Thursday, June 23, 2016

BENKI YA DUNIA YAIPATIA TANZANIA SHILINGI BILIONI 440 KWAAJILI YA KUSAIDIA KAYA MASIKINI

Na Benny Mwaipaja, WFM 

Serikali kupitia Wizara ya Fedha na Mipango imesaini hati ya makubaliano na Benki ya Dunia itayoiwezesha Tanzania kupata nyongeza ya fedha katika mradi wa Tasaf kiasi cha Shilingi Bilioni 440.

Hati hiyo ilisainiwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Dkt. Servacius Likwelile na Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Dunia Bella Bird, Makao Makuu ya Wizara ya Fedha, Dar es Salaam, leo, Juni 23, 2016.

Akiongea wakati wa kusaini hati hiyo Dkt. Likwelile alisema kuwa fedha hizo  zitaelekezwa katika mradi wa Tasaf II kwa ajili ya kuziwezesha kaya maskini kukuza kipato chao kupitia ajira za muda zitakazowawezesha kupeleka watoto shule na kuwapatia huduma za afya.

Aliongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2015/2016 Serikali kwa kushirikiana na Benki ya Dunia imefanya kazi kubwa iliyowezesha miradi kumi kupitishwa ambayo ina thamani ya Shilingi Trilioni 1.9.

"Miongoni mwa miradi iliyopata ufadhili ni pamoja na mradi wa kuboresha mazingira ya biashara uliopata shilingi Bilioni 168, mradi wa kusambaza umeme vijijini (REA), uliopata Shilingi Bilioni 440" Aliongeza Dkt. Likwelile.

Aidha, alisema kuwa Serikali inaendelea na majadiliano na Benki hiyo kwa ajili ya kuboresha Bandari ya Dar es Salaam, ambapo kiasi cha dola Milioni 600 zimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.

Dkt. Likwelile ameishukuru Benki ya Dunia kwa mchango wake mkubwa na kusema kuwa Serikali itahakikisha kuwa inazisimamia taasisi zinazotekeleza miradi hiyo ili ziweze kutumia fedha hizo vizuri na kwa malengo yaliyokusudiwa.

Kwa upande wake Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Dunia, Bella Bird, amepongeza juhudi za Serikali ya awamu ya tano katika kupambana na rushwa na kuweka mazingira rafiki kwa sekta binafsi.

Aliongeza kuwa sekta binafsi ndizo zinatoa ajira kwa wingi na kusaidia kuchangia katika kuongeza mapato ya Serikali. Ameahidi kuwa Benki yake itaendelea kushirikiana na Tanzania ili kuiwezesha kufikia malengo yake ya kiuchumi na kijamii kwa faida ya wananchi wake.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Servacius Likwelile (wa pili kulia) na Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania Bi. Bella Bird (wa pili kushoto), wakisaini Hati ya Makubaliano itakayoiwezesha Tanzania kupata nyongeza ya Sh. Bilioni 440 kwa ajili ya mradi wa Tasaf II. Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Wizara Jijini Dar es salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Servacius Likwelile na Muwakilishi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania Bi. Bella Bird wakibadilishana Hati ya Makubaliano itakayoiwezesha Tanzania kupata nyongeza ya Sh. Bilioni 440 kwa ajili ya mradi wa Tasaf II, Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Wizara Jijini Dar es salaam.
Waandishi wa habari pamoja na wadau wengine wakifuatilia maelezo ya Hati ya Makubaliano itakayoiwezesha Tanzania kupata nyongeza ya Sh. Bilioni 440 kwa ajili ya mradi wa Tasaf kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Servacius Likwelile na Mwakilishi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania Bi. Bella Bird. Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Wizara Jijini Dar es salaam
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Servacius Likwelile akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu Makubaliano yaliyofanywa kati ya Tanzania na Benki ya Dunia ya ili kupata nyongeza ya Sh. Bilioni 440 kwa ajili ya mradi wa Tasaf II. Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Wizara Jijini Dar es salaam

Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango na Mlipaji Mkuu wa Serikali Dkt. Servacius Likwelile akibadilishana mawazo na Mratibu Maendeleo ya Sekta Binafsi na SAGCOT kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu mara baada ya kumaliza kusaini Hati ya Makubaliano itakayoiwezesha Tanzania kupata nyongeza ya Sh. Bilioni 440 kwa ajili ya mradi wa Tasaf II. Tukio hilo limefanyika katika Ukumbi wa Wizara Jijini Dar es salaam.

No comments: