Wednesday, January 21, 2015

Mchezaji Hamis Tambwe alia na TFF,ataka wanaoleta vurugu wachukuliwe hatua


Mshambuliaji Hamis Tambwe amelitaka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kuchukua hatua stahiki dhidi ya wachezaji wa Ruvu Shooting kwa kitendo cha kumshambulia na kumtolea lugha chafu uwanjani ikiwemo kumbagua kwa kumuita mkimbizi.


Akizungumza Makao Makuu ya klabu ya Yanga iliyopo mtaa wa Twiga na Jangwani leo, Tambwe alisema kuwa kitendo alichofanyiwa ni cha kinyama na anakilaani kwa nguvu zote, na anataka aelezwe wazi iwapo wachezaji kutoka mataifa mengine hawatakiwi kucheza Tanzania.

"Uwanja wa Taifa kuna kamera, matendo mengi sana mabaya tumekuwa tukifanyiwa wachezaji wa kigeni, naamini baada ya mchezo TFF wanakaa kupitia mikanda ya mchezo wanaona kila kitu lakini hakuna adhabu zinazochukuliwa tunavyodhalilishwa na kubaguliwa.

"Nimetukanwa, nimeitwa Mkimbizi, nipo nchini kihalali na nafanya kazi kwa kufuata sheria zote kwa nini waniite mkimbizi, nipo tayari kusema matusi waliyonitukana kwa mabosi wangu na kwa TFF ili hatua stahiki zichukuliwe, mpira sio vita, mpira ni burudani, mpira ni 'fair play', lakini hapa imekuwa ni tofauti.

"Kitendo walichonifanyia ni sawa na kunishikia bastola, ni unyama wa hali ya juu walitaka kuniua, yani wamenikaba nilikuwa naona roho yataka toka, hatukuwa vitani walitakiwa wacheze mpira wa 'profesional' hivi tutaogopa kucheza Tanzania."alisema kwa masikitiko.

"Hawakuja kucheza soka, walikuja kupigana, walinipiga kiwiko, wakanipiga ngumi na mwisho walinikaba shingoni nikaona pumzi zinataka niishia.


Hii ni hatari, kuna mtu anaweza kuanguka akapoteza maisha siku moja. Wale wanajeshi hawaingii uwanjani kucheza soka, wanakwenda kucheza na mwili wa wachezaji wenzao.


"Maneno makali waliyonitamkia yananiuma sana roho hadi sasa, wameniita mkimbizi, eti nimekimbia vita nyumbani Burundi, vita hata hapa inaweza kutokea, hakuna anayependa mabaya kama hayo yatokee, kumwambia mtu haujui kapoteza ndugu wangapi, si sahihi kabisa, cha kushangaza wale ni wanajeshi lakini hawaonyeshi kuwa wanajua athari za vita.

Naye Ofisa habari wa Yanga Jerry Muro akizungumzia suala hilo aliitaka TFF kuweka adharani ripoti ya kamisaa wa mchezo huo ulichezwa mwishoni mwa wiki iliyopita na kumalizika kwa sare na kuwachukulia hatua stahiki waamuzi, na kamisaa ikiwa ni pamoja na kocha wa Ruvu Shooting Tom Olaba hatua kali za kinidhamu huku wakiitadharisha TFF kutowapanga waamuzi hao katika mechi zao za Ligi zinazofuata ikiwemo ya kesho kutwa jumamosi dhidi ya Polisi Morogoro la sivyo watagoma kucheza ligi.

Katika mchezo huo uliomalizika kwa suluhu, Tambwe alichezewa rafu kadhaa na beki wa timu hiyo, George Michael, hadi akachanika mdomoni lakini mwamuzi hakuchukua hatua yoyote.

Ofisa habari wa TFF Boniface Wambura alipoulizwa kuhusiana na suala hilo kwanza alionyesha kushtushwa na taarifa za Tambwe kuitwa mkimbizi na kudai kuwa bado hawajapata malalamiko ya mchezaji huyo wala viongozi wa Yanga na iwapo watapata watafanyia kazi na kudai kuwa ripoti ya kamisaa haiwezi kuwekwa hadharani na kuwataka Yanga kuacha kujichanganya.

Katika hatua nyingine, Katibu wa Yanga Jonasi Tiboroha amedai kuwa Yanga ipo kwenye harakati za kujenga uwanja wa Jangwani kama ulivyo Azam Complex ambapo utakuwa na uwezo wa kuchukua watu 6,000.

Tiboroha alisema kuwa mkataba wao wa awali dhidi ya Kampuni ya kichina ya Beljing Construction Engineering ambao walikuwa wajenge uwanja wa watu 25,000 umekufa baada ya serikali kuwanyima eneo la nyongeza na sasa wanaelekeza nguvu kujenga uwanja wa mazoezi na kurekebisha Jengo lao ikiwa ni hosteli za wachezaji na ofisi za utawala.

No comments: