Tuesday, June 14, 2016

Balozi wa China Nchini Ajitokeza Kuchangia Damu Muhimbili

Na Neeema Mwangomo, Dar es salaam

Balozi wa China nchini Dk. LU Youqing leo amejitokeza kuchangia damu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa lengo la kuwahamasisha wananchi kuwa na moyo wa kuchangia damu, lakini pia kuadhimisha siku ya wachangia damu Duniani ambayo huadhimishwa Juni 14 kila mwaka.

Balozi Youqing amesema wakati tukiadhimisha siku hii muhimu, tunatukumbushwa kujenga utamaduni wa kuchangia damu kwa upendo ili kuokoa maisha ya wale wenye uhitaji wa damu.

Pamoja na mambo mengine, Balozi Youqing amesisitiza kwamba Serikali ya China itaendelea kushirikiana na Tanzania katika shughuli mbalimbali ikiwamo kuisaidia sekta ya afya .

Awali akizungumza kabla ya shughuli kuchangia damu, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Makwaia Makani amemshukuru Balozi huyo wa China kwa kuwa Balozi wa kwanza wa kigeni kujitokeza kuchangia damu kwenye hospitali hiyo kwani hatua hiyo imeonyesha ni jinsi gani anaguswa katika kuokoa maisha ya Watanzania.

“Timu ya wataalamu mbalimbali wa afya kutoka China wamekua na ushirikiano mzuri na wa muda mrefu na hospitali hiyo katika kusaidia huduma za afya na tumekuwa tukifanya nao kazi tangu mwaka 1968,” amesema Kaimu Mkurugenzi Makani.

Akifafanua amesema kimsingi mahitaji ya damu ni makubwa kwani Hospitali ya Taifa Muhimbili inahitaji chupa za damu 100 hadi 150 kwa siku, lakini chupa zinazopatikana ni 60 na kwamba upungufu ni asilimia 25.

Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Maabara wa MNH Dk, Alex Magesa amesema pamoja na jitihada zinazofanywa na Hospitali hiyo za kukusanya damu, lakini zoezi hilo linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo uchache wa vitanda vinavyotumika wakati wa kutoa damu, jokofu kubwa la kiibailojia kwa ajili ya kuhifadhia damu na usafiri wa kwenda kukusanya damu nje ya Hospitali.

Katika kuadhimisha siku ya wachangia damu duniani Hospitali ya Taifa Muhimbili inatembelea maeneo mbalimbali ya wazi ikiwamo vyuoni ili kukusanya damu.

Maadhimisho hayo ambayo kitaifa yanafanyika mkoani Dodoma yamebeba kauli mbiu ‘Damu inaunganisha kila mtu.’

Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Makwaia Makani akimkaribisha Balozi wa China nchini Tanzania, Dk. LU Youqing ambaye amefika kwenye hospitali hiyo LEO kwa ajili ya kuchangia damu katika maadhimisho ya siku ya damu duniani.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Makani akisoma taarifa fupi kwa Balozi Dk. LU Youqing kabla ya kuchangia damu leo.
Baadhi ya madaktari wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) na wa China wakimsikiliza Kaimu Mkurugenzi, Makani wakati akisoma taarifa fupi kwa balozi huyo.
Balozi wa China, Dk. LU Youqing nchini Tanzania akizungumza na waandishi wa habari LEO katika hospitali hiyo. Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa Mohammed Janabi na kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa MNH, Makwaia Makani.
Baadhi ya Madaktari wakimsikiliza Balozi huyo leo katika hospitali hiyo.
Mkurugenzi wa Upasuaji, John Kimaro na Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi, Praxeda Ogweyo wakifuatilia mkutano huo Leo kwenye hospitali hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa Mohammed Janabi akizungumza na waandishi wa habari kwenye hospitali hiyo. Kutoka kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa MNH, Makani na Balozi wa China, Dk. LU Youqing.
Sista Elizabeth Mweta akimwezesha Balozi wa China, Dk. LU Youqing kuchangia damu leo kwenye hospitali hiyo.
Balozi Dk. LU Youqing akiendelea kuchangia damu katika hospitali hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo akimkabidhi cheti Balozi Dk. LU Youqing baada ya kuchangia damu leo.
Balozi Dk. LU Youqing akinywa chai baada ya kukamilisha shughuli ya uchangiaji damu leo katika hospili hiyo.

No comments: