Monday, May 16, 2016

TAMKO LA WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KULAANI TUKIO LA UKATILI WA KINGONO ALILOFANYIWA MWANAMKE NA PICHA ZAKE KUSAMBAZWA KATIKA MITANDAO


Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesikitishwa na tukio la ubakaji na udhalilishwaji lililofanywa na wanaume wawili dhidi ya mwanamke mmoja, ambaye alishurutishwa kuwa mtupu, kufanya ngono bila ridhaa yake, kupigwa picha na kusambazwa katika mitandao ya kijamii hapa nchini.

Wizara inalaani vikali kitendo hiki cha ukatili na udhalilishaji kilichofanywa na wanaume wawili, ambao wamekamatwa na Polisi kwa kuhusishwa na udhalilishaji huo. Mazingira ya ukatili huo yanahuzunisha, kwani inaelezwa kuwa wanaume hao kwa wakati mmoja walihusika kumwingilia kimwili pasipo ridhaa yake, ilihali,wakimpiga picha za tukio zima la ubakaji huo. Kitendo hiki, ni ukatili usio na kifani, maana kimefedhehesha utu wake binafsi na kudhalilisha familia yake, na wanawake kwa ujumla. Aidha, kitendo hiki kinaweza kusababisha madhara makubwa kwa mwanamke huyu kimwili,kisaikolojia, kijamii na kihisia.

Wizara inaamini kuwa, vitendo hivi vya ubakaji na udhalilishaji havistahili kuvumiliwa hata kidogo, maana vinaashiria kuwepo kwa matumizi ya nguvu, vitisho, kulazimishwa kuingiliwa, na kuna uwezekano mkubwa wa mwanawake huyu kuwa katika hali ya hatari zaidi ambayo inagusa maisha yake binafsi, jambo ambalo ni haki yake ya msingi.
Naomba ieleweke kuwa, Wizara haitetei ukosefu wa uaminifu miongoni mwa wanandoa au watu wenye mahusiano ya kimapenzi, bali tunasisitiza kwamba mwanawake sawa na binadamu wengine anastahili na ana haki ya kuthamaniwa utu wake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ikumbukwe kuwa uhuru na haki ya kufanya mapenzi ni hiari na kamwe hayafanyiki kwa kulazimishwa.
Navipongeza vyombo vya usalama kwa weledi wa kazi yao ambavyo vimewasaka na na kufanikisha kupatikana kwa watuhumiwa wa ukatili huo. Serikali itahakikisha mkondo wa sheria unafuatwa kuhakikisha haki inatendeka. 
Natoa wito kwa wananchi wote kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha vitendo hivi vinakoma kabisa katika jamii zetu za Kitanzania. Hakika huu sio utamaduni wetu! ni lazima tuhakikishe tunapambana kukomesha tabia za udhalilishaji wa wanamke na watoto wa kike kwa nguvu zote. Tujenge tabia ya kutoa taarifa kwa haraka matukio yote ya ukatili dhidi ya wanawake yanapotokea katika jamii zetu. Aidha, natoa rai kwa mamlaka zinazohusika na ulinzi na haki za wanawake zihakikishe zinaelimisha jamii kubadilika na kuhakikisha wanawake wanalindwa maana hawa ni mama zetu, dada, zetu, na binti zetu. Pia, natoa wito kwa viongozi mbalimbali katika jamii kutofumbia macho matukio ya udhalilishaji wa wanawake yanayo kiuka maadili ya jamii yetu.

Naomba kutoa rai kwa wawakilishi wa kisiasa, watendaji, na wadau wa haki za watoto kutumia nafasi zetu katika kuelimisha wananchi kuondokana na tabia za ukatili dhidi ya wanawake, hususan suala zima la udhalilishaji wa picha za utupu kupitia mitandao ya kijamii, tabia ambayo imeibuka kwa kasi kubwa katika siku za hivi karibuni. Kamwe Taifa haliwezi kuhesabika kuwa limeendelea kama utu wa mwanamke utwezwa na kudhalilishwa usoni mwa mataifa mengine duniani.

 Erasto T. Ching’oro
Mkuu wa Kitengo cha Mawasilino
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

16/5/2016

No comments: