Wednesday, March 23, 2016

WAZIRI WA MALIASILI PROF. JUMANNE MAGHEMBE AONANA NA BALOZI WA MAREKANI HAPA NCHINI MHE. MARK CHILDRESS KUJADILI MAENDELEO YA SEKTA YA MALIASILI NCHINI

Waziri wa Maliasili Prof. Jumanne Maghembe (kushoto) akizungumza katika kikao na Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Mark Childress (kulia) na Ujumbe wake katika ukumbi wa Selous Makao Makuu ya Wizara hiyo Mpingo House leo tarehe 23 Machi, 2016. Waziri Maghembe amemuomba Balozi huyo wa Marekani kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kukuza sekta ya utalii nchini kwa kuwakaribisha wawekezaji kutoka Marekani kuwekeza katika sekta hiyo.
Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Mark Childress (kulia) akizungumza na Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe (kushoto). Balozi huyo wa Marekani ameahidi kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya Tanzania na Marekani katika kuendeleza sekta ya uhifadhi hapa nchini. Ameahidi pia kusaidia katika vita dhidi ya ujangili.
Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe (kushoto) akisisitiza jambo kwa  Balozi wa Marekani hapa nchini Mhe. Mark Childress (wa pili kushoto). Mhe. Maghembe alimueleza balozi huyo kuwa Tanzania haiko tayari kuteketeza meno ya Tembo yaliyohifadhiwa mpaka hapo itakapoona namna bora zaidi ya kufanya kwani kwa sasa Meno hayo yanaweza kutumika kwa ajili ya tafiti mbalimbali za kisayansi na kusaidia pia katika utambuzi na vielelezo vya mashtaka ya ujangili. Mhe Maghembe alisema hayo baada ya Balozi Childress kutoa pendekezo kwa Serikali kuona uwezekano wa kuteketeza sehemu ya meno ya Tembo yaliyohifadhiwa ili kutoa ujumbe duniani wa namna Serikali ya Tanzania ilivyodhamiria katika vita dhidi ya Ujangili.
Sehemu ya wajumbe kutoka ubalozi wa Marekani walioongozana na Mhe. Balozi Mark Childress wakifuatilia mada katika kikao hicho. Wajumbe hawa kila mmoja aliwasilisha mada ikionyesha ushirikiano wa Serikali ya Marekani na Tanzania katika sekta ya uhifadhi hapa nchini.  
Baadhi ya wajumbe kutoka ubalozi wa Marekani na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kikao hicho.
Wajumbe kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii walioshiriki katika kikao hicho. Kulia ni Naibu Katibu Mkuu Bi. Angelina Madete.
(Picha na Hamza Temba - Wizara ya Maliasili na Utalii)

No comments: