Thursday, March 3, 2016

SHULE DIRECT YASHIRIKI KILI MARATHON KUSAIDIA WANAFUNZI WASIOSIKIA (VIZIWI) KUJIFUNZA

Mgeni Rasmi Afisa Elimu Manispaa ya Moshi, Bw. Deo Tulo Fundi (pichani kulia) akifafanua jambo wakati wa hafla fupi ya kukabidhi kompyuta zenye matini ya masomo tisa ya Sekondari (kidato cha kwanza – sita), kompyuta hizo zilitolewa na Shule Direct kwa ajili ya kusaidia wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia katika Shule ya Ufundi Sekondari Moshi. (Kushoto ni Bw. Erasmus Kyara, Mkuu wa Shule ya Ufundi Moshi).
Afisa Elimu wa Elimu ya Mahitaji Maalum Manispaa ya Moshi akitoa neno wakati akishuhudia tukio la makabidhiano ya kompyuta zenye matini za kujifunzia zilizotolewa na Shule Direct kwa ajili ya wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia katika Shule ya Ufundi Sekondari Moshi.
Baadhi ya wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia katika Shule ya Ufundi Sekondari Moshi na mwalimu wao Mwl. Raphael Lukumai (aliyekaa kulia) wakifurahia pamoja na baadhi ua wageni waliofika shuleni kwao kukabidhi kompyuta zenye masomo tisa ya Sekondari ndani yake.
Baadhi ya wanafunzi wa shule ya ufundi sekondari Moshi wakielekezana jambo katika mojawapo ya kompyuta walizokabidhiwa na Shule Direct, shuleni kwao,
Aneth Gerana, mtanzania wa kwanza mwenye ulemavu wa kusikia kupata shahada ya Chuo Kikuu, ambaye pia alijitokeza kuunga mkono jitihada za Shule Direct, akiongea na baadhi ya wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia katika shule ya ufundi sekondari Moshi wakati wa hafla fupi ya kukabidhi kompyuta shuleni hapo.
Aneth Gerana na baadhi ya wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia kutoka shule ya ufundi sekondari Moshi, wakifurahia kompyuta zilizotolewa na Shule Direct ili kuwasaidia wanafunzi hao kujifunza kwa urahisi zaidi.
Faraja Nyalandu, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mkuu wa Shule Direct na Aneth Gerana wakikimbia mbio za kilometa 21.1 wakati wa mbio za Kili Marathon. Shule Direct walishiriki mbio hizo kwa ajili ya kuchangisha fedha kuwezesha upatikanaji wa kompyuta zenye matini ya masomo tisa ya Sekondari kwa ajili ya kusaidia wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia katika shule za Ufundi Sekondari Moshi na Njombe Sekondari ya viziwi.
Wakiwa wenye nyuso za furaha, Faraja Nyalandu, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mkuu wa Shule Direct, Aneth Gerana na wengine kutoka Shule Direct na marafiki wa Shule Direct mara baada ya kumalizi mbio za kilometa 21.1 wakati wa Kili Marathon.

Namna bora ya kufundisha wanafunzi wenye ulemavu ni kuwafundisha wakiwa wamechanganyika darasa moja na wanafunzi wasio na ulemavu. Hii inamaanisha kwamba kwa wanafunzi wasiosikia ni muhimu walimu watakaofundisha hilo darasa wawe ni wataalamu wa lugha ya ishara ili waweze kufundisha kwa matamshi na ishara ili kukidhi mahitaji ya wote. Hii ni ngumu kwasababu si walimu wengi wenye utaalamu wa lugha ya ishara. Matokeo yake wale wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia wanaachwa nyuma bila kuelewa na hatimaye kufeli masomo yao.

Shule Direct ilitambua umuhimu wa kutafuta mifumo mingine ya kuwasaidia wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia, kuweza kujifunza. Masomo yakiwa ndani ya Kompyuta ni rahisi kwa mwanafunzi huyo kusoma na kujifunza katika kasi yake na kulingana na uelewa wake.
Hivyo, Shule Direct ikaazimia kushiriki mbio za Kili Marathon 2016 ili kuchangisha fedha kwa ajili ya Shule ya Sekondari ya Moshi Technical na Njombe Shule ya Sekondari ya Viziwi (Shule pekee ya Sekondari ya viziwi Tanzania). Fedha hizo ni kwa ajili ya kuwapatia ‘Content Lab’ kila shule. ‘Content Lab’ inakuwa na kompyuta 20, masomo tisa ya Shule Direct yaliyotengenezwa kwa mujibu wa ‘Syllabus’ ya Tanzania yanayowekwa moja kwa moja kwenye kompyuta hizo kurahisisha upatikana ji bila ‘internet’ na kamusi ya lugha ya ishara ya signwiki.

Tarehe 27 Februari 2016, Mgeni rasmi, Afisa Elimu wa Manispaa ya Moshi Bw. Deo Tulo Fundi akiwa na Afisa Elimu wa Elimu ya Mahitaji maalumu wa Manispaa ya Moshi, Bi. Joyce Sawuo walishuhudia awamu ya kwanza ya utoaji wa vifaa hivyo katika Shule ya Sekondari ya Moshi Tech.

Kabla ya makabidhiano hayo, timu ya ufundi ya Shule Direct iliweza kutoa mafunzo ya namna ya kutumia nyenzo hizo kwa walimu na wanafunzi wa Moshi Technical, hususan wale walimu wanaosimamia wanafunzi wenye ulemavu. 

Wakitoa shukrani zao za dhati wakiongozwa na Mwalimu Mkuu wa Moshi Tech Mwl. Erasmus Kyara na Mwalimu msimamizi wa anayesimamia mafunzo ya wanafunzi wenye ulemavu walielezea furaha yao kupata kompyuta hizo zenye nyenzo za kujifunzia, walisema kwa kipindi kirefu sasa wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia wamekuwa wakiwasindikiza tu wenzao kwa maana matokeo yao huwa hayavuki daraja la nne, wanakumbuka kwa jina, mwanafunzi mmoja tu mwenye ulemavu wa kusikia aliyewahi kupata daraja la tatu katika shule hiyo. 

Akiongea kwa niaba ya wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia shuleni hapo, mwanafunzi wa kidato cha nne, Raphael, alielezea furaha yake kuwa wanafunzi wenye tatizo kama lake wameweza kupatiwa msaada wa kompyuta zenye masomo zitakazowawezesha kujisomea na kuelewa masomo yao zaidi, alishukuru sana kupata nafasi ya kupata mafunzo ya vitendo ya jinsi kutumia kompyuta hizo, zaidi alishukuru kwa fursa ya pekee ya kukutanishwa na mwanadada Aneth Gerana ambaye aliongozana na timu ya Shule Direct. Aneth ni mtanzania wa kwanza mwenye ulemavu wa kusikia aliyefanikiwa kupata shahada ya Chuo Kikuu Cha Dar Es Salaam, naye ni miongoni mwa wadau waliojitokeza kujiunga na Shule Direct katika zoezi hili kwa kuwashirikisha wanafunzi maisha yake na kuwaasa kuwa wafanye bidii katika masomo yao ili waweze kufaulu katika maisha.

Zoezi la kusaidia wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia la Shule Direct lililopatiwa jina la #KiliShuleThon 2016 lilifanikishwa kwa kiasi kikubwa sana na mchango wa wadau mbali mbali wa elimu na maendeleo waliojitokeza kuchangia, pia zoezi hili liliwezeshwa kwa mchango mkubwa na ushirikiano na waandaaji wa Kili Marathon, Benki ya NMB, Freedom Computers Limited na Lensmark Studios.

No comments: