Monday, April 4, 2016

Balozi Masilingi amtembelea Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar

Balozi wa Tanzania Nchini Marekani Balozi Wilson Masilingi akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofika Vuga kubadilishana naye mawazo ukiwemo mchakato wa uchaguzi mkuu.
Balozi Seif akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo yake na Balozi wa Tanzania Nchini Marekani Balozi Wilson Masilingi Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Balozi Masilingi alimthibitishia Balozi Seif juhudi atakazochukuwa katika kuieleza Dunia hali halisi ya Tanzania ilivyo hivi sasa baada ya kumalizika kwa uchjaguzi Mkuu. Picha na – OMPR – ZNZ.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema kwamba Uhusiano wa Kidiplomasia uliopo kati ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Marekani sambamba na Zanzibar utaendelea kuwepo kama kawaida kwa faida ya Wananchi wa pande mbili husika.

Alisema kinachohitajika kwa sasa katika kukabiliana na changamoto zinazojitokeza kwenye miradi ya Kiuchumi na Maendeleo ni kupatiwa Taaluma kwa watendaji wa Taasisi na mashirika ya Misaada kuelewa vyema  mazingira halisi ya Tanzania hasa Zanzibar kisiasa na ustawi wa jamii.

Balozi Seif Ali Iddi alieleza hayo hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar wakati akibadilishana mawazo na Balozi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Marekani Balozi Wilson Masilingi anayefanya kazi zake Jijini Washington  DC.

Alisema wapo watendaji wa baadhi ya Mashirika na Taasisi za Misaada ya Maendeleo wanaofanya kazi  Nchini ambao hupata ushawishi unaombatana na utashi wa watu wenye nia isiyo sahihi kwa maendeleo ya Wananchi na matokeo yake kuisumbua jamii ya walio wengi.

“ Uhusiano wetu na Marekani bado ni mzuri na utaendelea vyema, lakini kinachohitajika kwa Taasisi nyengine za Misaada ni kupatiwa Taaluma ya kuyaelewa mazingira halisi ya Tanzania hasa ule upande wa Zanzibar ”. Alisema Balozi Seif.

Balozi Seif alisema Mashirika na Taasisi zinazotoa misaada hapa Nchini lengo lake kuu ni kuimarisha uhusiano kupitia Balozi zake na kamwe si sindikizo la baadhi ya watendaji wake kutaka kufanya wanavyotaka kibinafsi.

Akizungumzia suala la uchaguzi wa marejeo Zanzibar uliofanyika Tarehe 20 Machi mwaka huu, Balozi Seif alimueleza Balozi Masilingi kwamba kazi inayowakabili Watanzania hivi sasa ni kujielekeza zaidi katika kuimarisha miradi ya kiuchumi badala ya kuendeleza porojo.

Alisema Tume ya Uchaguzi Zanzibar { ZEC } ilifikia maamuzi ya kufuta Uchaguzi na matokeo yake yote kutokana na hitilafu kadhaa zilizojitokeza zikiwemo za kuchafuliwa kwa matokeo makusudi kwenye vituo mbali mbali.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimpongeza Balozi Wilson Masilingi kwa juhudi kubwa anazoendelea kuzichukuwa za kuieleza Dunia hali halisi ya mazingira ya Tanzania ilivyo kiuchumi na kisiasa.

Alisema jitihada za Balozi Masilingi na umakini wake katika kutekeleza majukumu yake ndizo zilizopelekea kubadilishwa kituo kidogo cha kazi na kuhudumia kituo kikubwa zaidi.

Mapema Balozi wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Nchini Marekani  Balozi Wilson Masilingi anayefanyia kazi zake Jijini Washington DC aliwashukuru Viongozi na Wananchi wa Tanzania Bara pamoja na Zanzibar kwa kumaliza zoezi zima la uchaguzi katika misingi ya amani na utulivu.

Alisema Watanzania walio nje ya Nchi hasa katika Majimbo mbali mbali ya Marekani walikuwa katika mazingira magumu pale waliposikia uchaguzi Mkuu wa Zanzibar umefutwa pamoja na matokeo yake yote hasa ikizingatiwa historia ya  Zanzibar katika medani ya Kisiasa.

Balozi Masilingi alieleza kwamba faraja ya Watanzania hao ilirejea kama kawaida pale Viongozi wa Kitaifa walipokuwa wakitoa Taarifa rasmi za Serikali kuhusu yaliyojitokeza pamoja na ufafanuzi wa kina wa Viongozi wa Taasisi zinazohusika na usimamizi wa Uchaguzi { yaani tume }.

No comments: