Wednesday, June 1, 2016

Baada ya kumalizika kwa mradi wa SCMS, USAID yaahidi kuendelea kuisaidia Tanzania

Baada ya kufanyika nchini kwa miaka 10, mradi wa SCMS ambao ulikuwa ukisimamiwa na John Snow Incorporated (JSI) kwa ushirikiano na Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii Jinsia, Wazee na Watoto, Shirika la Misaada la Watu wa Marekani (USAID) limeiahidi serikali ya Tanzania kuwa litaendelea kuisaidia katika misaada mbalimbali ya afya licha ya kumalizika kwa mradi huo.

Hayo yamesemwa na Naibu Mkurugenzi wa USAID nchini, Tim Donnay katika mkutano ambao ulikutanisha wadau mbalimbali wa afya ili kujadili mradi wa SCMS ambao umefikia tamati baada ya kufanyika nchini kwa miaka 10.

Bi. Donnay alisema serikali ya Marekani kupitia USAID imejipanga kuendelea kuisaidia Tanzania katika sehemu mbalimbali ambazo zinahusu Afya.

“USAID itaendelea kuisaidia Tanzania ili kuwezesha kufikiwa kwa malengo ya upatikanaji wa huduma bora wa kiafya ... kumalizika kwa mradi huu hukutafanya kusitishwa kwa huduma ambazo zinatolewa kwa sasa,” alisema Bi. Donnay.
Naibu Mkurugenzi wa USAID nchini, Tim Donnay akiwasilisha ujumbe kwa niaba ya serikali ya Marekani katika mkutano wa hitimisho wa mradi wa SCMS.

Nae mgeni rasmi katika mkutano huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dr. Mpoki Ulisubya alisema kufanyika kwa mradi huo nchini kumewezesha kusaidia kuboreshwa kwa kasi huduma za afya tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.

“Mradi huu umetusaidia sana awali hata utolewaji wa dawa kwa waathirika wa UKIMWI ulikuwa ni laki na nusu kwa mwaka ila kwa sasa kuna upatikanaji wa dawa hadi laki nane kwa mwaka,

“Mbali na hiyo pia wametujengea maghala ambayo yanatumika kuhifadhi dawa na hata kusaidia kuweza kuwasogezea huduma wananchi ambazo awali hazikuwa zikitolewa,” alisema Ulibusya.

Na Rabi Hume.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dr. Mpoki Ulisubya akitoa neno la shukrani kwa niaba ya serikali katika mkutano wa hitimisho la mradi wa SCMS uliotolewa na USAID na kusimamiwa utekelezaji wake na John Snow Incorporated (JSI) kwa kushirikiana na Wizara ya Afya. (Picha zote na Rabi Hume).
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Zanzibar, Dr. Juma Malik Akil akitoa neno la shukrani kwani niaba ya serikali ya Zanzibar baada ya kumalizika kwa mradi wa SCMS.
Mfamasia wa Serikali, Henry Irunde akielezea utaratibu wa usambazaji wa dawa nchini uliotumika wakati ambao mradi huo ulikuwa ukifanyika nchini.
Baadhi ya wadau wa sekta ya afya walioshiriki mkutano huo.
Mkurugenzi wa John Snow Incorporated (JSI), Deo Kimera akizungumzia Mradi wa SCMS.
Baadhi ya wafaidika wa mradi wa SCMS wakielezea jinsi mradi huo umeweza kuwasaidia wao binafasi na katika sehemu ambazo wanafanyia kazi.
Baadhi ya wahudhuriaji wa mkutano huo uliofanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere wakiwasikiliza wafaidika wa mradi wa SCMS.
Muonekano wa kazi ambazo zimefanywa na mradi wa SCMS kwa kipindi cha miaka 10 tangu ulipoanza mwaka 2005.
Baadhi ya waandaji wa mkutano huo wakiwa katika picha ya pamoja.

No comments: