Saturday, December 1, 2018

SERIKALI YAWATOA WASIWASI WAFANYABIASHARA WA UGANDA

Serikali imewahakikishia wafanyabiashara wa mafuta kutoka uganda kuwa imejipanga kutatua  changamoto zote zilizopo kwenye usafirishaji ili kupunguza gharama za uchukuzi  kati ya Tanzania na nchi hiyo. Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, amesema hayo wakati wa kikao maalum kilichowakutanisha wafanyabiashara wa Mafuta wa Uganda na taasisi za Uchukuzi za Tanzania na kusema kuwa Serikali inatekeleza hayo kwa kuboresha miundombinu ili kuvutia wafanyabiashara wengi zaidi

“Niwahakikishie kuwa changamoto zote zilizoainishwa baada ya majumuisho ya ziara yenu ya siku 5 nchini tutazifanyia kazi", amesema Naibu Waziri  Nditiye. Aidha, Naibu Waziri Nditiye ameongeza kuwa Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ikiwemo upanuzi wa bandari,ukarabati wa reli na ukarabati wa meli ili mizigo inayokwenda Uganda kupitia bandari ya Dar es Salaam ifike kwa wakati.

Kwa upande wake Meneja Mkuu wa Kampuni ya Meli, Eric Hamis amesema mpaka sasa tayari wamesafirisha zaidi ya tani elfu kumi na tano za Uganda kwa kutumia meli ya MV Umoja na kusema kuwa wamejipanga kusafirisha mzigo mkubwa zaidi kabla ya mwaka wa fedha kuisha. Sisi kama Kampuni ya meli tuliifanyia ukarabati meli ya MV Umoja na imekuwa ikisafirisha mzigo wa Uganda na niwahakikishie kuwa kupitia ziara hii na jitihada nyingine tunazozifanya tutapata wafanyabishara wengine ambao watasafirisha mizigo yao kwa kutumia meli hii” amesema Hamis.

Kwa upande wake Mchumi Mwandamizi kutoka Wizara ya Ujenzi ya Uganda,  Gerald Akini,  amemwahidi Naibu Waziri Mhandisi Nditiye kuwa yale ya kisera yanayohusu Uganda atayafikisha katika ngazi husika ili yafanyiwe kazi ili kuimarisha ushirikiano uliopo kibiashara. Bw Gerald ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa utayari wake wa kuwapokea wafanyabiashara na kuweka mazingira mazuri ili watumie bandari ya Dar es Salaam.

Aidha, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha miundombinu ikiwemo kupunguza vituo vya mizani,ujenzi wa reli ya kisasa,uboreshaji wa bandari na kuahidi kuendeleza ushirikiano kwa kushawishi wafanyabiashara wengi zaidi kutumia bandari ya Dar es salaam. Wafanyabiashara wa mafuta kutoka nchini Uganda wamefanya ziara ya siku 5 nchini ambapo wametembelea bandari ya Dar es salaam, Tanga,Mwanza pamoja na kukagua miundombinu ya reli na meli za kampuni ya meli na kuridhishwa na hatua zinazochukuliwa na Tanzania kuimarisha biashara baina ya nchi hizo.


Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Atashasta Nditiye, akiwa katika picha ya pamoja na wafanyabiashara wa mafuta wa Uganda mara baada ya kukutani nao jijini Mwanza.

No comments: