Friday, April 29, 2016

WAZAZI WAWALINDE WATOTO NA AJALI BARABARANI.

Na. Catherine Sungura.
Wazazi nchini wametakiwa kuwakinga watoto wao wakati waendeshapo magari kwa kuhakikisha wanawafunga mikanda ili kuwaepusha na ajali za barabarani na kudhibiti madhara yatokanayo na ajali.

Rai hiyo imetolewa leo jijini hapa na kaimu  kamanda kikosi cha usalama barabarani Tanzania,Kamishna Msaidizi wa Polisi Fortunatus Musilimu    wakati akifungua  mafunzo kwa Mawakili,Mahakimu ,Waendesha Mashitaka na Askari wapelelezi wa kesi za ajali za barabarani,iliyoandaliwa na wizara ya afya kwa kushirikiana na shirika la Afya Duniani (WHO) kupitia mpango wa Bloomberg Initiative Global Road Safety.

Alisema wazazi wengi wanapokuwa wanaendesha magari hawawafungi mikanda watoto wao na hivyo ajali inapotokea watoto wanakuwa ni wahanga wakubwa kwa kupoteza maisha au kupata ulemavu wa kudumu
“Wazazi mnawalindaje watoto,baba anaendesha gari,mtoto yupo kwenye usukani anaendesha nae gari,hiyo siyo sahihi ,tuwalinde watoto wawe salama kwa kuvaa mikanda”

Aidha, Kamanda   Musilimu alisema tatizo la ajali barabarani nchini imekua ikiongezeka kila mwaka na hii ni kutokana na wananchi kutokuona kama ajali ni tatizo kubwa na la haraka ambalo linafanya kuongezeka kwa vifo nchini kulinganisha na magonjwa mengine na hivyo kupoteza nguvu kazi ya taifa kiuchumi.

“Watu bado hawaoni kama ajali ni tatizo ,vifo inatokea hapohapo na watoto wanabaki kuwa tegemezi,hizi ni changamoto hivyo mshirikiane kubadilishana uzoefu ili muweze kutatua kesi zote zinazowafikia na kupunguza malalamiko pamoja na kutenda haki,alisema.

Takwimu za hapa nchini kwa  miaka miwili zinaonesha mwaka 2014 zilitokea ajali 14,360,vifo 3,760 na majeruhi 14,530 na mwaka 2015 zilitokea ajali 8,337,vifo 3,468 na majeruhi 9,383,hata hivyo Ripoti ya Shirika la Afya Duniani ya mwaka 2015 zinaonesha ajali huua watu 1.25 milioni Duniani kila mwaka, watu kati ya 20 na 50 milioni hujeruhuwa kila mwaka na hivyo  asilimia 90 ya ajali hizi na vifo hutokea katika nchi zenye uchumi wa kati na wa chini kama Tanzania.

Kamanda Musilimu alisema kasi hii ya ajali ikiendelea hadi ifikapo mwaka 2030,ajali itashika nafasi ya 5 kwa kusababisha vifo Duniani.
Mradi wa Bloomberg Initiatives ni mradi wa miaka mitano hapa nchini umeanzishwa mwaka 2015 ukiwa na nia ya kuweka vipaumbele vya kuzuia vyanzo vya ajali hatarishi kama vile mwendo kasi,kutokuvaa kofia ngumu,kutokufunga mikanda,vifaa maalumu vya kuwakinga watoto kwenye magari pamoja na ulevi.


No comments: