Tuesday, January 15, 2013

Kilimo Kwanza ni moja ya vipaumbele vyetu—Dkt. Turuka


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na technolojia, Dkt. Florens Turuka akisisitiza jambo kwa waandishi wa habari, Jijini Dar es Salaam jana, namna wizara yake ilivyojipanga katika utekelezaji wa dhana ya kilimo kwanza.

Na Mwandishi wetu, Dar es Salaam

Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia imesema mkakati wa Kilimo Kwanza unaolenga kufikia mapinduzi ya kijani Tanzania ni moja vipaumbele vyake katika juhudi za kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Hii ni kwa sababu sekta hiyo ya kilimo inabeba maisha ya watu wengi hapa nchini na ikiendelezwa vizuri ina uwezo wa kubadilisha maisha ya wananchi wengi katika nchi hii ambayo ina ardhi kubwa yenye kufaa kwa kilimo.

“Tumejipanga kutumia fungu la serikali kwa ajili ya utafiti na maendeleo kusaidia tafiti zitakazosaidia maendeleo ya wananchi na taifa kwa ujumla na Kilimo Kwanza ni moja ya vipaumbele vyetu,” Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Florens Turuka aliwaambia waandishi wa habari jana.

Kilimo Kwanza ni mkakati wa serikali unaolenga kutumia kilimo kama daraja la kufikia mapinduzi ya uchumi hapa nchini kwa kukigeuza kilimo kuwa cha kisasa zaidi kwa faida ya watanzania na taifa lote kwa ujumla zikihusishwa sekta binafsi na ile ya umma.

“Tumeamua kutumia fedha hii ya serikali inayolenga utafiti na maendeleo kusaidia tafiti zinazolenga kufanikisha Kilimo Kwanza,” alisema Dkt. Turuka.

Aliyataja baadhi ya maeneo ambayo yanapewa kipaumbele kama utafiti kuhusu pembejeo na masoko ya mazao.

“Unatakiwa kuwa na soko la uhakika ili kufanikiwa katika kilimo,” alisema, na kufafanua kwamba unaweza kuwa na mazao mengi lakini kama huna soko la uhakika inakua haina faida sana.

Alieleza kwamba hii ndio sababu Wizara yake imeamua kusaidia tafiti zinazolenga kuibua fursa za masoko kwa faida ya watanzania na wadau wote wanaojihusisha na kilimo.

Aliyataja maeneo mengine yanayolengwa kama tafiti zinazohusiana na kuimarisha mnyororo ya thamani na kuongeza bidhaa za kulimo thamani.

Takwimu zinaonyesha kwamba nchi zilizoendelea hutumia hadi dola za kimarekani 180 kuongeza thamani tani moja ya mazao wakati nchi zinazoendelea hutumia dola 40 tu kuongeza thamani katika tani moja ya mazao ya kilimo.

“Eneo hili la kuongeza thamani mazao ni la muhimu sana kufanyia utafiti zaidi…ndio maana tunalipatia kipaumbele,” alisema.

Kwa mujibu wa wataalamu, bado kilimo cha Tanzania kinategemea sana wakulima wadogowadogo na kinachangia asilimia 50 ya pato la taifa na kuendesha maisha ya asilimia 80 ya wananchi wote.

No comments: