Sunday, March 6, 2016

Serikali ipo kwenye hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa Barabara ya Tanga,Pangani

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akionyeshwa eneo la uwanja wa ndege itakakopita barabara ya Mchepuko itakayotoka Horohoro kuunga na inayokwenda Pangani kupitia Utofu, Majani Mapana hadi Duga.

SERIKALI ipo kwenye hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa Barabara ya Tanga,Pangani ,Saadani mpaka Bagamoyo yenye urefu wa kilometa 242 kwa kiwango cha lami ambapo mpaka sasa tayari kazi  iliyobaki ni kupata mzabuni wa kuendesha mradi huo.

Waziri wa ujenzi,uchukuzi na Mawasiliano Prof.Makame Mbarawa alisema kuwa ujenzi  wa Barabara hiyo utaanza rasmi kutekelezwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 na kwamba serikali ipo kwenye mazungumzo na Benki ya Maendeleo ya Afrika(ADB)ambayo imeonesha nia ya kufadhili mradi huo.

Mradi huo utaenda sambamba na ujenzi wa Daraja katika  Mto Pangani lenye urefu wa mita 550 ambalo linategemewa kuwa kiunganishi cha mawasiliano ya kuimarisha shughuli za utalii katika ukanda wa Pwani ya Bahari ya Hindi.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akipima eneo la barabara inayohitajika katika eneo la hifadhi ya uwanja wa ndege wa Tanga.

Kwa mujibu wa Prof.Mbarawa ni kwamba wakati wa utekelezaji wa mchakato huo serikali itawalipa fidia wananchi ambao wanastahili na wameshafanyiwa tathimini kwa mujibu wa sheria ya Barabara ya mwaka 2007 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2009.

“Nasisitiza kwamba kama sheria inavyotamka kwamba nani anastahili kulipwa basai kila mwenye haki na anayestahili kulipwa atalipwa na kama hastahili hatalipwa na hii itakuwa ni kulingana na tathmini iliyokwishafanyika......”,alisema Waziri huyo.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akitazama ramani ya gati ya Bandari ya pangani ambayo inajengwa kwa gharama ya sh. bilioni 2.3.

Alisema kuwa serikali inatambua umuhimu wa ujenzi wa Barabara hiyo kwamba ndiyo kiini na moyo wa uchumi wa wilaya ya Pangani hasa kwa kutambua namna ambavyo ina vivutio vingi vya kitalii hatua itakayolenga kuwaongezea fursa za kibiashara wananchi na kukuza Pato lao.

“Daraja hili litakuwa na uwezo wa kupitisha magari na watembea kwa miguu kwa wakati mmoja na hivyo ni mkombozi wa wananchi hasa kwa kuzingatia kuwa walikuwa wakitegemea kuvuka ng’ambo ya pili ya mto kwa kutumia kivuko tu ambacho wakati mwingine kinakumbwa na hitilafu”,alifafanua Prof.Mbarawa ambaye yupo mkoani Tanga katika ziara ya kikazi.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akitazama ramani ya daraja la Mto Pangani ambalo upembuzi yakinifu wa ujenzi wake umekamilika na litaanza kujengwa hivi karibuni.

Akizungumza wakati wa majumuisho ya ziara yake baada ya kukagua Kivuko cha Mto Pangani,Barabara ya Tanga,Saadani mpaka Bagamoyo na eneo linalotakiwa kujengwa Daraja,Prof.Mbarawa  aliuagiza Uongozi wa Wakala wa ufundi na Umeme(Temesa)kuhakikisha wanaweka kumbukumbu za utendaji wa kivuko kwa kila siku.

Aliwaagiza kutumia mfumo wa malipo kwa njia ya elektroniki ili kuepusha vitendo vya ubadhirifu wa fedha wakati serikali ikiwa kwenye mpango wa ukusanyaji wa fedha kwa ajili ya maendeleo ya wananchi.

“Suala la kutumia mashine za kieletroniki halina mjadala habari ya kutumia vitabu vya risiti ili muongeze sifuri mbele hatuzitaki....hapa kuna shida kuna siku I naandikwa imeingia shilingi milioni moja lakini Benki zimeenda laki nane na hamsini hii laki moja na hamsini zinaishia wapi hili ni tatizo”,alisema.

Hata hivyo alisema ipo haja kwa Temesa kuajiri manahodha wa vivuko ambao wanafanya kazi kwa viwango vya kitaaluma ambavyo vinakubalika badala ya kutumia Wazee ambao wanafanya kazi kwa mazoea.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawaakitoa maelekezo kwa meneja wa Tanroads Mkoa wa Tanga, Alfred Ndumbaro kuhusu ujenzi wa barabara ya mchepuko.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa akifafanua jambo katika makutano ya barabara ya mchepuko eneo la Duga.
Muonekano wa gati inayojengwa katika bandari ya Pangani iliyogharimu kiasi cha sh. bilioni 2.3.

No comments: