Sunday, March 13, 2016

MTAMBO WA KUSUKUMA MAJI KUTOKA RUVU CHINI KWENDA JIJINI DAR ES SALAAM WAWASHWA KWA MAJARIBIO

Mkuu wa Matengenezo wa Mtambo wa kuzalisha maji wa Ruvu Chini Tumaini Ndosi (aliyepanda juu) akitoa ufafanuzi kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Muhandisi Mbogo Futakamba kuhusu moja ya mita inayosoma kiwango cha ujazo wa maji yanayosafirishwa kutoka kwenye Pampu za kusukumia maji.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Muhandisi Mbogo Futakamba (kulia) akizungumza jambo na Meneja wa Mtambo wa kuzalisha maji wa Ruvu Chini, Emmanuel Makusa (kushoto) na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASCO Muhandisi Cyprian Luhemeja mara baada ya kukagua mitambo na pampu za kusukumia Maji za Mtambo wa Ruvu Chini, Bagamoyo mkoani Pwani.
Eneo la ndani la Mtambo wa kuzalisha maji likiwa limekamilika mara baada ya kufungwa pampu mpya zenye uwezo wa kusukuma maji Lita milioni 270 kwa siku kuja jijini Dar es salaam na maeneo ya Mkoa wa Pwani.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Muhandisi Mbogo Futakamba (katikati) akieleza namna wakazi wa jiji la Dar es salaam na mkoa wa Pwani watakavyonufaika na huduma ya Maji mara baada kukamilika kwa ujenzi wa bomba la kusafirishia Maji kutoka mtambo wa Ruvu Chini kuja jijini Dar es salaam. Kushoto ni Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) Muhandisi Archard Mutalemwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASCO Muhandisi Cyprian Luhemeja.
Sehemu ya maungio ya Mabomba yanayoingiza maji ndani ya Mtambo huo kutoka mto Ruvu, chini.
Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASCO) Muhandisi Cyprian Luhemeja akitoa ufafanuzi kwa waandishi namna DAWASCO ilivyojipanga kuwahudumia wananchi wa mkoa wa Dar es salaam kwa kuwafikishia huduma ya Maji Safi kufuatia kukamilika ujenzi wa bomba la Maji kutoka Mtambo wa Ruvu Chini, Bagamoyo mkoani Pwani.
Moja ya maungio ya Bomba kubwa la kusafirishia Maji kutoka mtambo wa Maji wa Maji wa Ruvu Chini, Bagamoyo Pwani lililoko eneo la Tegeta jijini Dar es salaam likiwa limekamilika.
Sehemu ya ndani ya Matenki yanayopokea maji kutoka mtambo wa Ruvu Chini yaliyoko eneo la Chuo Kikuu cha Ardhi jijini Dar es salaam. Picha na Aron Msigwa –MAELEZO.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Muhandisi Mbogo Futakamba akibonyeza moja ya mashine inayoongoza pampu za kusukuma Maji kwenda jijini Dar es salaam kutoka Mtambo wa kuzalisha Maji wa Ruvu Chini wilayani Bagamoyo mkoani Pwani ikiwa ni sehemu ya majaribio ya mtambo huo mara baada kukamilika kwa ujenzi wa bomba la kusafirisha maji lenye urefu wa kilometa 55.9.

Na. Aron Msigwa – MAELEZO.

Hatimaye moja ya Pampu kubwa katika mtambo wa kuzalisha Maji kwenye chanzo cha maji cha Ruvu Chini, Bagamoyo mkoani Pwani imewashwa kwa majaribio kufuatia kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa bomba kubwa la kusafirishia maji lenye urefu wa kilometa 55.9 kutoka chanzo hicho kwenda jijini Dar es salaam.

Majaribio hayo ni sehemu ya awali ya kupitisha maji yenye msukumo mkubwa kwenye bomba hilo kuelekea kwenye matenki makubwa ya kuhifadhia maji yaliyoko eneo la Chuo Kikuu Ardhi jijini Dar es salaam.

Akizungumza mara baada ya kuwasha Pampu hiyo Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Umwagiliaji Muhandisi Mbogo Futakamaba amesema kuwa majaribio hayo ambayo yameonyesha mafanikio yatawawezesha wakazi wa jiji hilo na maeneo ya mkoa wa Pwani kupata huduma ya uhakika ya Maji kufikia mwishoni mwa mwezi Machi mwaka huu.

Amesema mradi huo utakuwa suluhisho la tatizo la maji la muda mrefu kwa kuwa kiwango cha maji kitakachozalishwa kwa siku kitafikia lita milioni 270 ambazo zitaongezwa kwenye msukumo wa lita milioni 182 zilizokuwa zikizalishwa hapo awali kabla ya kukamilika kwa ujenzi wa bomba hilo.

“Hii ni faraja kwa Serikali na wakazi wa jiji la Dar es salaam na mkoa wa Pwani, sasa tutapata lita Zaidi ya milioni 270 kwa siku haya ni mafanikio makubwa, kulingana na mahitaji tuliyokuwa nayo tutahakikisha tunayasambaza maji haya ili kukidhi mahitaji ya wananchi” Amesema Muhandisi Futakamba.

Muhandis Futakamba amewataka wahandisi na watendaji wanaosimamia uendeshaji wa mitambo hiyo kuwa mahili na makini katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuhakikisha inafanya kazi kwa ufanisi na kwa maslahi ya umma.

Ameiagiza DAWASA na DAWASCO kuendelea kuwajengea uwezo kielimu Wahandisi wa ndani wanaohusika na utunzaji wa miundombinu hiyo ili miradi ya maji wanayoisimamia iweze kudumu na kuwa endelevu kupitia matengenezo na huduma mbalimbali watakazozifanya.

“Ninyi kama wahandisi na wasimamizi wa miradi na mitambo hii mikubwa hakikisheni mnajenga uwezo wenu wa ndani ili muweze kuiendesha na kuidhibiti mitambo hii pia kuwa na uelewa wa ndani wa mifumo yote iliyotumiwa wakati wa uwekaji wake na mabadiliko ya teknolojia” Amesisitiza.

Pia amewataka watendaji hao kuhakikisha kuwa wanatunza mitambo na miundombinu yote ya maji ili iweze kudumu kwa muda mrefu na kuendelea kuwanufaisha wananchi wengi zaidi.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA) Muhandisi Archard Mutalemwa akizungumza mara baada ya kukagua mitambo ya kuzalisha Maji ya Ruvu Chini amesema kuwa kukamilika kwa bomba hilo ni mwendelezo wa juhudi za Serikali kupitia DAWASA za kuhakikisha wananchi wanafikiwa na huduma ya maji Safi.

Amesema DAWASA itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kuhakikisha inaendeleza na kusimamia miradi ya maji ikishirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo na kuhakikisha inawawezesha wakazi wa jiji la Dar es salaam na maeneo ya mkoa wa Pwani yanapata huduma ya Maji Safi kupitia miradi iliyo chini yake.

Naye Afisa Mtendaji Mkuu wa Shirika la Maji Safi na Maji Taka Dar es salaam (DAWASCO) Muhandisi Cyprian Luhemeja akizungumza mara baada ya kuwashwa kwa mtambo huo amesema kuwa DAWASCO imejipanga kuhakikisha inawasambazia huduma ya maji wakazi wengi zaidi wa jiji hilo ambao walikua na miundombinu lakini hawapati huduma hiyo pamoja na kuunganisha wateja wapya kwa gharama nafuu.

“Naishukuru Serikali kwa kuwezesha mafanikio haya sisi kama DAWASCO tumejipanga na tutahakikisha maji yanayozalishwa yanawafikia wananchi, yapo maeneo mengi yaliyokuwa na changamoto ya huduma hiyo hata yale ambayo yalikua yameunganishwa tayari katikati ya jiji nay ale yaliyo pembezoni mwa jiji tutahakikisha tutayafikia” Amesisitiza.

Akizungumzia hatua zinazochukuliwa kudhibiti wa wizi wa maji amesema DAWASCO imeanzisha maeneo 25 (DMA) ambayo yamefungwa mita kubwa katika wilaya za jiji hilo ili kuwawezesha Mameneja wa Zoni husika kuweza kubaini wizi , upotevu wa maji, ubovu wa mita na tatizo la usomaji na kisha kuchukua hatua kwa wale wanaobainika kuhujumu miundombinu hiyo.

Aidha, amesema DAWASCO imeandaa mpango wa kuziondoa mita zote ambazo zimefikia umri wa miaka 10 ifikapo mwezi Juni mwaka huu.

Ikumbukwe kuwa mradi wa ujenzi wa bomba kubwa la kusafirishia maji kutoka mtambo wa Ruvu Chini wenye urefu wa kilometa 55.9 umejengwa na Kampuni ya JBG Gauff Ingenieure kwa gharama ya shilingi Bilioni 141 ambazo zote zimetolewa na Serikali ya Tanzania.

No comments: