Saturday, October 12, 2013

WADAU MBALIMBALI WA LAPF WAZAWADIWA KWA MICHANGO YAO KWA MFUKO HUO














 



HOTUBA YA WAZIRI WA NCHI OFISI YA WAZIRI MKUU TAMISEMI MHE. HAWA ABDULRAHAMAN GHASIA WAKATI WA KUFUNGUA MKUTANO MKUU WA SITA WA WADAU WA LAPF TAREHE 11/10/2013 KATIKA UKUMBI WA KIMATAIFA WA MIKUTANO (AICC) – JIJINI ARUSHA

Mheshimiwa Gaudencia Kabaka, Waziri wa Kazi na Ajira
Mkuu wa Mkoa wa Arusha;
Manaibu Mawaziri mlioko hapa;
Waheshimiwa Wabunge;
Makatibu Tawala wa Mikoa na Makatibu Wakuu mlioko hapa;
Mwenyekiti na Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya LAPF;
Mkurugenzi Mkuu wa LAPF;
Viongozi wa Wizara, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makampuni, Mashirika na Taasisi mbalimbali mnaochangia LAPF;
Wageni toka Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ndani na nje ya nchi,
Wanahabari, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana. 
Nianze kwa kukushukuru Mwenyekiti wa Bodi, Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini pamoja na Menejimenti ya LAPF kwa kunikaribisha kwenye mkutano wenu huu lakini pia niwapongeze sana kwa maandalizi mazuri ambayo sote tumeyaona.

Ndugu Washiriki, tumesikia maelezo toka kwa Mwenyekiti wa Bodi kuhusu masuala ya kisera na mwelekeo wa Mfuko lakini pia tumesikia toka kwa Mkurugenzi Mkuu Bwana Sanga kuhusu maendeleo ya LAPF kwa mwaka 2012/2013.  Nawapongeza sana kwa mafanikio makubwa mliyopata na nasema jitihada hizo ziongezeke ili wanachama wenu na wananchi wengine waweze kunufaika zaidi.

Ndugu Washiriki, mkutano huu ni muhimu sana kwani ndio mkutano pekee katika mwaka unaowakutanisha ninyi na hivyo kuwapa fursa ya kujadili hoja mbalimbali toka LAPF.  Ni fursa pia kwenu kuweza kuueleza uongozi mambo ambayo mngependa Mfuko ufanye kwa manufaa yenu na wananchi kwa ujumla.  Hivyo tutumie vizuri sana siku hizi mbili za mkutano kuibua maazimio ambayo ninyi pamoja na Mfumo mtaenda kuyafanyia kazi.

Tumeambiwa kuwa kauli mbiu yetu ni Kutosheleza kwa mafao ya Kustaafu: Changamoto na Njia za Kuboresha.  Kauli mbiu hii ni muhimu sana ikajadiliwa kwa kina kwa matokeo ya mjadala wake itatupa mwelekeo wa nini kifanyike kuboresha zaidi mafao ya wanachama wa Mfuko.  Ni kweli kabisa wapo wastaafu wetu wamepata fedha nyingi sana lakini ndani ya mwaka mmoja au miwili fedha hizo zinakuwa zimekwisha na hakuna jambo la msingi walilofanya.

Inaonyesha dhahiri kuwa nidhamu ya utunzaji fedha kwa watumishi na wastaafu wengi ni tatizo.  Ni vizuri eneo hili likajadiliwa kwa kina na mkaondoka hapa na maazimio ya kurekebisha dosari hii.  Najua kuwa uongozi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Hifadhi ya Jamii uko hapa.  Naomba mtumie nafasi hii kuona namna ambavyo mnaweza kuboresha sekta hii ili iwanufaishe walengwa zaidi.

Nimeambiwa pia kuwa ipo mada kwa ajili ya mbinu za ujasiriamali.  Tupende tusipende ujasiriamali haukwepeki kama tunataka kumaliza sehemu yetu ya maisha kwa furaha na amani.  Kila shughuli utakayoifanya baada ya kumaliza utumishi wako ni ujasiriamali na shughuli hiyo itakuwa na manufaa kwako endapo utakuwa umeifanyia maandalizi ukiwa bado kazini.  Wale wanaokimbilia kujifunza biashara kwa mfano ya  daladala baada ya kustaafu kimsingi wanajitafutia matatizo.  Sio biashara nyepesi kama wanavyofikiri ila ni rahisi endapo imefanyiwa utafiti wa kutosha juu ya namna ya kuisimamia.  Hivyo naona Mfuko umefanya jambo la msingi sana kuleta mada hii hapa.  Aidha, nashauri isiishie hapa ila nanyi mhakikishie kuwa watumshi wengine walio kule maofisi wanapata taaluma hiyo japo kwa uchache.

Ndugu Washiriki, katika sekta hii ya hifadhi ya jamii huduma bora ni jambo muhimu mno. Wastaafu wengi wanasumbuka kupata mafao yao wanakuwa wamestaafu.  Leo nafurahi kusikia na kuona kuwa LAPF sasa inaweza kulipa wanachama wake kabla au katika siku ya kustaafu.  Hili ni jambo zuri nami nashauri waajiri mlichukue kwa umuhimu wake kwa kuhakikisha wale wanaokaribia kustaafu maombi yao yanawasilishwa LAPF angalau miezi mitatu minne kabla ya tarehe ya kustaafu ili Mfuko uweze kufanya malipo kama tulivyoona leo hapa.  Huduma bora ni kivutio kikubwa cha wanachama hivyo mkiendelea na kasi hiyo hakika mtapata wanachama wengi zaidi.
Ndugu Washiriki, nitoe rai kwa Mfuko wa LAPF kufanya kazi moja.  Angalieni uwezekano wa kutoa “Guarantee” kwa wanachama wenu ili wapewe mikopo na mabenki.  Hii itasaidia kukuza mitaji yao na kuzalisha zaidi, hivyo kua na uwezo wa kuchangia zaidi katika mfuko.  Ni matumaini yangi likifanyiwa kazi jambo hili linaweza likawa ni fursa kwa Mfuko na wanachama pia.

Mwaka jana tulizungumza kuhusu uwezekano wa kutoa mikopo ya elimu kwa wanachama wa Mfuko.  Leo mmesema kuwa jambo hili sasa liko kwa mtathmini wa Mfuko.  Naomba liharakishwe kwani nina uhakika wanachama wenu wanalisubiri kwa hamu kubwa sana.

Ndugu Washiriki, nikirudi sasa kwenu, nawaomba sana mtimize wajibu wenu kwa kuwasilisha michango kwa wakati.  Michango hii inahitaji kuwekezwa kwa wakati ili kuujengea Mfuko uwezo wa kuboresha zaidi mafao ya wanachama wenu.  Sasa inapocheleweshwa ni hatari mfuko kupoteza mapato na hivyo uwezo wa kuboresha zaidi mafao.

Ndugu Washiriki, Sheria ya Mamlaka imetoa uhuru wa watumishi wapya kuamua Mfuko wanaoupenda, hii ni njia nzuri ya kujenga mazingira ya ushindani na kuhakikisha kila mfuko unaboresha huduma zake na mafao yanayotolewa ili kuweza kupata wanachama zaidi.  Waajiri mnapaswa kutoa fursa kwa mifuko kujieleza mbele ya watumishi wapya kila mnapowaajiri ili wafanye maamuzi sahihi kuhusu mfuko wanaotaka.  Naomba kusiwe na upendeleo au mizengwe ya aina yoyote katika eneo hili.

Aidha, wanachama mnaofaidi na mikopo ya LAPF kupita SACCOS zenu muendelee kurejesha fedha husika kwa wakati na pia muwe na mipango madhubuti ya kuitumia mikopo hiyo ili ionekane kuwa na manufaa kwenu na kuwaletea maendeleo. Nashauri LAPF na Mifuko mingine muwaelimishe wanachama wenu jinsi ya kusimamia mikopo hiyo ili iwe na tija kwao.

Mwisho napenda kuwashukuru tena kwa kunipa heshima hii na kuipongeza kwa dhati Bodi ya Wadhamini na Uongozi wa LAPF kwa kazi yenu nzuri.  Nasema endeleeni na kazi hiyo kwa manufaa ya wanachama na Taifa kwa ujumla.  Baada ya kusema hayo machache sasa natamka kuwa mkutano wa sita wa Wadau wa LAPF mwaka 2013 umefunguliwa rasmi.
 ASANTENI SANA


No comments: