenzake kwa sababu yoyote ile.

Mkuu huyo wa mkoa amewapa mwezi mmoja wakuu hao wapya wa wilaya kumaliza tatizo la madawati pamoja na kuwachukulia hatua watumishi hewa 1,057 waliogundulika kwenye wilaya zote za mkoa wa Mwanza.

Mongella amewata wakuu hao wa Wilaya kuhakikisha kwamba matumizi ya dawa za kulevya katika wilaya zao yanakomeshwa ambapo amepiga marufuku matumizi ya shisha katika hoteli na klabu zote za muziki pamoja uchezaji wa "pool table" na unywaji wa pombe saa za kazi huku akitanabaisha kwamba atakaeshindwa kutekeleza maagizo hayo ni dhahiri shahiri kwamba atakuwa ameshindwa kusimamia majukumu yake.

Aidha Mongella amemtaka mkuu wa Wilaya ya Nyamagana kuhakikisha kwamba hadi ifikapo Agosti mosi mwaka huu awe amewaondoa wafanyabiashara ndogondogo waliosambaa kwenye maeneo mbalimbali ya katikati ya jiji Mwanza.

Wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza walioapishwa, wamesema wamejipanga vyema kushirikiana na viongozi wengine pamoja na wananchi katika Wilaya zao ili kuhakikisha kwamba wanatekeleza vyema majukumu yao ikiwemo kuimarisha suala la ulinzi na usalama katika jamii.

Wakuu wapya wa Wilaya saba za Mkoa wa Mwanza walioapishwa hii leo ni Mary Onesmo Tesha wa Nyamagana, Estomin Francis Chang’a wa Ukerewe, Hadija Rashid Nyembo wa Magu, Juma Samwel Sweda wa Misungwi, Emmanuel Enock Kipole wa Sengerema, Dkt.Leonard Moses Masale wa Ilemela na Mhandisi Mtemi Msafiri Simion wa Kwimba ambapo wote wamekabidhiwa vitendea kazi ikiwemo Katiba ya Tanzania pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015/20.
Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Mh.Emmanuel Enock Kipole (kulia), akiapa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella (kushoto).
Mkuu wa Wilaya ya Ukerewe, Mhe.Estomin Francis Chang’a (kushoto) akiapa mbele ya mkuu wa mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (kulia).
Mkuu wa Wilaya ya Magu, Mhe.Hadija Rashid Nyembo, akiapa hii leo
Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Mhe.Juma Samwel Sweda, akiapa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (kushoto).
Mkuu wa Wilaya ya Ilmela, Mhe.Dkt.Leonard Moses Masale (kushoto) akiapa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (katikati).
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Mhe.Mary Onesmo Tesha, akiapa hii leo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (kushoto)
Mkuu wa Wilaya ya Kwimba, Mhandisi Mhe.Mtemi Msafiri Simion (kulia), akiapa mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhe.John Mongella (katikati).
Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, CP.Clodwin Mtweve, akizungumza katika hafla fupi ya kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza iliyofanyika hii leo katika viunga vya ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Sala kutoka kwa Sheikh mkuu wa Bakwata mkoani Mwanza, kabla ya kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za mkoa wa Mwanza
Sala kutoka kwa Kiongozi wa Umoja wa Makanisa Jijini Mwanza, kabla ya kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za mkoa wa Mwanza
Afisa Habari na Mahusiano kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza
Baadhi ya Wakuu wa Wilaya waliomaliza muda wao, ambapo kushoto ni aliekuwa Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana, Baraka Konisaga maarufu kwa jina la Mtumishi wa Mungu akiwa pamoja na aliekuwa Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Manju Msambya.
Meneja wa Shirika la Posta mkoani Mwanza akifuatilia shughuli ya kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza
Viongozi mbalimbali wa Serikali na Siasa mkoani Mwanza
Viongozi wakifuatilia zoezi la kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza
Viongozi wa dini mkoani Mwanza, wakifuatilia zoezi la kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza
Baadhi ya viongozi kutoka kamati ya ulinzi na usalama mkoani Mwanza, wakifuatilia zoezi la kuwaapisha wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza
Wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, wa nne waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na Wakuu wapya wa Wilaya za Mkoa wa Mwanza (waliosimama nyuma) na viongozi wa kamati ya ulinzi na usalama mkoa wa Mwanza.

No comments: