Wednesday, November 20, 2013

WATENDAJI WABOVU KUTIMULIWA TEMESA

Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuili (aliyeshika mkasi) akikata utepe kuashiria uzinduzi wa vifaa vipya vya karakana za TEMESA mikoani. Kushoto kwa Waziri ni Mwakilishi wa Mwenyekiti wa Bodi ya TEMESA Eng. Brig. Gen. Reginald Chonjo na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Eng. Marcelin Magessa. Kulia kwa Waziri Magufuli ni Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi Mhe. Eng. Gerson Lwenge, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi Alhaj Eng. Mussa Iyombe, Mkurugenzi wa Vivuko wa TEMESA Eng. Japhet Masele na Mkurugenzi wa Huduma za Ufundi na Umeme kutoka Wizara ya Ujenzi Eng. Dkt. William Nsahama.
Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuili (wa pili kushoto) akionyeshwa na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Eng. Marcelin Magessa (aliyeshika karatasi) baadhi ya vifaa vipya vilivyonunuliwa kwa ajili ya karakana za TEMESA mikoani.
Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuili (mbele) akionyeshwa na Mtendaji Mkuu wa TEMESA Eng. Marcelin Magessa (aliyeshika kipaza sauti) baadhi ya vifaa vipya vilivyonunuliwa kwa ajili ya karakana za TEMESA mikoani.
Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pombe Magufuili akisalimiana na baadhi ya Mameneja wa TEMESA mara baada ya kuongea nao wakati wa hafla ya kukabidhi vifaa vipya vilivyonunuliwa kwa ajili ya karakana za TEMESA mikoani.
Sehemu ya Mameneja wa TEMESA kutoka mikoa mbali mbali hapa nchini wakati wa hafla ya kukabidhiwa vifaa vipya kwa ajili ya karakara za TEMESA mikoani.

Waziri wa Ujenzi Mhe. Dkt. John Pembe Magufuli amewataka Mameneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme Tanzania (TEMESA) walioko mikoani na katika karakana kuu za hapa Dar es Salaam za MT Depot na Vingunguti, kwamba ni budi wawe wabunifu na wajitume wakati wakitekeleza majukumu waliyokabidhiwa vinginevyo wizara yake haitasita kuwaondoa mara moja kuanzia sasa.

Waziri Magufuli aliyasema hayo wakati akikabidhi vifaa vipya kwa ajili ya karakana za TEMESA zilizoko mikoani. Vifaa hivyo vyenye thamani  ya Shilingi milioni 823.5 vimetolewa katika awamu mbili ambapo awamu ya kwanza ilijumuisha mikoa ya Geita, Katavi, Iringa, Kilimanjaro, Tanga, Shinyanga, Kigoma, Rukwa na Pwani.

Awamu hii ya pili imejumuisha vifaa kwa ajili ya kazi za gereji za magari na mitambo, shughuli za ufundi wa umeme, elektroniki na viyoyozi. Vifaa hivyo  vilivyokabidhiwa ni kwa ajili ya mikoa ya Tabora, Simuyu, Dodoma, Mbeya, Arusha, Morogoro, Mara, Mtwara na vituo vya MT Depot na Vingunguti  vya hapa jijini Dar es Salaam.

Akizungumza na Mameneja hao katika ofisi za TEMESA zilizoko Chang’ombe jijini Dar es Salaam, Mhe. Magufuli alihoji kwamba “inashangaza kuona magari yanatoka hapa Dar es Salaam na kupelekwa katika karakana ya TEMESA ya Kibaha mkoani Pwani kwa ajili ya matengenezo, kwani hapa Dar es Salaam kumetokea nini au mmebaki kuwa mawakala wa gereji binafsi tu?”.

Akifafanua zaidi Waziri huyo alibainisha kuwa zipo baadhi ya gereji ambazo hazina hadhi kabisa ya kutoa huduma hiyo lakini utakuta magari ya Serikali yako huko na hata malipo yake hufanyika haraka haraka wakati yale ya TEMESA hayalipwi na hakuna ufuatiliaji.

Aidha, katika hatua nyingine Waziri wa Ujenzi alimpongeza Kaimu Meneja wa Karakana ya TEMESA ya Bukoba mkoani Kagera kwa ubunifu na utendaji wake mzuri kiasi cha kuvutia hata sekta binafsi kufanyia matenegezo magari yao katika karakana hizo za Serikali. “Mtendaji kama huyu anatakiwa kupewa kituo kamili” alielekeza Dkt. Magufuli na kumtaka Mtendaji Mkuu wa TEMESA kutosita kumuondoa mtendaji yeyote anayeshindwa kutekeleza majukumu yake inavyostahili.

“Ikibidi tutakuwa tunawapangia vituo watendaji wazuri kama huyu wa Kagera hata kama hawana digrii ili hawa wasomi waliopo ambao wameshindwakazi wajifunze kutoka kwa hao wenye ubunifu” alimalizia Waziri Magufuli na kusema kuwa maana ya kuwa na elimu ya juu ni kuonyesha ufanisi.

Naye Mjumbe wa Bodi ya TEMESA Injinia Brig Gen. Reginald Chonjo ambaye alimwakilisha Mwenyekiti wa Bodi hiyo alisema kuwa pamoja na kutolewa kwa vifaa hivyo lakini mafunzo ya namna ya kutumia vifaa hivyo ni muhimu kuzingatiwa ili vifaa hivyo viweze kufanyakazi zilizokusidiwa kwa ufanisi na kwa muda mrefu.

Awali wakati akimkaribisha Waziri wa Ujenzi, Mtendaji Mkuu wa TEMESA Injina Marcellin Magesa alimshukuru Waziri wa Ujenzi kwa kuweza kutoa kipaumbele kwa Taasisi hiyo na kuitengea fedha zilizowezesha kupatikana kwa vifaa hivyo katika kipindi hiki muafaka kwani karakara nyingi tayari zilikuwa katika hali mbayo kutokana na kukosa vitendeakazi.

No comments: