Thursday, October 18, 2012

TUNAWEZA KUITOKOMEZA MALARIA- MAHADHI JUMA MAALIM



Na Mwandishi Maalum
Naibu  Waziri wa Mambo ya Nje na  Ushirikiano wa Kimataifa,  Mahadhi Juma Maalim (Mb)pichani juu,  ameliambia Baraza Kuu la 67 la Umoja wa Mataifa, kwamba Tanzania na Afrika kwa ujumla iko katika mwelekeo mzuri wa kuutokomeza ugonjwa wa malaria licha ya changamoto mbalimbali.
Ameyasema hayo siku ya jumatano wakati Baraza  Kuu lilipokuwa likijadili   ajenda tatu ambazo zilihusu ni  Muongo wa kutokomeza Malaria katika nchi za Afrika, taarifa ya  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Ushirikiano  Mpya wa  Maendeleo ya Kiuchumi ( NEPAD) kati ya Umoja wa Mataifa na Afrika na chanzo za migogoro Barani Afrika na  uimarishaji wa  amani ya kudumu.
Katika majadiliano hayo ambayo yalifunguliwa na Rais wa Baraza hilo, Bw. Vuk Jermic, Naibu  Waziri anasema katika  kuukabili ugonjwa wa malaria,   serikali nyingi za  Afrika  ikiwamo ya Tanzania  zinatambua   njia zipi zinafanya kazi katika kuukabili ugonjwa huo na ni  njia   zipi hazifanyi kazini.
Kwa mfano anasema, Tanzania bara na visiwani   imefanikiwa katika kuhakikisha pamoja na mambo mengine  kwamba, vyandarua vyenye viatilifu siyo tu vinapatikana lakini pia vinapatikana kwa bei nafuu kwa kuondoa kodi  mbalimbali.
“ Serikali yangu ilifanya maamuzi ya makusudi kabisa  ya kuhakikisha kwamba inagawa bure  vyandarua vyenye viatilifu, mpango huu ambao unakwenda sambamba na uangamizaji wa mazalia ya mbu,  upatikanaji wa kinga  na  huduma za upimaji na matumizi ya dawa mseto za malaria, mbinu hizi zote zimesaidia sana katika kupunguza idadi ya kesi za  malaria na hata vifo vitokanavyo na ugonjwa huo.” Akaeleza.
Akatumia fursa hiyo kuzihimiza serikali za nchi nyingine kuiga mfano wa Tanzania hasa katika kupunguza au kuondoa  kodi na ushuru kwenye vyandaru na bidhaa nyingine zinazohitajika katika kuudhiti ugonjwa, kupunguza bei  ya bidhaa hizo kwa watumiaji na kuboresha biashara huru.
“Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza katika Afrika kufanya hivyo, kwa kuondoa   kodi  na ushuru imesaidia kupunguza muda wa uagizaji wa bidhaa hizo na kuwapo kwa   unafuu kwa sekta za umma na binafsi. Faida ya kiafya iliyopatika kwa kutumia utaratibu huu ni kubwa mno ikilinganishwa na  mapato tuliyopoteza” akasisitiza Naibu Waziri.
  Hata hivyo akasema, licha ya mafanikio chanya ambayo yamekwisha kupatikana kupitia mbinu hizo na nyingine, bado kunachangamoto kadhaa.
“ Hapana shaka kwamba vita dhidi ya malaria inahitaji mambo mawili, uongozi na raslimali.  Viongozi wa Afrika kupitia  Muungano wao dhidi ya  Malaria ( ALMA) wameonyesha uongozi wa pamoja wa kuukabili ugonjwa huu. Hata hivho wanakabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa raslimali. Sote tunafahamu kuwa ugonjwa  wa malaria unatibika lakini mkazo wetu umekuwa katika kuudhibiti kwa sababu ndiyo njia nafuu na rahisi” akaeleza Naibu Waziri
Na kuongoza kwamba matibabu sahihi na kamili ya  ugonjwa huo na kuwepo wa miundombinu ya kuutibu  ikiwa ni  pamoja na  uwepo wa vituo vya afya kwa umbali mfupi vikiwa na wataalamu  wakutosha wa afya ni njia sahihi zaidi.
Lakini anasema Naibu Waziri  “ Hapa ndipo hasa penye tatizo,  karibu serikali zetu nyingi hususani katika nchi zinazoendelea hazina uwezo wa kuwakikishia wananchi wao  upatikanaji wa huduma hizo na hasa katika maeneo ya vijijini ambako wananchi wengi wanaugua malaria bila wao wenyewe kutambua kwamba wanaugua ugonjwa huo”.
Na kwa sababu hiyo, Naibu Waziri  Mahadhi amezitaka nchi zilizoendelea  ikiwa ni pamoja na  Umoja wa Mataifa kuendelea kushirikiana kwa karibu na   Viongozi wa Afrika ili hatimaye ugonjwa huu uweze kutokomezwa au kupunguzwa kabisa Barani Afrika ifikapo 2015.
Baadhi ya wachangiaji wa ajenda hiyo ya   Malaria,  akiwamo Naibu Waziri  Mkuu  na Waziri wa  Mambo ya  Nje wa  Luxembourg, Bw. Jean Asselborn  yeye  ameeleza kwamba nchi yake imekuwa  ikishirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) ambapo nchi hiyo inafadhili  shughuli mbalimbali za kupambana na Malaria,  na utafiti wa magonjwa mengine ya kitropikali  maeneo ambayo kila mwaka imekuwa ikichangia euro milioni tatu.
Aidha akasema mchango wao wa hiari katika Mfuko wa Kupambana na  Ukimwi,  Kifua Kikuu na   Malaria bajeti yake inafikia euro milioni 2.5
“ Tunahitaji kuwa wabunifu zaidi na siyo tu pale inapokuja katika kufadhili upatikanaji wa huduma za kuudhibiti na kuutibu ugonjwa wa malaria, lakini pia katika  kutopoteza mwelekeo na  kuwa na  mtazamo mpana zaidi wa kuimarisha mifumo wa kitaifa wa huduma za afya ili  iwe endelevu” akasisitiza   Naibu Waziri  Mkuu na  Waziri wa Mambo ya Nje, Jean Asselborn..

No comments: