Friday, January 4, 2019

MAKAMBO AENDELEZA WEMBE WAKE, ACHAGULIWA MCHEZAJI BORA WA MWEZI DISEMBA

Na Zainab Nyamka, Globu ya Jamii 

MSHAMBULIAJI wa kimataifa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wa timu ya Yanga Heritier Makambo amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Desemba wa Ligi Kuu Tanzania Bara (TPL) msimu wa 2018/2019 ikiwa ni mara ya pili mfululizo. 

Makambo , alitwaa tuzo hiyo baada ya kuwashinda wenzake wawili, Miraji Athumani wa Lipuli ya Iringa na Idd Selemani wa Mbeya City alioingia nao fainali katika uchambuzi uliofanywa Dar es Salaam wiki hii na Kamati ya Tuzo ya TPL. 

Kwa mwezi huo wa Desemba, Yanga ilicheza michezo mitano, ambapo Makambo alitoa mchango mkubwa kwa Yanga kupata pointi 15 ikishinda michezo yote mitano iliyocheza, huku mshambuliaji huyo akitoa mchango mkubwa kwa timu yake ikiwa ni pamoja na kufunga mabao manne. 

Kwa upande wa Miraji Athumani alikuwa na mchango mkubwa katika mafanikio ya timu ya Lipuli kwa mwezi huo, ambapo timu yake ilicheza michezo minne ikishinda mitatu na kutoka sare mmoja ikijikusanyia pointi 10 na kupanda kutoka nafasi ya 14 hadi ya nane, huku Idd Selemani naye alionesha uwezo wa hali ya juu kwa timu yake ya Mbeya City kwa mwezi huo. 

Pia Kamati ya Tuzo, imemchagua Kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera kuwa Kocha Bora wa mwezi Desemba akiwashinda Kocha Mkuu wa Lipuli, Samuel Moja na Kocha Mkuu wa Kagera Sugar Mecky Maxime aliongia nao fainali. Zahera aliiongoza timu yake katika michezo minne kati ya mitano iliyocheza, ambayo Yanga ilishinda michezo yote mitano na kuvuna pointi 15 hivyo kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi ikipanda kutoka nafasi ya pili. 

Kwa upande wa Moja yeye aliiongoza timu yake katika michezo yote minne iliyocheza ikishinda mitatu na kutoka sare mmoja, wakati Maxime aliiongoza Kagera Sugar katika michezo yote mitatu iliyocheza ikishinda miwili na kutoka sare mmoja. 

TFF ina utaratibu wa kuwazadiwa wachezaji bora wa kila mwezi, huku pia mwisho wa msimu kukiwa na tuzo mbalimbali zinazohusu ligi hiyo, ambapo msimu wa mwaka 2017/2018 kulikuwa tuzo 16 zilitolewa kwa washindi wa kada mbalimbali, ambapo kwa ushindi huo Makambo atazawadiwa tuzo, king’amuzi kutoka Azam na Sh milioni moja. 

Washindi wengine wa tuzo hiyo kwa msimu huu na miezi yao katika mabano ni mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere (Agosti), mshambuliaji wa Mbeya City, Eliud Ambokile, mshambuliaji wa Simba Emmanuel Okwi (Oktoba) na Makambo (Novemba). 

Kwa upande wa makocha walioshinda tuzo hizo kwa msimu huu ni Amri Said wa Mbao FC (Agosti), Mwinyi Zahera wa Yanga (Septemba), Hans Pluijm wa Azam (Oktoba) na Zahera (Novemba). 


MSHAMBULIAJI wa kimataifa raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wa timu ya Yanga Heritier Makambo ambaye amechaguliwa kuwa Mchezaji Bora wa mwezi Desemba wa Ligi Kuu Tanzania Bara (TPL) msimu wa 2018/2019 ikiwa ni mara ya pili mfululizo.

No comments: