Friday, November 23, 2018

Hasunga kufungua mkutano wa Baraza la Kilimo Tanzania.




Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi ya Baraza la Kilimo Tanzania Dkt Sinare Yusuph Sinare akisisitiza jambo wakati wa kikao cha siku mbili cha Bodi ya wakurugenzi wa Baraza la Kilimo, kulia kwake ni Makamo Mwenyekiti Bi Jacqueline Mkindi .
Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Kilimo Tanzania Bi Janeth Bitegeko akiwa katika moja ya vikao vya Bodi ya wakurugenzi ya Baraza la Kilimo Tanzania. 




Waziri wa kilimo Nchini Mh Japhet Hasunga anatarajia kufungua Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Kisera wa Baraza la Kilimo Tanzania unaotarajiwa kufanyika Nov 26 na 27 mwaka huu jijini Dra es salaam wenye lengo kukusanya maoni ya yahusuyo Sera za Kilimo ili kuona namna zinavyoweza kufanyiwa marekebisho.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Kilimo Tanzania Bi Janeth Bitegeko imesema mkutano huo wenye kauli mbiu ya Kilimo na Maendeleo ya Viwanda Tanzania unatarajiwa kuhudhuliwa na wadau wa sekta ya kilimo zaidi ya 100 kutoka ndani na nje ya nchi.

Bi Janeth alitaja mada zitakazowalishwa katika mkutano huo kuwa ni apmoja na mada kuu ya Kilimo na Maendeleo ya Viwanda Tanzania, Fursa ya Sekta Binafsi Katika Utekelezaji wa ASDP II, Nafasi ya Vijana na Utekelezaji wa ASDP II ikiwa ni pamoja na Kuimarisha Ushirika kwa Faida ya Wazalishaji.

“ Kwetu Baraza la Kilimo Mkutano huu ni muhimu kwa sababu ndiko tunapopata changamoto za kisera zinazowakabili wadau wa kilimo nchini na kwenda kukaa meza moja na serikali na kuzifanyia kazi, ndio maana utaona tumewaalika wadau wote wa kilimo nchini,

“ Na tumegusa wadau wote wanaojihusisha na mboga mboga, maziwa, mifugo kwa ujumla, kilimo , Uvuvi na yeyote anayeguswa na sekta nzima ya kilimo tunaamini kwa kuwaweka pamoja wote hawa tutatoka na maazimio mazuri yatakayolenga kuendelea kuiboresha sekta ya kilimo nchini” alisema Bi Janeth Bitegeko Mkurugenzi Mtendaji Baraza la Kilimo Tanzania.

Katika mkutano huo na vyombo vya habari ofisini kwake aliongeza kuwa “ Mambo yote yatakayojadiliwa katika mkutano huu ndio kipaumbele chetu kwa mwaka ujao 2019, kwasababu tumekuwa tukiyafanyia kazi na kumekuwa na matokeo chanya kwasababu sisi tumekuwa tukifanya kazi na serikali kwa karibu zaidi ndio maana unaona masuala mengi yaliyokuwa changamoto kwa wakulima kama vile tozo serikali imekwisha kuyafanyia kazi”.



“Katika Mkutano huu pia tutatoa mrejesho wa yote yaliyoibuliwa katika Mkutano wa Mwaka jana 2017, lakini pia tutatoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Baraza la Kilimo kwa mwaka mzima, hii pia itakuwa ni fursa pekee kwa wanachama wa baraza kujua nini kilifanyika kwa mwaka mzima”.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Baraza la Kilimo Tanzania Bw Timothy Mmbaga aliwaeleza wanahabari kuwa maandalizi yote ya Mkutano huo yamekwisha kukamilika na tayari Waziri wa Kilimo Mh Japhet Hasunga amethibitisha kushiriki katika mkutano huo wa Nov 26 nq 27.

“Baraza la Kilimo limekuwa likifanya kazi na taasisi pia za kimataifa kama .SACAU na EAFF nao pia wamekwisha kuthibitisha kushiriki mkutano huu, kwahiyo ni rai yangu kwa wadau wengine wa kilimo kushiriki mkutano huu muhimu kwa sababu ndio nafasi pekee ya wao kusema sera zipi kwao ni kikwazo na wangependa serikali izifanyie kazi ili kuzidi kuiimarisha sekta ya kilimo nchini ” alisema Bw Mmbaga.

Aidha ilielezwa kuwa mafanikio makubwa yaliyokwisha kufikiwa na Baarza la Kilimo Tanzania yametokana na mikutano ya kisera ambapo kupitia mikutano hiyo mambo kadha wa kadha yalifikiwa na wadau wa kilimo na baadae serikali kuyafanyia kazi.



“Unajua sisi kama Baraza la Kilimo tunajifunia kuwa vinara kwa sababu nini sisi tulioshawishi hadi kuanzishwa Banki ya Kilimo Tanzania na mnaona inavyofanya kazi, ni sisi pia tulioshawishi hadi serikali ikaja na Kilimo Kwanza lakini pia ni sisi Baraza la Kilimo tulihakikisha SAGCOTT inaanzishwa,

“ Kwa hivyo unaweza kuona nguvu ya ushawishi tuliyonayo lakini yote haya yanawezakana kupitia mikutano kama hii ya kisera kwa sasa sisi kama Baraza tunaamini katika ushirikishwaji na ndio maana tumekuwa tukifanikiwa katika masuala mengi yanayohusu sekta yetu ya Kilimo” alisema Mkurugenzi Mtendaji wa Bazaar la Kilimo Bi Janeth Bitegeko.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya wakurugenzi ya Baraza la Kilimo Tanzania anayemaliza muda wake Dkt Sinare Yusuph Sinare alisema kwa muda wote ambao amehudumu katika nafasi ya uenyekiti wa Bodi, mikutano ya kisera imekuwa na manufaa makubwa na wamefanikiwa kuweza kufanyia kazi changamoto zote zilizokuwa zikiibuliwa na wadau wa kilimo

“ Kimsingi naondoka kwenye nafasi ya uenyekiti nikiwa sina shaka kabisa na uwezo wa Baraza la Kilimo Tanzania katika kushughulikia changamoto hasa za kisera zinazoikabili sekta ya kilimo kwa hivyo naamini hata yatakayojili katika mkutano wetu wa Nov 26 na 27 pia yatafanyiwa kazi kwa umahili uleule” alisema Dkt Sinare anayetarajiwa kumaliza muda wake katika mkutano mkuu wa Baraza la kilimo utakaofanyika Nov 28 mwaka huu..

Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Baraza la Kilimo Tanzania miongoni mwa wadau wa kilimo watakaoshiriki mkutano huo kutoka ndani na nje ya nchi ni pamoja na Shirikisho la Vyama vya Wakulima vya Afrika ya Mashariki, Muungano wa Vyama vya Wakulima Kusini mwa Afrika ikiwa ni pamoja na Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania.

No comments: