Friday, May 6, 2016

zanchick yajipanga kushirikiana na wizara ya kilimo,maliasili,mifugo na uvuvi kuwasaidia wafugaji na wakulima wadogowadogo.

Uongozi wa Shamba la Kuku Maruhubi { Zanchick } umejipanga kushirikiana na Wizara ya Kilimo,  Maliasili, Mifugo na Uvuvi katika kuwasaidia wafugaji na wakulima wadogo wadogo Nchini ili waendeshe miradi yao ya uzalishaji katika misingi ya kitaaluma.

Mkuu na muanzilishi wa Shamba hilo Dr. David Elua akiuongoza ujumbe wa Viongozi watatu wa shamba hilo alieleza hayo wakati akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwake vuga Mjini Zanzibar.

Dr. David Elua alisema mpango huo uliolenga kutekelezwa pande zote mbili za Muungano, Tanzania Bara na Zanzibar utawanufaisha wanachi wa kipato cha chini zaidi ya 45,000 kwa kupata ajira katika uendeshaji wa miradi ya ufugaji kuku kwa kutumia njia ya kisasa.Alisema katika hatua ya awali shamba hilo tayari limeshatoa ajira zipatazo 300 katika kiwanda chake cha kutotoa vifaranga vya Kuku kiliopo Maruhubi juhudi zikiwekwa zaidi katika kuunga mkono azma ya Serikali Kuu katika uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo.

Dr. David alimfahamisha Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba Sera hiyo iliyoanzishwa na Serikali na kuanza kukubalika kwa baadhi ya mashirika na taasisi za uwekezaji ndani na nje ya nchi itawasaidia zaidi vijana kupata ajira badala ya kusubiri ajira za serikali ambazo ni finyu kwa miaka ya sasa.

Akizungumzia ugonjwa wa kuambukiza wa kipindupindu ulioikumba Zanzibar katika Kipindi hichi Mkuu na Muanzilishi wa Shamba hilo la Kuku Maruhubi Dr. David alisema Uongozi wake umepata mshtuko kutokana na janga hilo linaloendelea kusumbua wananchi hasa Watoto wadogo.

Dr. David alisema Zanchick imeahidi kutoa mchango wa shilingi Milioni 10,000,000/- ili zisaidie nguvu ya Serikali katika mapambano yake dhidi ya maradhi hayo yaliyopoteza maisha ya watu wasiopungua 53 tokea yavikumbe Visiwa vya Zanzibar mwezi septemba mwaka uliopita.

Akitoa shukrani zake kwa Uongozi wa Shamba hilo la Kuku Maruhubi {Zanchick} Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeahidi kuzifanyia kazi changamoto zote zinazoikumba Taasisi hiyo katika kuendesha miradi yake ya uwekezaji hapa Nchini.

Balozi Seif alisema Serikali imeamua kuimarisha miundombinu katika sekta mbali mbali za Uwekezaji ili kujenga mazingira bora yatakayotoa fursa kwa Taasisi na Makampuni ndani na nje kuwekeza miradi yao ya kiuchumi ili hatimae isaidie uchumi wa Taifa.

Shamba la Kuku Maruhubi ni miongoni mwa Taasisi za uwekezaji zilizohamasika kuja kuwekeza miradi yao Nchini kufuatia ziara ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif aliyoifanya Nchini Marekani mwezi Oktoba mwaka 2011 kwa mualiko wa shirika la uwekezaji vitega uchumi Barani Afrika la Nchini Marekani.

Ziara hiyo ya Balozi Seif ililenga kuitangaza Zanzibar kwa taasisi na mashirika ya Marekani kuangalia uwezekano wa kuwekeza miradi yao katika maeneo yaliyomo ndani ya Sekta za Utalii, Biashara, Elimu, Kilimo, Afya, Miundombinu pamoja na Mazingira.
 
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
6/5/2016. 

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akisalimiana na Ujumbe wa Viongozi wa Shamba la Kuku Maruhubi { Zanzchick } uliofika ofisini kwake kubadilishana mawazo juu ya sekta ya uwekezaji.Aliyempa mkono ni Mkuu na muanzilishi wa shamba hilo Dr. David Elua, wa kwanza kutoka kulia ni Meneja operesheni wa Shamba hilo Bw. Christopher Kontonasios na wa kwanza kutoka kushoto ni Nd. Issa Kassim.
 Balozi Seif akizungumza na Ujumbe wa Viongozi wa Shamba la Kuku Maruhubi { Zanzchick } ukiongozwa na Mkuu na muanzilishi wa Shamba hilo Dr. David Elua.
Balozi Seif akiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe wa Viongozi wa Shamba la Kuku Maruhubi { Zanzchick } mara baada ya mazungumzo yao.Kulia ya Balozi Seif ni Mkuu na muanzilishi wa Shamba hilo Dr. David Elua, Bwana Michael Mantheakis, Nd. Issa Kassim na kushoto ya Balozi Seif ni Meneja operesheni wa Shamba hilo Bw. Christopher Kontonasios.Picha na – OMPR – ZNZ.

No comments: