Tuesday, November 17, 2015

TANZANIA YATAKA MASHIRIKA YA UMOJA WA MATAIFA KUTEKELEZA KWA VITENDO DHANA YA UWAZI NA UWAJIBIKAJI

Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi ( picha ya Maktaba) ametoa wito kwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Ofisi zake kutekeleza kwa vitendo dhana ya uwazi na uwajibikani kama yanavyozishikiza Nchi Wanachama, kwa kile alichosema, utekelezaji wa dhana hiyo haupashwi kuwa jukumu la Serikali peke yake. Ametoa wito huo wakati wa majadiliano ya Ripoti ya Baraza la Haki za Binadamu iliyowasilishwa siku ya jumatatu mbele ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Na Mwandishi Maalum,  New York

Jamhuri ya Muungano wa  Tanzania,  imetoa wito kwa Mashirika ya   Umoja wa Mataifa, ikiwamo Baraza la  Haki za Binadamu    kuitekeleza kwa vitendo dhana ya uwazi na uwajibikaji.

Tanzania imesisitiza  pia   kwamba,   haitoshi kwa  Mashirika hayo  kuzitaka   nchi wanachama kwa maana ya serikali kuwajibika na kuwa wazi  katika utekelezaji wa majukumu  yake ili hali yenyewe yanafanya kinyume.

Wito huo umetolewa siku ya  Jumatatu na Mwakilishi wa  Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, Balozi Tuvako Manongi,  wakati  Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa,  lilipopokea na kujadili Ripoti   ya Mwaka ya  Baraza la  Haki za  Binadamu ya   Umoja wa Mataifa.

Balozi Manongi ambaye alikuwa  miongoni mwa Mabalozi kati ya wengi waliochangia Ripoti hiyo  iliyowasilishwa na   Rais wa  Baraza la   Haki za Binadamu  Bw.Joachim Rucker .Amesema,  Tanzania  inatoa wito   huo   kutoka kile kinachoonekana  dhahiri   kwamba ama Mashirika hayo  yamekuwa yakionyesha  kuegemea  upande mmoja  dhidi ya mwingine   au  kupendelea  nchi  moja dhidi ya  nyingine  kitendo  ambacho kinakwenda kinyume  na kile  wanachokihubiri.

Akatoa mfano kwa kusema,  wakati Rais wa Baraza la   Haki za Binadamu akisisitiza katika ripoti yake umuhimu wa uwajibikaji, Ofisi ya  Haki za Binadamu  katika mwezi Octoba   ikishirikiana na  UNICEF na  Canada,  ilidhamini onyesho la Filamu kuhusu  kijana kutoka Geita mwenye alibinisim,  pasipo  Taasisi hiyo  kuujulisha Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania ili hali wakijua Tanzania ilikuwa mlengwa wa filamu hiyo.

  “ Akiwasilisha  Taarifa yake mbele ya Baraza hili  mwanzoni mwa  mkutao huu, Raisi wa Baraza la   Haki za Binadamu amesisitiza umuhimu wa  uwazi na uwajibikaji. Cha  kusikitisha  tukio la konyeshwa kwa filamu  ambayo maudhui yake yalihusu Tanzania na sisi kama Tanzania hatukujulishwa, hakika inakwenda kinyume kabisha na dhana  ambayo Rais wa Baraza la   Haki za Binadamu amekizungumza hapa” akasema Balozi Manongi.

Na kuongeza “ ndiyo maana Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatoa wito kwa  Mashirika ya Umoja wa Mataifa au Ofisi zake kuonyesha kwa  vitendo  dhana ya  uwazi,   uwajibikaji na kutoegemea upande wowote”.

Akabainisha kuwa,  Mashirika ya Umoja wa Mataifa hayapashwi   kujionyesha kuwa yanaegemea upande wowote au hata kupendelea  baadhi ya   nchi  wanachama dhidi  nchi nyingine na hasa  pale ambapo Mashirika hayo  binafsi hayajapitia na kujiridhisha juu ya kile ambacho wanataka kukiunga mkono  au  kutaka kujihusisha nacho.

Akaeleza Zaidi  mbele  ya wajumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwamba,  Tanzania  haikupinga na wala haipingi filamu kuhusu kijana wa   Geita,  filamu iliyolenga katika kuonyesha changamoto  zinazowakabili watu wenye ualibino nchini Tanzania.

“ Tulichopinga na tunachopina  ni maelezo yaliyoandikwa na  muandaaji wa  filamu hiyo,  maelezo ambayo yalikuwa  na upotoshaji mkubwa. Kwa mfano,  baadhi ya  maelezo  ya filamu hiyo  yanasema,   hakuna utashi wa kisiasa kutoka Serikali   ya Tanzania  katika kukabili uovu wanaotendewa watu  wenye ualibino. 

Kwamba, msukumo kutoa mataifa ya nje ni wa lazima ili kutokomeza uovu huo,  kwamba ujinga  ni laana kubwa  inayowakabili  waaafrika na  jawabu pekee ni kuwaelimisha, kwamba filamu hiyo ilikuwa ni kuwashawishi watu wa nje ili kuleta mabadiliko ya kweli. Na  vilevile filamu  hiyo ilikuwa ni  kusherehekea  roho ya  utu na kazi nzuri inayofanywa na watu wa Canada katika kuwasaidia watu wenye ualibino” akasisitiza  Balozi Manongi.

 Akasema Baloz, Ni kwa  kuzingatia upotoshaji huo na mwingine ulioelezwa na  muandaaji wa filamu hiyo, haishangazi kuona kwamba  Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania  haukualikwa kufadhili onyesho la filamu hiyo iliyoonyeshwa  Umoja wa Mataifa.

“ Rais wa Baraza la  Haki za  Binadamu pia amezungumzia wajibu wa  Asasi za Kijamii katika   uhamasishaji wa haki za Binadamu.  Tunakubaliana na  pendekezo wake.  Wakati tunauga mkono  mchango wa Asasi za kijamii, ni lazima basi Asasi hizo nazo zikaonyesha uwajibikaji na uwazi  pamoja na kujipambanua  katika utekelezaji wa majukumu yao. Uwajibikaji hauwezi kuwa ni jukumu la serikali peke yake” akasisitiza Balozi Manongi.

Akizungumzia Zaidi kuhusu changamoto zinazowakabili watu wenye  ualibino, Mwakilishi huyo wa Tanzania, amesema,  Tanzania  kwa kutambua changamoto kubwa za kijamii na kiuchumi pamoja na    upatikanaji wa haki za msingi kwa watu wenye ualibino ndiyo maana  kwa kushirikiana na  Malawi   imeamua kuwasilisha mbele ya Kamati ya Tatu ya Baraza Kuu la   Umoja wa Mataifa Azimio kuhusu watu  wenye ualibino.

Amesema  dhumuni kuu la Azimio hilo na ambalo linatarajiwa kupitishwa wiki hii ni  kupanua wigo na   ushiriki mpana wa   wadau mbalimbali  ukiwamo  Umoja wa Mataifa katika  kuzikabili  changamaoto zinazowakabili watu wenye ualibino.

 Na kwa sababu hiyo, Balozi  Manongi ameziomba nchi   wanachama  wa Umoja wa Mataifa,  kuunga mkono   azimio  hilo pamoja na  jitihada zinazofanywa na Serikali ya Tanzania pamoja  na  Chama cha Watu wenye Ualibino Tanzania (TAS) katika  kuzitafutia  ufumbuzi   changamoto  zinazowakabili  watu wenye ualibino vikiwamo vitendo vya kikali wanavyofanyiwa na watu wasio na  mapenzi mema.

No comments: