Monday, March 11, 2013

UMOJA WA MATAIFA WAISHUKURU TANZANIA



Na Mwandishi Maalum
Umoja wa  Mataifa umeishukuru Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutoa eneo la ujenzi wa  majengo mapya ya  Kimataifa  yatakayotumika  kushughulikia Mashauri Masalia ya  Mahakama ya Kimataifa ya   makosa ya Jinai  Tawi la Arusha. ( International Residual  Mechanism)
Majengo  hayo ambayo ujenzi wake  utagharamiwa na  Umoja wa  Mataifa, yatajengwa katika eneo la Laki Laki katika  Jiji la Arusha.  Yatahusisha pia  uhifadhi wa nyaraka na  kumbukumbu zote muhimu zinazohusiana na  Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji  ya Kimabari ya Rwanda ( ICTR).
 Shukrani hizo zimetolewa  mwishoni mwa wiki,na Mkurugenzi wa Idara ya  Mipango na Kitengo  cha Bajeti cha Umoja wa Mataifa,   Bw. Johannes Huisman, wakati alipokuwa akiwasilisha  mbele ya  wajumbe wa Kamati ya Tano ya Baraza  Kuu la Umoja wa Mataifa, taarifa ya  Katibu Mkuu ,  kuhusu  mchakato wa ujenzi wa majengo hayo  mapya ya Kimataifa.
Kamati ya Tano ndiyo Kamati  inayoshughulikia masuala  yote yanayohusu  na Utawala na Bajeti  katika  Umoja wa Mataifa.
“  Ninanayo furaha  ya   kuiwasilisha kwenu  taarifa  ya Katibu Mkuu, kama taratibu zinavyoagiza.  Lakini kwanza ninapenda kuchukua fursa hii kuishukuru Tanzania kwa kutupatia eneo hilo na vile vile   kwa ushirikiano  ambao serikali inaendelea kutupatia hadi sasa katika  maandalizi ya  utekelezaji wa mradi huu” akasema Bw. Huisman.
 Kwa mujibu kwa Mkurugenzi  huyo,  tayari Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, limekwisha kutenga  kiasi cha dola za kimarekani 3 milioni   za kuanzia ujenzi huo unaotarajiwa  kugharimu   dola  za kimarekani 8.79 milioni
Bw. Johannes Huisman akafafanua zaidi kwa kusema   kumekuwa na  maendeleo kadhaa kuhusiana na utekelezaji wa mradi  tangu kuwasilishwa kwa taarifa ya mwisho  ya Katibu Mkuu  iliyotolewa mwaka jana.
Akazitaja baadhi ya kazi ambazo zimekwisha kufanyika kuwa ni pamoja na mambo mengine, kupatikana kwa eneo la ujenzi , maandalizi ya michoro ya majengo,  upembuzi yakinifu wa  gharama za mradi pamoja na  ratiba ya ujenzi  hadi kukamilika kwa  mradi huo.
“Ninapenda kueleza kwamba  katika  mambo yaliyofanyika  ni pamoja na hili la  kupunguza  muda wa ujenzi wa  mradi  kutoka makadirio ya awali ya miaka  mitano na miezi mitatu hadi miaka minne, matarajio  ni kwa mradi huo  ukamilike   mwishoni mwa mwaka 2015.” Akaeleza.
Naye   Makamu Mwenyekiti wa  Kamati ya Ushauri kuhusu masuala ya Utawala na  Bajeti ( ACBQ), Bw. Richard Moon  akiwasilisha  maoni ya kamati yake kuhusu mradi huo  alieleza kwamba, kamati yake imeridhishwa na  kwanza,  kupunguzwa kwa muda wa utekelezaji wa maradi na pili uamuzi wa kutumia uzoefu uliopo katika  uandaaji wa michoro ya majengo hayo.
Aidha akaeleza kwamba pamoja na kuridhika na maelezo yote kuhusu mradi huo lakini  Kamati imegundua kwamba gharama za ujenzi huo zilikuwa hazijahusisha gharama za  ununuzi wa samani za majengo hayo.
 Na kwa sababu hiyo alibainisha kwamba kamati itahitaji  ufafanuzi kuhusiana na  walakini huo pamoja na  swala la  kutoingizwa  kiasi cha  dola za kimarekani 1.5 milioni katika  taarifa hiyo ya Katibu Mkuu
Aidha akizungumza kwa  niaba ya Kundi la  Nchi 77 na China ( G77),  Bw. Sainivalati Navoti, aliunga mkono hoja ya kutaka maelezo ya kwa nini kiasi hicho cha dola  za kimarakani 1.5 milioni zilikuwa  hazijaainishwa katika ripoti hiyo.
Kundi hilo la G77  pia limeunga mkono punguzo la  muda wa ujenzi wa mradi  na likaenda mbali zaidi kwa kushauri kwamba hata miaka hiyo minne  bado ni  mingi na  ikiwezekana  ipunguzwe hadi miaka mitatu lakini bila kuathiri ubora na viwango vya mradi huo.
Bw. Brouz Coffi akizungumza kwa niaba ya kundi la nchi za Afrika, alisema Kundi la nchi za Afrika linaunga mkono utekelezaji wa mradi huo nchini Tanzania na kwamba hamu ya kundi hilo nikuona unatekelezwa kwa wakati na kwa  ubora unaotakiwa.
Akaishukuru  Serikali ya Tanzania kwa kutoa  eneo la Ujenzi, na kusisitiza kwamba Umoja wa Mataifa uendelee kushirikiana na kufanya kazi kwa karibu na Mamlaka za Tanzania na  kusisitiza zaidi kwamba  badiliko lolote litakalogusa mradi huo lazima lijadiliwe na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kama taratibu zinavyotaka..
Mwaka 2010, Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, lilipitisha Azimio namba 1966  la kuanzisha Mfumo wa Kimataifa wa kushughulikia umalizaji wa mashauri ya masalia ya mahakama za kimataifa za mauaji ya  halaiki  ya   iliyokuwa Yugoslavia ya Zamani,  (ICTY) na mauaji ya kimbari ya  Rwanda( ICTR.)
Kwa upande wa ICTY  tawi la mahakama hiyo litakuwa  The Hague, Uholanzi na ICTR iliamuliwa  tawi lake litakuwa Arusha, Tanzania.  Mfumo huo wa kimataifa wa kushughulikia mashauri masalia utakuwa na haki , stahili na wajibu kama ilivyo kwa mahakama hizo ambazo zinatarajiwa kukamilisha kazi zake si zaidi ya Desemba 31, 2014.

No comments: