Friday, March 20, 2015

Waziri Prof. Mghembe awaonya wanaoharibu vyanzo vya maji

Mchungaji wa mifugo akinywesha maji mifugo yake kwenye eneo lenye maji ambalo Waizri Prof. Maghembe amepiga marufuku kunywesha kwenye eneo hilo.

Na Hussein Makame-MAELEZO, Musoma

WAZIRI wa Maji Profesa Jumanne Maghembe amewaonya wananchi wanaoharibu vyanzo vya maji kwamba kufanya hivyo kunahatarisha uhai wa vyanzo hivyo.

Ametoa onyo hilo kwa nyakati tofauti wakati akiwa kwenye shughuli za kuweka mawe ya msingi kwenye miradi ya maji kwenye maeneo mbalimbali ya wilaya ya Serengeti mkoani Mara ambako Maadhimisho ya Wiki ya Maji kitaifa yanafanyika. 

 Akiwa katika kijiji cha Rung’abure, Waziri alishuhudia baadhi ya wafugaji wakinywesha mifugo yao kwenye maeneo ya vyanzo vya maji huku baadhi wakilima karibu na chanzo cha maji.

“Jamani mradi huu ni wa kwenu, lakini nilichokiona pale kwenye chanzo cha maji, nilina ng’ombe kwenye eneo chepechepe” alisema Waziri Prof. Maghembe na kungeza: “Jamani fanyeni juhudi au lolote mnalofanya lakini msiingizi ngombe mule kama mkiingiza basi maisha ya mradi yatakuwa mafupi na hakuna mtu wa kumlaumu kwa sababu ni nyinyi wenyewe mmekuwa kama mtu anayekata tawi la mti alilokalia” Aliongeza kuwa katika eneo la mradi wa Rung’abure kuna mkulima analima kwenye msitu ulioko karibu na chanzo cha maji cha mradi wa kijiji hicho, hivyo anahatarisha chanzo hicho.

“Mtu yule tunamuomba mwaka huu avune mazao yake lakini mwaka kesho asipande pale.Mwenyekiti naomba mumpe shamba lingine kwa sababi akiendelea kulima hakuna maji pale” alisema Waziri Prof. Maghembe.

Alifafanua kuwa suala la kuondoka si hiyari kwani hairuhusiwi kisheria kulima mita 60 kutoka chanzo cha maji, hivyo mkulima huyo ni lazima aondoke mwakani.

“Hili jambo ninalosema si hiari ni suala la kisheria hairuhusiwa kulima kwenye chanzo cha maji kwa umbali wa mita 60 na hilo sio jambo la kumuomba mtu ni jambo la kutekeleza sheria” alisema na kuongeza: “Ninachosema yule aliyelima pale mwaka huu avune mazoa yake mi sina tatizo kabisa baada ya hapo tunamuoba aondoke pale sheria hii sio ya mwaka huu, wala mwaka jana wala mwaka juzi na hilo ni sheria imetungwa mwaka ya 2006” Aliitaka Serikali ya kijiji hicho pia wanasimamia kuhakikisha ng’ombe hawapelekwi kunywa maji kwenye eneo la chanzo cha maji badala yake wakanywe maji kwenye mabirika yaliyojengwa.

Akiwa mjini Mugumu wilayani Serengeti, ambako alitembelea ujenzi wa chujio la maji ya bwawa la Manchira na baada ya ukaguzi huo alizungumza na wananchi wa mji huo. Alisema chujio hilo litachuja maji na kuweka dawa kwenye maji yanayokwenda mjini na kutatua tatizo la uchafu wa maji ambalo linawakabili wananchi wa Mugumu.

“Lakini pia niwaombe sana ndugu zangu mtunze sana mazingira kwani tumeona rasilimali za maji zinapungua sana ninawaomba mtunze sana vyanzo vya maji mtunze na bwawa letu la Manchira” alisema Waziri Prof. Maghembe. Hivyo alisisitiza kuwa ili kuhakikisha bwawa hilo na linaendelea kutumika kwa kipindi kirefu, kitu kikubwa ni kutunza sana mazingira ili kiasi cha rasilimali kilichopo kisiendelee kupungua.

Akiwa katika vijiji vya Ligamba A na Mumagunga vilivyoko wilayani Bunda mkoani Mara, Waziri aliwataka wananchi wapande miti ili kulinda vyanzo vya maji kwenye maeneo yao. Alisema utunzaji wa vyanzo vya maji ni jambo muhimu ili kuhakikisha kuwa vyanzo vya maji havikauki na kujharibiwa kwani kufanya hivyo kutahatarisha upatiakanaji wa maji.

Waziri Prof. Maghembe anaendelea na ziara ya kukagua na kuweka mawe ya msingi kwenye miradi ya maji katika vijiji mbalimbali vya wilaya za mkoa wa Mara ikiwa ni sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Maji Kitaifa.

No comments: